Rais Kikwete afungua mkutano wa Maendeleo ya Kilimo Barani Afrika

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akisisitiza jambo wakati akifungua Mkutano wa kuzungumzia Mustakabali wa maendeleo ya Wakulima Barani Afrika uliofanyika katika hoteli ya White Sands jijini Dar es Salaam leo.mkutano huo umeandaliwa na asasi ya(The southern African Confederation of Agriculktural Unions(SACAU).Wapili kushoto ni Kaimu Rais wa SACAU Bwana Ishmael Sunga na Watatu kushoto ni Waziri wa Kilimo Christopher Chiza.
Baadhi ya wajumbe waliohudhuria Mkutano utakaojadili Mustakabali wa Maendeleo ya Wakulima Barani Afrika uliofanyika katika hoteli ya White Sands jijini Dar es Salaam ambao umendaliwa na asasi ya SACAU(The Southern African Confederation of Agricultural Unions).(picha na Freddy Maro).

RAIS KIKWETE AZINDUA KITUO CHA TAASISI YA KIMATAIFA YA KILIMO CHA KITROPIKI (IITA) DAR ES SALAAM

Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chifu Olesegun Obasanjo akihutubia wakati wa uzinduzi wa jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.
 
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo na Rais Mstaafu wa Tanzania Mzee Benjamin William Mkapa wakionja mikate iliyotengenezwa kwa unga wa muhogo wakati wa uzinduzi wa jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na mazungumzo na Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo baada ya uzinduzi wa jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.
 
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo na Rais Mstaafu wa Tanzania Mzee Benjamin William Mkapa
wakisikiliza maelezo ya kitaalamu juu ya utafiti wa maradhi ya migomba toka kwa Profesa Rony Swennen wakati wa uzinduzi wa jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati wa uzinduzi wa jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati wa uzinduzi wa jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo wakiangalia mashine ya kuvunia mihogo
Wadau wakionja vyakula mbalimbali vinavyotengenezwa kwa unga wa muhogo
Wadau wakiwa katika sherehe hizo
Mmoja wa watafiti akielezea kazi yake kituoni hapo
Watafiti wakielezea kazi zao
Wadau wa ITTA ambao ni wapenzi wa Globu ya Jamii
Wadau shereheni
Wageni waalikwa
 
 
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo wakifungua kituo hicho
Rais Dkt. Jakaya Kikwete achunguza kitu kwa kutumia kifaa cha kisayansi katika taasisi hiyo.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mh. Benjamin Mkapa pamona na Balozi wa Marekani nchini Tanzania wakiagalia sehemu ya vifaa vya kisayansi katika taasisi hiyo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo wakifungua kituo hicho
 
Rais Jakaya Mrisho Kikwete,Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo pamoja na Rais Mstaafu,Mh. Benjamin Mkapa wakizindua rasmi jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.
Picha ya pamoja.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisindikizwa na Rais mstaafu wa Nigeria na Balozi wa heshima wa IITA Chief Olesegun Obasanjo baada ya uzinduzi wa jengo la sayansi katika kituo cha Taasisi ya Kimataiafa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Mikocheni jijini Dar es salaam leo Mei 13, 2013.

Rais Kikwete awatkaa wanajeshi wanaokwenda DRC,kuilinda heshima ya Tanzania

 
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi bendera kiongozi wa batalioni ya wanajeshi wa JWTZ wanaokwenda kujiunga na jeshi la Umoja wa Mataifa la kulinda amani Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo,
katika sherehe za kuwaaga zilizofanyika Msangani, Kibaha, Mkoa wa Pwani leo Mei 8, 2013.
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Shamsi Vuai Nahodha na Mkuu wa Majeshi Jenerali Davis Mwamunyange wanashuhudia.
 
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimtakia kila la heri kiongozi wa batalioni ya wanajeshi wa JWTZ wanaokwenda kujiunga na jeshi la Umoja wa Mataifa kulinda amani Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo,katika sherehe za kuwaaga zilizofanyika Msangani, Kibaha, Mkoa wa Pwani leo Mei 8, 2013.Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Shamsi Vuai Nahodha na Mkuu wa Majeshi Jenerali Davis Mwamunyange wanashuhudia.

PICHA NA IKULU.

 
Wanajeshi wa Tanzania wanaokwenda kulinda amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wametakiwa kudumisha utamaduni wa askari wa kulinda amani wa Tanzania katika maeneo mbali mbali duniani kwa kuifanya kazi hiyo kwa heshima, nidhamu na utii ili kulinda heshima yao wenyewe na ile ya Tanzania.
 
Askari hao wamekumbushwa utamaduni huo wa askari wa kulinda amani wa Tanzania katika maeneo mbali mbali duniani na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete.
 
Rais na Amiri Jeshi Mkuu alikuwa akiwaaga wanajeshi wa Tanzania wanaokwenda kulinda amani chini ya Umoja wa Mataifa katika DRC katika hafla iliyofanyika leo, Jumatano, Mei 8, 2012, kwenye Makao Makuu ya Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu la Tanzania yaliyoko Msangani, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani.
 
Akizungumza na askari hao, Rais Kikwete amewaambia kuwa hana wasiwasi kuhusu uwezo wao wa kutelekeza majukumu yao yanayowapeleka DRC isipokuwa tu kwamba waifanye kazi hiyo vizuri na kulingana na utamaduni wa majeshi ya kulinda amani ya Tanzania katika sehemu mbali mbali duniani.
 
“Tunakwenda kutelekeza majukumu ya Umoja wa Mataifa, sina shaka kuwa majukumu yenu mnayaelewa vizuri. Kazi yetu ni kulinda amani na wala hatuendi kupigana na yoyote. Kazi ya kijeshi mnaijua vizuri vile vile na kwa hili pia sina wasiwasi hata kidogo,” amesema Amiri Jeshi Mkuu na kuongeza:
 
“Kubwa ambalo lazima tulikumbuke ni kwamba nchi yetu kila ilikopeleka majeshi ya kulinda amani imejenga utamaduni wa pekee. Imejenga utamaduni wa askari wetu kuifanya kazi ya kulinda amani kwa heshima, kwa nidhamu na kwa utii wa kiwango cha juu. Hii ni heshima kwetu binafsi na heshima kwa taifa letu. Nawashukuruni na nawatakie kila la heri”
 
Kama ishara ya kuagana na askari hao, Rais na Amiri Jeshi Mkuu amemkabidhi Bendera ya Taifa Luteni Kanali Orestess Cassian Komba, Kamanda wa Kikosi cha Tanzania katika DRC ambacho kitajulikana kwa jina la TANZBATT 1-DRC, akimwambia “Bendera na Ikapepee”.
 
Katika jukumu la kulinda amani Mashariki mwa DRC, Kikosi cha Tanzania chenye askari 1281, kitajiunga na vikosi vya Malawi na Afrika Kusini ambavyo vyote vitakuwa chini ya Kamanda wa Brigedi hiyo, Brigedia Jenerali James Mwakibolwa wa Tanzania pia. Kundi la kwanza la askari hao Tanzania linaondoka nchini kesho.
 
Majeshi hayo ya Tanzania yatalinda amani katika DRC chini ya Azimio Nambari 2098 (2013) la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
8 Mei, 2013

RAIS KIKWETE AKIWA ARUSHA KUHANI MISIBA YA WALIOKUFA KATIKA MLIPUKO WA BOMU KANISA LA OLASITI

Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mke wake Mama Salma Kikwete wakihani msiba wa msichana Patricia Joachim Assey (10) nyumbani kwa wazazi wa marehemu katika kitongoji cha Majengo kata ya Elerai aliyefariki kutokana na mlipuko wa bomu jumapili iliyopita Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti. jijini Arusha Mei 7, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mke wake Mama Salma Kikwete wakishiriki dua ya pamoja, wakati walipomtembelea Askofu Mkuu wa Jimbo la Arusha la Kanisa Katoliki jijini Arusha Muadhama Josephat Lebulu katika makazi yake rasmi kutoa pole kwa shambulio la kigaidi katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti ambako alikutana pia na Maaskofu wa Makanisa mbalimbali waliokuwa hapo Mei 7, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mke wake Mama Salma Kikwete wakitoa mkono wa pole kwa watawa wa kanisa hilo wakati walipomtembelea Askofu Mkuu wa Jimbo la Arusha la Kanisa Katoliki jijini Arusha Muadhama Josephat Lebulu katika makazi yake rasmi kutoa pole kwa shambulio la kigaidi katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti ambako alikutana pia na Maaskofu wa Makanisa mbalimbali waliokuwa hapo Mei 7, 2013.
Wananchi wakimuaga Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mke wake Mama Salma Kikwete baada ya kumtembelea Askofu Mkuu wa Jimbo la Arusha la Kanisa Katoliki jijini Arusha Muadhama Josephat Lebulu katika makazi yake rasmi kutoa pole kwa shambulio la kigaidi katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti ambako alikutana pia na Maaskofu wa Makanisa mbalimbali waliokuwa hapo Mei 7,2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mke wake Mama Salma Kikwete wakihani msiba wa kijana James Gabriel (16) aliyefariiki katika shambulio la kigaidi katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti jijini Arusha Jumapili iliyopita.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na Bw. Joachim Assey (aliyekaa kushoto kwake) wakati akihani msiba wa msichana Patricia Joachim Assey (10) aliyefariki kutokana na mlipuko wa bomu jumapili iliyopita katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti jijini Arusha Mei 7, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mke wake Mama Salma Kikwete wakihani msiba wa marehemu Regina Longino Kurusei (45), mkazi wa Olasiti aliyefariiki katika shambulio la kigaidi katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti jijini Arusha Jumapili iliyopita.
Mama Salma Kikwete akipungia wakati msafara wa Rais Kikwete ukiondoka baada ya kuhani msiba wa msichana Patricia Joachim Assey (10) katika kitongoji cha Majengo kata ya Elerai aliyefariki kutokana na mlipuko wa bomu Jumapili iliyopita katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti. katika kitongoji cha Majengo kata ya Elerai jijini Arusha Mei 7, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikaribishwa na Askofu Mkuu wa Jimbo la Arusha la Kanisa Katoliki jijini Arusha Muadhama Josephat Lebulu alipowasili katika makazi yake rasmi kutoa pole kwa shambulio la kigaidi katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti Jumapili iliyopita.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mke wake Mama Salma Kikwete walipomtembelea Askofu Mkuu wa Jimbo la Arusha la Kanisa Katoliki jijini Arusha Muadhama Josephat Lebulu katika makazi yake rasmi kutoa pole kwa shambulio la kigaidi katika Kanisa la Mtakatifu Joseph, Parokia ya Olasiti ambako alikutana pia na Maaskofu wa Makanisa mbalimbali waliokuwa hapo Mei 7, 2013. PICHA NA IKULU.

TAMKO LA RAIS KIKWETE JUU YA TUKIO LA MLIPUKO WA BOMU JIJINI ARUSHA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa ya tukio la leo, Jumapili, Mei 5, 2013 la mlipuko kwenye Kanisa Katoliki la Mt. Joseph Mfanyakazi la Olasiti Jijini Arusha. Tukio hilo la kigaidi limesababisha mtu mmoja kupoteza maisha na wengine 40 kujeruhiwa. Rais Kikwete analaani vikali shambulio hilo lililofanywa na mtu au watu katili, waovu na wenye dhamira mbaya na nia mbaya kwa Tanzania na watu wake.
Rais Kikwete ameagiza vyombo vya usalama nchini kumsaka mtu au watu waliohusika na kitendo hicho kiovu na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria. Vile vile Rais Kikwete amewataka wananchi wote kuwa watulivu wakati Serikali na vyombo vyake inaendelea kufuatilia tukio hili.
Tutawasaka popote walipo na kupambana nao bila huruma. Aidha, tutakabiliana na aina yoyote ya uhalifu nchini iwe ni ugaidi au aina yoyote ya uhalifu wa namna hiyo au wa namna nyingine, uwe na chimbuko lake ndani ya nchi ama nje ya nchi yetu. Kamwe hatutakubali kuwaacha wavuruge amani na usalama wa Tanzania na watu wake. Rais anaamini kuwa Serikali, kwa msaada na ushirikiano wa wananchi, watu hao watapatikana na kuadabishwa ipasavyo.
Aidha, Rais Kikwete anatoa rambirambi za dhati ya moyo wake kwa wafiwa na wale wote ambao wamejeruhiwa katika tukio hilo. Anaungana nao katika machungu na msiba. Rais pia anawaombea wote walioumia katika tukio hili wapate nafuu ya haraka na waendelee na shughuli zao za ujenzi wa taifa.
 
Rais Kikwete vilevile anatoa pole nyingi kwa viongozi na waumini wa Kanisa Katoliki kwa tukio hili la kusikitisha na kuvurugika kwa ibada na shughuli yao muhimu ya uzinduzi wa Kanisa lao.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
IKULU,
DAR ES SALAAM
5 Mei, 2013

RAIS KIKWETE MGENI RASMI MAADHIMISHO YA MIAKA 25 YA HOSPITALI YA KAIRUKI, DAR ES SALAAM, LEO

Rais Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wengine wakikata utepe kuzindua rasmi hosteli ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki wakati wa sherehe za miaka 25 ya hospitali ya Hubert Kairuki Mikocheni, Dar es salaam, leo Machi 16, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati wa sherehe za miaka 25 ya hospitali ya Kumbukumbu ya Hubert Kairuki Mikocheni, Dar es salaam, leo Machi 16, 2013.
Mkurugenzi Mkuu wa hospitali ya Kumbukumbu ya Hubert Kairuki, Mama Koku Kairuki akimkabidhi tuzo Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa kutambua mchango wake mkubwa katika kuendeleza sekta ya afya nchini wakati wa sherehe za miaka 25 ya hospitali hiyo leo Machi 16, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Rais Mstaafu Alhaj Ali Hassan Mwinyi tuzo kwa kutambua mchango wake mkubwa katika sekta ya afya nchini wakati wa sherehe za miaka 25 ya hospitali hiyo leo Machi 16, 2013.
Baadhi ya viongozi wa dini waliohudhuria sherehe za miaka 25 ya hospitali ya Hubert Kairuki Mikocheni, Dar es salaam, leo Machi 16, 2013.
Msanii Mrisho Mpoto akiburudisha wakati wa sherehe za miaka 25 ya hospitali ya Hubert Kairuki Mikocheni, Dar es salaam, leo Machi 16, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu Alhaj Ali Hassan Mwinyi, Waziri Mkuu Mstaafu, Dkt Salim Ahmed Salim
wakiangalia watoto wachanga waliotunzwa katika chumba maalum muda mfupi baada ya kuzaliwa wakati Rais Kikwete alipotembelea sehemu mbalimbali
za hospitali ya Kumbukumbu ya Hubert Kairuki akiwa mgeni rasmi katika sherehe za miaka 25 ya kuanzishwa kwake leo Machi 16, 2013.
Seehemu ya wageni waalikwa na wanafunzi na wafanyakazi wa hospitali ya Kumbukumbu ya Hubert Kairuki wakati wa sherehe za miaka 25 ya hospitali ya Hubert Kairuki Mikocheni, Dar es salaam, leo Machi 16, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi, Waziri Mkuu Mstaafu Dkt Salim Ahmed Salim, na viongozi wa hospitali ya Hubert Kairuki wakiwa katika picha ya pamoja na vijana waliozaliwa
katika hospitali hiyo miaka 25 iliyopita leo Machi 16, 2013.PICHA NA IKULU.

Rais Kikwete azindua jengo la kitivo cha sayansi chuo kikuu cha kiislamu cha morogoro

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia katika sherehe za uzinduzi wa jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Kiislamu mjini Morogoro leo
 Rais Kikwete akiendelea na hotuba huku akishangiliwa
 Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kiislamu Morogoro Mama Mwantumu Malale akiongea machache na kumkaribisha Rais Kikwete
Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika picha ya pamoja na uongozi wa chuo katika sherehe za uzinduzi wa jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Kiislamu mjini Morogoro leo
 Sehemu ya wanafunzi
 Profesa Juma Mikidadi Mtupa akikaribishwa kupata picha na mheshimiwa
 Picha na wahadhiri
 Picha na viongozi wa wanafunzi 
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizindua jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Kiislamu mjini Morogoro leo
 Rais Kikwete akipeana mikono na Bw Ahmed Saggaf
 Rais Kikwete akitembelea moja ya vyumba vya maabara
 Rais Jakaya Kikwete akipata maelezo ya ujenzi wa jengo la kitivo cha TEKNOHAMA katika Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizindua jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Kiislamu mjini Morogoro leo
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikata utepe kuzindua jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Kiislamu mjini Morogoro leo
 Makamu Mkuu wa Chuo Profesa Hamza Mustafa Njozi akisoma ripoti  ya chuo kwa Rais Kikwete
Sehemu ya wanafunzi na wageni waalikwa.

 

HOTUBA YA MHESHIMIWA RAIS JAKAYA MRISHO KIKWETE KATIKA UFUNGUZI RASMI WA JENGO LA KITIVO CHA  SAYANSI KATIKA CHUO KIKUU CHA WAISLAMU CHA  MOROGORO (MUM),

TAREHE 14 MACHI, 2013, MOROGORO

 

Mzee Kitwana Suleiman Kondo, Mwenyekiti wa Taasisi ya Maendeleo ya Waislamu (MDF);

Mheshimiwa Joel Bendera, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro;

Mama Mwantumu Malale, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro;

Profesa Hamza Mustafa Njozi, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro;

Viongozi mbalimbali wa Serikali, vyama vya siasa na Jumuiya mliohudhuria;

Wageni waalikwa;

Mabibi na Mabwana;

Niruhusuni niungane na wenzangu walionitangulia kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kukutana hapa.  Nakushukuru sana Mama Mwantumu Malale, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro na viongozi wenzako kwa kunialika kuja kujumuika nanyi katika siku hii adhimu ya ufunguzi wa jengo la Kitivo cha Sayansi katika Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro. Mmenipa heshima kubwa ya kuwa sehemu ya historia ya Chuo hiki.  Kwa kweli, nimefarijika sana kuona Chuo chetu kinazidi kupata mafanikio ya kutia moyo hasa ukizingatia ukweli kwamba kina muda mfupi tu tangu kuanzishwa kwake.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Natoa pongezi nyingi kwako, Makamu Mkuu wa Chuo na wale wote walioshiriki kubuni wazo la kuwa na jengo la Kitivo cha Sayansi na kufanikisha ujenzi wake.  Juhudi zao na moyo wao wa kupenda maendeleo ndio umetufanya sisi kujumuika hapa leo kushuhudia mafanikio haya. Hakika ni jambo la kujivunia. Pia, nawapongeza sana Wajenzi na Mhandisi Mshauri kwa kazi nzuri waliyofanya ya ujenzi wa jengo hili.  Sote tunaliona jengo lilivyojengwa vizuri na kwa namna yake linapendezesha mandhari ya Chuo.

Kwa namna ya pekee napenda kwa niaba yenu nitoe shukrani zangu za moyoni kwa taasisi ya Al-Barakah kwa kufadhili ujenzi wa jengo hili.  Asanteni sana kwa ukarimu wenu na upendo mkubwa mliouonesha kwa nchi yetu na watu wake. Naomba taasisi nyingine na watu binafsi waige mfano huu mzuri wa kusaidia miradi mbalimbali inayonufaisha jamii.  Tukumbuke ule msemo wa wahenga kuwa “kutoa ni moyo, usambe si utajiri”.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Mabibi na Mabwana;

Kwa miaka mingi madhehebu ya dini  na mashirika ya dini yamekuwa washirika muhimu sana wa Serikali katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu.  Yamekuwa yanajihusisha na kutoa huduma kwa jamii kama vile afya, elimu na nyinginezo. Kwa ajili hiyo watu wengi sana nchini wamenufaika na wanaendelea kunufaika na huduma zinazotolewa na mashirika ya dini.

Kwa miaka mingi  mashirika na  taasisi za madhehebu ya dini ya Kikristo ndiyo yaliyokuwa yakionekana kutoa huduma hizo. Kwa upande wa Waislamu, ukiacha Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan, mchango umekuwa mdogo sana. Ni jambo la faraja kubwa kuona Taasisi ya Maendeleo ya Waislamu (MDF) ikionyesha njia.  Kwa kumiliki na kuendesha Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro kwa ufanisi, MDF inatoa mchango muhimu katika kuendeleza elimu ya juu na maendeleo nchini.  Idadi kubwa ya wanafunzi waliofuzu masomo yao na waliopo katika Chuo hiki tangu kilipoanzishwa mwaka 2005 ni ushahidi tosha wa kazi nzuri inayofanywa na MDF.  Hongereni sana.  Tunawaombea kwa Mola mpate mafanikio makubwa zaidi miaka ya usoni kwa upande wa elimu na huduma nyingine muhimu.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Katika kipindi cha miaka saba sasa, Serikali yetu imeongeza sana uwekezaji katika upanuzi wa elimu  tangu ya awali hadi elimu ya juu.  Tumeamua kufanya hivyo kwa sababu vijana wengi waliokuwa wanastahili kupata elimu ya awali, msingi, sekondari, ufundi na elimu ya juu walikuwa hawapati. Tanzania ni kubwa kuliko Kenya na Uganda kwa eneo na idadi ya watu lakini ndiyo tuliokuwa na idadi ndogo ya wanafunzi kwa ngazi zote hizo.  Kwa mfano, mwaka 2005 idadi ya wanafunzi waliokuwa Chuo Kikuu nchini Kenya ilikuwa108,407, Uganda 88,360 na kwa baadhi ya nchi za SADC kama vile Afrika Kusini idadi hiyo ilikuwa 717,973. Wakati wenzetu wakiwa na idadi hiyo, sisi tulikuwa na wanafunzi 40,719 tu katika vyuo vikuu nchini.  Hali ilikuwa hivyo pia kwa elimu ya sekondari.  Kenya ilikuwa na wanafunzi 925,341, Uganda 619,519 na Afrika Kusini 4,186,882 wakati Tanzania ilikuwa na wanafunzi 524,325 tu waliokuwa katika shule za sekondari.

Tuliona hali hii haikubaliki hivyo tukaamua hatuwezi kuiacha iendelee.  Tukaamua kudhibiti. Tukachukua hatua tulizochukua za kupanua elimu katika ngazi zote.  Matokeo ya uamuzi huo ni kwamba vijana wanaopata fursa ya kupata elimu katika ngazi zote wamekuwa wengi kuliko wakati mwingine wo wote katika historia ya nchi yetu, tumewafikia na kuwapita majirani zetu. Kazi kubwa tunayoendelea nayo sasa ni kuwekeza katika kuimarisha ubora wa elimu waipatayo vijana wetu kwa kuongeza walimu, vifaa vya kufundishia, vitabu na huduma nyinginezo. Inshallah hata kwa dhamira yetu, hii njema Mola atatuwezesha. Mwanzo mgumu lakini hatma itakuwa nzuri.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Kufuatia juhudi hizo, idadi ya wanafunzi waliopo kwenye vyuo vikuu nchini imeongezeka sana, kutoka wanafunzi 40,719 mwaka 2005 hadi wanafunzi 166,484 mwaka 2012. Kwa upande wa sekondari mwaka 2011 tulikuwa na wanafunzi milioni 1.79 na wenzetu wa Kenya walikuwa na wanafunzi milioni 1.77. Haya ni mafanikio makubwa.

Serikali itaendelea kuwekeza  kwenye upanuzi wa fursa za elimu na ubora wake. Hata hivyo ushiriki wa wadau wengine kuunga mkono juhudi za serikali ni jambo muhimu sana.  Tumeweka  mazingira mazuri kwa wadau hao kufanya hivyo na mafanikio yanaonekana wazi. Kama nilivyokwishasema awali, mashirika ya dini yamekuwa wadau wa kutumainiwa na mchango wao uko wazi. Unajieleza wenyewe. Kwa mfano, katika vyuo vikuu 49 vilivyopo nchini, vinavyomilikiwa na umma ni 14 tu. Vyuo vikuu 24 vinamilikiwa na mashirika ya dini na 11 na sekta binafsi.

 

 

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa na muhimu unaotolewa na vyuo vikuu vinavyomilikiwa na mashirika ya dini na sekta binafsi.  Ninyi mmekuwa washirika wazuri na wa uhakika katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya elimu katika nchi yetu.  Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuwaunga mkono na kushirikiana nanyi ili kuwawezesha vijana na Watanzania wengi zaidi waweze kupata elimu. Uamuzi wa kufanya utaratibu wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu uhusishe wanafunzi wa vyuo visivyokuwa vya umma ni moja ya mambo mengi muhimu yanayofanywa na Serikali kuthibitisha usemi wangu huo.

Tulipoingia madarakani mwaka 2005 tulifanya mambo mawili muhimu kuhusu mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu.  Kwanza uamuzi kwamba, mikopo itolewe kwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya umma na vile visivyokuwa vya serikali. Kabla ya hapo ilihusu vyuo vya umma pekee. Pili kwamba, kila mwaka tuongeze fedha zinazotengwa  kwa ajili ya Mfuko huo ili idadi ya wanafunzi wanaonufaika iongezeke. Tulikuta Mfuko ukiwa na  shillingi billioni 56.1 unanufaisha wanafunzi 16,345 mwaka 2005. Tukaongeza kila mwaka na katika mwaka huu wa fedha (2012/13) tumetenga shillingi bilioni 345 zinazowanufaisha wanafunzi 98,772.

Tutaendelea kuongeza fedha katika Mfuko huo ili wanafunzi wengi zaidi wanufaike na hata ifikie siku moja tuweze kuwakopesha wote bila ya kujali sifa ya uwezo wa wazazi au walezi kulipa ada.  Kwa kasi tuliyonayo na kwa jinsi tunavyozidi kufanikiwa katika kukusanya mapato ya serikali, naamini miaka michache ijayo tunaweza kufikia lengo hilo. Nawasihi Bodi ya Mikopo iwekeze katika  kuimarisha uwezo wa kuwafuatilia waliokopeshwa kulipa mikopo waliyopewa. Matamanio yangu ni kuwa fedha zilizotolewa zizunguke ili tupunguze kiasi kinachotolewa na bajeti ya serikali kila mwaka.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Mabibi na Mabwana;

Niruhusuni nitumie nafasi hii kukupongeza wewe Mkuu wa Chuo, Makamu Mkuu wa Chuo, Wahadhiri  na Jumuiya nzima ya Chuo Kikuu hiki  kwa kazi kubwa na nzuri muifanyayo ya kuendeleza na kuboresha Chuo. Tumeshuhudia ujenzi wa jengo nililolifungua leo. Tumeona mafanikio kwa upande wa ongezeko la idadi ya wanafunzi, walimu, wafanyakazi na fani zinazofundishwa katika kipindi hiki kifupi cha uhai wa Chuo hiki.

Nimefurahishwa na kufarijika sana  kusikia kuwa ubora wa elimu inayotolewa hapa chuoni ni jambo linalopewa kipaumbele cha kwanza.  Jambo hili ni muhimu sana kulisisitiza kwani tunataka wahitimu wa Chuo hiki wafanane na wahitimu wa Chuo chochote kizuri nchini na hata duniani.  Ningependa kuona wahitimu wa Chuo hiki wanagombewa katika soko la ajira.  Hili ni jambo linalowezekana.  Kinachotakiwa  ni uamuzi wa Baraza na Seneti kuwa iwe hivyo na kuchukua hatua zipasazo.  Sina shaka kuwa mnaweza kufanya hivyo.  Hakika mnaweza, na sote kwa umoja wetu tunaweza.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Nimefurahi sana, pia, kusikia kuwa Chuo kinatoa mafunzo ya ualimu. Bila ya shaka mnaelewa kwa nini nafurahi. Tuna uhaba mkubwa wa walimu nchini hivyo Chuo cho chote kinachotoa mafunzo ya ualimu hunifurahisha.  Endeleeni kuimarisha mafunzo hayo ili Chuo chenu kitambulike na kukubalika nchini kwa sifa ya kutoa walimu wazuri.  Walimu wa kutoka Chuo hiki wawe wale wanaojua vyema masomo wanayofundisha, mahiri kufundisha na waadilifu.  Naomba pia mtoe kipaumbele cha juu kwa mafunzo ya ualimu wa masomo ya sayansi na hisabati.  Mkifanya hivyo, mtakuwa mnatoa mchango mkubwa katika jitihada za kupunguza uhaba wa walimu wa masomo hayo nchini.  Naamini kitendo cha kuzindua Jengo la Kitivo cha Sayansi, kilichofanyika muda mfupi uliopita kinatoa matumaini ya Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro kuchangia katika jitihada za kupunguza pengo la walimu wa sayansi nchini.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Nimewasikia mkieleza kwa ufasaha changamoto kubwa na ndogo ambazo Chuo inakabiliana nazo.  Nawapongeza kwa dhati, wewe na viongozi wenzako kwa ubunifu wenu na hatua mnazochukua kuzikabili changamoto hizo.  Nawaahidi msaada na ushirikiano wangu na wa serikali kwa yale yaliyoko kwenye uwezo wangu na wa serikali katika kutafuta ufumbuzi kwa changamoto zinazowakabili.

Nawapongeza kwa uamuzi wenu wa kutafuta vyuo vikuu rafiki vilivyoko katika nchi mbalimbali duniani mnavyoweza kushirikiana navyo.  Endeleeni kufanya hivyo kwani vyuo vikuu vingi duniani hufanya hivyo.  Hamtakuwa wa kwanza na wala hamtakuwa mnafanya jambo la kustaajabisha. Mnaweza,        mkipenda, kuwaomba Mabalozi wetu waliopo katika nchi mbalimbali duniani wawasaidie. Ni wajibu wao kufanya hivyo kwani kusaidia kusukuma maendeleo ya hapa nchini kutoka huko waliko ndilo jukumu lao la msingi. Vile vile, nimefurahishwa na mipango yenu ya baadaye ya kuwa na matawi katika mikoa mbalimbali nchini.  Hongereni kwa uamuzi wenu wa busara. Lazima Chuo kitanuke kwa maana ya kuwa kikubwa zaidi, makao makuu na kwa kuwa na vyuo vishiriki na shule au  vitivo sehemu mbalimbali nchini.

Ndugu Mkuu wa Chuo;

Kazi iliyo mbele yenu ni kubwa, hivyo ni vyema kuweka mikakati mizuri na mipango thabiti ya utekelezaji na ufuatiliaji wa dhamira yenu hiyo njema.  Rai yangu kwenu ni kuwaomba muwe wabunifu zaidi hasa katika kutafuta vyanzo vingine vya mapato vitakavyosaidia Chuo kujiendesha bila kutegemea ada peke yake.  Chuo kiangalie uwezekano wa kufanya shughuli zitakazowaingizia mapato kama vile kufanya shughuli za kutoa ushauri. Pia muangalie uwezekano wa kuwekeza wenyewe kwenye miradi ya kiuchumi au kwa kushirikiana na wawekezaji katika baadhi ya maeneo.

Kuhusu nafasi mbili za ufadhili nilizopewa na Chuo kikuu cha Tun Abdul Razak cha Malaysia, nitafuatilia kujua  kilichoendelea na kinachoendelea. Je, nafasi hizo bado zipo?  Zikiwepo, nitawasiliana na wahusika waangalie uwezekano wa kuwapeni. Kama zimeshagawiwa basi tusubiri safari ijayo. Kwa  masuala ya ardhi na maombi mengine nimeyasikia, yaleteni tuangalie namna ya kusaidiana.

Ndugu Makamu Mkuu wa Chuo, na

Wafanyakazi wote wa Chuo cha Waislamu cha Morogoro;

Napenda kuwakumbusha kuwa mnayo dhamana kubwa na wajibu mkubwa na wa kihistoria. Ule ukweli kwamba ni mara ya kwanza kwa Taasisi ya Waislamu wazawa kuwa na Chuo Kikuu inawapeni wajibu maalum wa kuhakikisha Chuo kinafanikiwa. Ni mtihani na changamoto ya aina yake kuthibitisha kuwa Waislamu nao wanaweza kuwa na Chuo kizuri na chenye kutoa elimu ya ubora wa hali ya juu.  Kwa sababu hiyo hamna budi kuhakikisha kuwa mna mipango mizuri ya kujenga Chuo cha hadhi na ubora wa hali ya juu.  Ihakikishwe kuwa mipango hiyo inatekelezwa kwa ukamilifu.

Aidha jumuiya yote inao wajibu wa kufanya kazi kwa bidii, ubunifu, maarifa na weledi ili dhima hiyo ya Chuo iweze kutimizwa kwa ukamilifu. Timizeni wajibu wenu ipasavyo ili jina la Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro likue haraka. Sifa yake isambae na kuvuma kote nchini. Chuo kifanye vizuri ili wanafunzi waone fahari kuwa wahitimu wa Chuo hiki. Chuo ambacho, wazazi wapende kuleta vijana wao kuja kusoma hapa. Kwa jinsi Mkuu wa Chuo alivyoeleza, mimi nina imani mnaweza, fanyeni kweli.

 

 

Ndugu Wanafunzi wa Chuo cha Waislamu cha Morogoro;

Naomba wote muone fahari ya kuwa wanafunzi katika Chuo cha kihistoria hapa nchini.  Nawasihi mjitume kwa kadri ya uwezo na vipaji mlivyopewa na Mwenyezi Mungu mfanikishe kile kilichowaleta.  Jifunzeni kwa bidii mfaulu vizuri ili mkihitimu muwe kielelezo kizuri cha mafanikio na ubora wa  Chuo  Kikuu Cha Waislamu cha Morogoro.  Muwe Mabalozi na kioo cha ufanisi wa Chuo hiki. Nawasihi mjiepushe na mambo yatakayowapunguzia muda au kuwaondoa katika shughuli ya msingi iliyowaleta hapa ya kujifunza mpate digrii katika fani mliyochagua mwenyewe kuisomea.  Vishawishi ni vingi na wapo watu wengi wanaopanga kuwashawishi mtumie muda wenu adhimu kufanya wanayoyataka wao ambayo mkishiriki huwatoa kwenye malengo na kutekeleza yao. Mambo ya dunia ya nje ya Chuo ni mengi huna budi kutambua lipi ufanye na lipi usifanye na kwa wakati gani!

Mwanafunzi wa Chuo Kikuu ni mtu mzima, si mtoto. Lazima ujue kuwa unawajibika kwa kila unaloamua na kutenda.  Amua kuwajibika vizuri. Fikiri kabla ya kutenda, changanua lipi ni lipi kabla ya kufanya uamuzi wa kile unachotaka kufanya.  Wakati wote uongozwe na busara na hekima na siyo jazba na ushabiki wa matakwa ya kundi.  Kama ni jema fanya na kama si jema usifanye.  Kwanza tambua wewe ni nani na uko hapa kwa ajili gani. Lazima ujue kuwa hatma ya yote uko peke yako.  Utafaulu au kufeli wewe.  Utapata shahada wewe na si mtu mwingine.  Hakuna ubia wa kufaulu au kufeli au kiwango cha kufaulu. It will always remain personal. Katika masomo unanufaika wewe.  Shirikiana na wengi lakini usisahau kujali maslahi yako.  Maslahi ya wengi yasiyojumuisha yako, yahoji vizuri kabla ya kuamua kushiriki au kufanya. Vinginevyo labda kama umeamua kujitoa muhanga, uwe shujaa. Hata kwa hilo, sijui utakuwa shujaa wa nani.

Mabibi na Mabwana;

Kabla ya kumaliza napenda kutambua na kumshukuru Rais wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamin Mkapa na viongozi wa MDF kwa juhudi zao za pamoja zilizowezesha Chuo hiki kuwepo.  Nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowashukuru wananchi wanaokizunguka Chuo kwa ujirani mwema na wakazi wa Morogoro kwa ujumla kwa kukipokea vizuri na kuishi na wanajumuiya wa Chuo hiki kwa upendo mkubwa. Naomba muendelee na moyo na ushirikiano huo.

Baada ya kusema hayo, nawashukuru sana kwa kunialika. Nawatakia kila la heri na mafanikio tele.

Asanteni sana kwa kunisikiliza.

HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWA WANANCHI, 28 FEBRUARI, 2013


Utangulizi
Ndugu wananchi;
Namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujalia uzima na kutuwezesha kuwasiliana kupitia utaratibu wetu mzuri tuliojiwekea wa kufanya hivyo kila mwisho wa mwezi. Leo nimepanga kuzungumza nanyi mambo matatu; yaani Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Uhusiano wa Waislamu na Wakristo na Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Nne.
Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa
Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo

Ndugu Wananchi;
Tarehe 8 Februari, 2013 kule Addis Ababa, Ethiopia niliungana na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe. Ban Ki-Moon, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Mhe. Nkosozana Dlamini Zuma na viongozi wa nchi 12 za Afrika Mashariki, Kati na Kusini kutia saini Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na jirani zake. Pamoja na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo zilikuwepo nchi za Burundi, Rwanda, Uganda, Sudani Kusini, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Kongo, Angola, Zambia na Tanzania ambazo ni jirani ya Kongo. Nchi za Ethiopia, Msumbiji na Afrika ya Kusini pamoja na Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika zilitia saini kama wadhamini. Ethiopia kwa nafasi yake ya kuwa Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika na Msumbiji kwa kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC). Nchi wanachama wa Mkutano wa Ukanda wa Maziwa Makuu ziliwakilishwa na Uganda ambayo ni Mwenyekiti wake wa sasa. Afrika ya Kusini ilishirikishwa kwa kuwa taifa kubwa na linalotegemewa katika ukanda wetu.
Mpango huu ni jitihada nyingine ya kusaidia Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo ipate amani ya kudumu. Kama tujuavyo, tangu mwaka 1997 wakati wa vita vilivyosababisha kuondolewa kwa Rais Mobutu Seseseko mpaka sasa nchi hiyo rafiki na jirani haijapata amani na utulivu wa kudumu. Kumekuwepo jitihada na mipango kadhaa ya kuleta amani ambayo hata hivyo baada ya muda fulani machafuko hutokea tena na mipango hiyo kuvurugika. Inakadiriwa kuwa takriban watu milioni 5.4 wamepoteza maisha na watu wengi kuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi yao. Pia kumekuwepo na vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto pamoja na mali nyingi kuharibiwa au kuporwa.
Ndugu Wananchi;
Machafuko yaliyoanzishwa na waasi wa Kundi la M23 mapema mwaka wa jana ndiyo sababu ya kuwepo kwa Mpango huu wa sasa tuliotia saini kule Addis Ababa, Ethiopia tarehe 8 Februari, 2013. Katika Mpango huo Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na jirani zake, Tanzania ikiwemo, tumekubaliana kutokufanyiana vitendo vinavyohatarisha amani na usalama wa nchi zetu. Tumeazimia tusifanye hivyo ama moja kwa moja kama nchi au kwa kutumia watu wengine. Aidha, tumekubaliana tusiruhusu watu au vikundi vya watu kutumia nchi zetu kuhatarisha usalama wa nchi nyingine. Kimsingi tumekubaliana kuwa majirani wema. Katika Mkataba huo, majukumu ya kila nchi yameainishwa vizuri pamoja na yale ya Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika na Mashirika ya Kikanda hususan SADC na ICGLR.
Ndugu Wananchi;
Niliamua kukubali kushiriki na kutia saini Mpango ule kwa kutambua ukweli kwamba sisi majirani wa nchi ya Kongo tunao wajibu wa kusaidia kwa kile tunachoweza. Wananchi wa Kongo wameteseka kwa muda mrefu mno hivyo kama Mpango huu utawasaidia kupata amani na usalama hatuna budi kuunga mkono. Ni kwa misingi hiyo hiyo, tulikubali kuchangia kikosi kimoja katika Jeshi la Kimataifa la kulinda amani huko Mashariki ya Kongo kama ilivyoamuliwa na Mkutano wa Nchi za Maziwa Makuu mwezi Julai, 2012. Uamuzi huo umeungwa mkono na Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika na Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika. Umoja wa Mataifa umeamua Jeshi hilo liwe sehemu ya Jeshi la Umoja wa Mataifa la Kulinda Amani nchini Kongo (MONUSCO) jambo ambalo sote tumeliafiki. Tumepeleka walinzi wa amani Darfur, Sudan na Lebanon, kwa nini tusipeleke Kingo. Miaka ya nyuma tulishapeleka walinzi wa amani Liberia, Siera Leon na Eritrea.
Ni matumaini yetu kuwa Mpango huu mpya utatekelezwa kwa ukamilifu na kuzaa matunda yaliyokusudiwa. Kama nchi jirani, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo yenye amani, usalama na utulivu ni jambo lenye maslahi makubwa kwetu. Ina maana ya kutokuwa na wakimbizi kutoka nchi hiyo, uharamia katika Ziwa Tanganyika kutokuwepo na ustawi wa shughuli za kiuchumi na kibiashara kwa upande wetu na wao. Ni chachu muhimu ya maendeleo ya Mikoa ya pembeni mwa Ziwa Tanganyika na Tanzania kwa jumla.

Uhusiano wa Waislamu na Wakristo
Ndugu wananchi;
Jambo la pili ninalopanga kulizungumzia siku ya leo ni uhusiano wa Wakristo na Waislamu hapa nchini. Kwa miezi kadhaa sasa tangu mwaka wa jana kumekuwepo na matukio kadhaa yanayosababisha mifarakano na kupandikiza chuki baina ya waumini wa dini ya Kikristo na Kiislamu. Matukio ya kauli na vitendo vya kudharau dini za wengine, kunajisi vitabu vitakatifu vya dini hizo, kuchoma moto nyumba za ibada na mzozo kuhusu nani achinje. Kumekuwepo na matumizi mabaya ya radio na simu za mkononi na mifumo mingine ya mawasiliano iliyoeneza maneno na ujumbe wa chuki na vitisho kwa waumini na viongozi wa dini zetu hizi kubwa hapa nchini. Kauli na matendo hayo, katika baadhi ya maeneo yamekuwa chanzo cha uhasama na magomvi baina ya waumini na hatimaye kusababisha vifo kama ilivyotokea Buseresere Mkoani Geita na Beit-el-Ras, Zanzibar.

Ndugu zangu;
Watanzania hatujawahi kuwa hivi, kumetokea nini? Miaka yote Watanzania ni watu tunaotambua na kuheshimu tofauti za dini zetu mbalimbali tunazoabudu. Watanzania ni waelewa na kwa ajili hiyo tumekuwa tunavumiliana kwa tofauti zetu na ndiyo maana tumekuwa tunaishi pamoja kidugu, kwa umoja na kushirikiana kwa mambo yote yanayotuhusu maishani isipokuwa wakati kila mmoja anapoingia kwenye nyumba ya ibada kumuomba Mola kwa misingi na taratibu ya dini yake.
Watanzania wa dini zote na makabila tofauti wanaishi nyumba moja, wanasoma pamoja, wanafanya kazi pamoja kwa udugu, upendo, umoja na ushirikiano. Kuna koo na familia zenye watu wa dini tofauti, wengine Waislamu na wengine Wakristo. Wapo Waislamu na Wakristo wameoana, wamezaa na wamejukuu na kila mmoja amebakia kuwa mfuasi wa dini yake. Wapo pia ambao hawakuoa lakini wamezaa watoto na wanashirikiana kulea watoto wao. Hayo ndiyo maisha ya Watanzania na hiyo ndiyo Tanzania yenye amani na utulivu tuliyozaliwa, kukua na kuishi. Nawasihi sana Watanzania wenzangu, tuienzi na kuidumisha tunu hii waliyotujengea mababu zetu.
Ndugu Wananchi;
Kuna wenzetu kwa sababu wanazozijua wao na kwa manufaa wanayoyajua wao wanataka kutuvurugia nchi yetu hii nzuri. Tusiwape nafasi wachochezi hawa kwani hawatutakii mema na wala hawazitakii mema dini zetu na nchi yetu. Sisi katika Serikali hatutasita kuwachukulia hatua wale wote wanaochochea chuki za kidini, wanaodharau vitabu vitakatifu vya dini nyingine na wanaokejeli dini nyingine.
Nimewakumbusha Polisi na mamlaka husika kote nchini wasifanye ajizi kwenye matukio ya namna hiyo. Wawachukulie hatua stahiki wale wote wanaohusika. Nimewataka wazingatie msemo wa Kiswahili usemao “ajizi nyumba ya njaa”. Wachochezi wa mifarakano na chuki za kidini wasipodhibitiwa ipasavyo wataleta maafa kwa Watanzania wasiokuwa na hatia. Nimewakumbusha Wakuu wa Wilaya na Mikoa kama walinzi wa amani wa maeneo yao ya uongozi, watimize ipasavyo wajibu wao. Pia nimewataka Polisi wakamilishe mapema upelelezi wa makosa ya vurugu za kidini na wahusika wafikishwe haraka kwenye vyombo vya sheria ili iwe fundisho kwa wengine.
Ndugu Wananchi;
Naendelea kuwasiliana na viongozi wa dini kuzungumza nao juu ya wajibu wao maalum wa kuhakikisha kuwa wafuasi wao hawawi chanzo au sehemu ya tatizo na mifarakano miongoni mwa waumini wa dini mbalimbali nchini. Hali kadhalika naitumia nafasi hiyo kuwakumbusha umuhimu wa kuzungumza na wenzao wa upande mwingine kutatua tofauti au matatizo yanayoathiri uhusiano mwema baina yao.
Ndugu Wananchi;
Kuna msemo maarufu usemao “mjenga nchi ni mwananchi na mbomoa nchi ni mwananchi”. Naomba tuwe wajenga nchi na kamwe tusikubali kuwa wabomoa nchi. Hivi tukiibomoa nchi yetu tutakwenda wapi? Tutaishi wapi? Tusikubali kugeuka wakimbizi ndani ya nchi au nje ya nchi yetu.
Kwa mara nyingine tena, napenda kutumia nafasi hii kuwapa mkono wa pole makanisa, familia, ndugu na jamaa wote wa Mchungaji Kachila na Padri Mushi. Sote tunafahamu machungu waliyonayo kwa kuondokewa na wapendwa wao. Serikali na wapenda amani wote nchini wapo pamoja nanyi katika kipindi hiki kugumu. Vile vile natoa rambirambi zangu nyingi kwa waumini wote wa Kanisa la Pentekoste Assemblies of God na Kanisa Katoliki Tanzania kwa kuondolewa ghafla na viongozi wao. Tuzidi kumwomba Mwenyezi Mungu azipumzishe kwa amani roho za viongozi wetu. Amin.
Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Nne Mwaka 2012
Ndugu wananchi;
Tarehe 18 Februari, 2013 Baraza la Mitihani la Taifa lilitangaza matokeo ya Mtihani wa Taifa wa Kidato cha Nne ya mwaka 2012. Wanafunzi 397,132 walifanya mtihani huo na kati ya hao, waliofaulu ni 126,851 yaani sawa na asilimia 34.5. Wanafunzi 240,903 ambao ni sawa na asilimia 65.5 hawakufaulu mtihani huo. Kwa ulinganifu, matokeo hayo ni mabaya kuliko matokeo mengine ya mtihani huo ya miaka ya hivi karibuni.
Mwaka 2011, jumla ya wanafunzi 336,782 walifanya mtihani huo na waliofaulu walikuwa asilimia 53.6 na ambao hawakufaulu kabisa walikuwa asilimia 46.4. Mwaka 2010 jumla ya wanafunzi 352,045 walifanya Mtihani wa Taifa wa Kidato cha Nne, asilimia 50.4 ya wanafunzi hao walifaulu na asilimia 49.6 ya wanafunzi hawakufaulu.
Ndugu Wananchi;
Matokeo ya mitihani ya kidato cha nne mwaka 2012, yameshtua na kufadhaisha watu wengi nchini na kwa sababu stahiki kabisa. Kwanza, kwamba kiwango cha kufaulu kimeporomoka sana, tena ghafla, kutoka asilimia 53.6 mwaka 2011 hadi asilimia 34.5 mwaka 2012. Hili ni anguko la asilimia 19.1 ambalo, kwa kila hali, ni kubwa sana. Pili, kwamba hata shule zinazofahamika kuwa na historia ya kufaulisha vizuri kama vile seminari, shule za watu binafsi, za mashirika ya dini na sekondari kongwe za Serikali ambazo hazina matatizo kama ilivyo kwa zile sekondari za Kata, nazo safari hii hazikupata mafanikio kama ilivyo kawaida yao. Nazo zimejikuta zikiwa na idadi ya vijana waliopata daraja la kwanza, la pili na la tatu ikipungua wakati waliopata daraja la nne na waliofeli wakiongezeka.
Isitoshe na kiwango cha ufaulu wa vijana umepungua pia. Mwaka 2010 wanafunzi 10 bora wote walikuwa wamefaulu daraja la kwanza la alama au pointi 7. Mwaka 2011 katika wanafunzi 10 bora wanane walipata daraja la kwanza kwa alama 7 na wawili alama 8. Mwaka 2012 katika wanafunzi 10 bora, watatu walipata daraja la kwanza kwa alama 9, watatu alama 10 na wawili alama 11.
Ndugu Wananchi;
Haya ndiyo mambo yanayozua maswali kwa watu wengi yanayohitaji kupatiwa majawabu ya uhakika. Kulikoni mwaka 2012? Ndiyo msingi wa uamuzi wa Waziri Mkuu, Mhe. Mizengo Pinda, kuamua kuunda Tume ya kuliangalia suala zima la mitihani ya mwaka 2012 na matokeo yake. Hali hii haijawahi kutokea katika miaka ya hivi karibuni. Ni suala muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu, hivyo lazima ukweli wake ujulikane kwa uhakika. Hii itawezesha Serikali na wadau wengine kuchukua hatua stahiki kurekebisha mambo mapema iwezekanavyo ili hatimaye mambo yawe mazuri siku za usoni. Tusipofanya hivyo mambo yanaweza kuwa mabaya zaidi na lawama zinaweza kuwa kubwa zaidi kwa Serikali.
Ndugu Wananchi;
Hivi sasa kunatolewa mawazo lukuki kuhusu sababu za kwa nini matokeo yamekuwa mabaya. Wapo wanaodhani kuwa lipo tatizo katika utungaji wa mitihani, usahihishaji wake au kutoa maksi kwa watahiniwa. Wapo wanaodhani walimu hawawajibiki ipasavyo au baadhi yao kutokumudu masomo wanayofundisha. Wapo wanaofikiria kuwa wanafunzi hawako makini katika kufuatilia masomo na wazazi hawajali kufuatilia maendeleo ya watoto wao shuleni. Wapo wanaoinyooshea kidole Serikali kwa sera, mitaala na uwekezaji usiokidhi mahitaji ya maendeleo ya elimu. Wapo wanaofikiria kuwa Serikali kushindwa kuongeza mishahara ya walimu kwa asilimia 100 kama walivyotaka imechangia. Orodha ni ndefu, ali mradi kila mtu ana mawazo yake. Na sisi katika Serikali hatuwezi kuwa tunadhani kwa sababu tunayo dhamana maalum. Lazima tujue ukweli kwa uhakika na ndiyo maana kuna umuhimu wa Tume. Naomba kila mtu mwenye mawazo yake ayafikishe kwenye Tume hiyo hapo itakapoundwa ili tupate jawabu muafaka la tatizo hili.
Ndugu Wananchi;
Napenda kuwahakikishia kuwa sisi katika Serikali tumetoa kipaumbele cha juu sana kwa elimu na kwamba hakuna upungufu wa utashi kwa upande wangu na wenzangu wote Serikalini. Ndiyo maana tumeguswa sana na matokeo haya. Bajeti ya elimu ya shilingi trilioni 3.6 ambayo ni sawa na asilimia 24 ya bajeti yote ya Serikali ndiyo kubwa kuliko zote. Kwa ajili hiyo imetuwezesha kuendelea kukabili mahitaji na changamoto za upanuzi mkubwa wa elimu ya sekondari na elimu ya juu. Bado hatujazimaliza changamoto zote na kwamba bado tuna kazi kubwa mbele yetu, lakini mafanikio yanaendelea kupatikana. Tutaendelea kutoa kipaumbele cha juu kwa elimu mpaka hapo itakapofikia mahali kwamba matatizo makubwa yatakapokuwa yamepungua sana.
Hitimisho
Ndugu Wananchi;

Mungu Ibariki Tanzania!
Mungu Ibariki Afrika!
Nashukuru kwa kunisikiliza!

RAIS KIKWETE ATEMBELEA MAKAO MAKUU YA JKT JIJINI DAR ES SALAAM LEO

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na uongozi wa juu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) jijini Dar es salaam alipotembelea Makao Makuu ya Jeshi hilo leo February 27, 2013. Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Vuai Shamsi Nahodha, Mkuu wa Majeshi Jenerali Davies Mwamunyange pia walihudhuria.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia makamanda wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) alipotembelea makao makuu yao leo February 27, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipokea zawadi ya saa toka kwa Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Meja Jenerali Raphael Muhuga huku Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Vuai Shamsi Nahodha, Mkuu wa Majeshi Jenerali Davies Mwamunyange wakishuhudia. Saa hiyo imeandaliwa na makamanda wa JKT kumpongeza Rais Kikwete kwa kurejesha mafunzo ya jeshi la ulinzi kwa mujibu wa sheria kuanzia mwaka huu.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na uongozi wa juu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) jijini Dar es salaam alipotembelea Makao Makuu ya Jeshi hilo leo February 27, 2013. Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Vuai Shamsi Nahodha, Mkuu wa Majeshi Jenerali Davies Mwamunyange pia wapo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akielekea kwenye uwanja wa sherehe baada ya kupata maelezo na kutoa maagizo kwa uongozi wa juu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) alipotembelea makao makuu yake leo February 27, 2013. Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Vuai Shamsi Nahodha na Mkuu wa Majeshi Jenerali Davies Mwamunyange pia walihudhuria.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na kada mbalimbali za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) alipotembelea leo February 27, 2013. 
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongozana na Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Meja Jenerali Raphael Muhuga,pamoja na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Vuai Shamsi Nahodha, Mkuu wa Majeshi Jenerali Davies Mwamunyange wakati akiondoka Makao Makuu ya Jeshi hilo leo. PICHA NA IKULU

Rais Kikwete akagua Ukumbi mpya Wa Mikutano wa Kimataifa jijini Dar es Salaam

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akikagua ukumbi mkubwa wa mikutano wa Julius Nyerere multi-purpose International conference Hall uliopo mtaa wa Shaaban Robert jijini Dar es Salaam. Ukumbi huo wa Serikali upo chini ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.


Ujenzi wa Ukumbi huo uko katika hatua za mwisho na Rais Kikwete mbali na kuridhishwa na hatua hiyo ametoa maelekezo kwa wahandisi kutenga sehemu maalumu kwa Wapiga picha na waandishi wa habari ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi.


Rais Kikwete pia ameelekeza wahandisi kuweka viti na meza zinazohamishika ili kukidhi matakwa ya mikutano na vikao vya aina mbalimbali. Picha na Freddy Maro.
Sehemu ya jukwaa kuu
Nafasi za wajumbe wa mikutano
Viti
Upande wa juu

Rais Kikwete afungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa maofisa waandamizi wa Jeshi la Polisi

 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa maofisa waandamizi wa Jeshi  la Polisi ulifanyika katika ukumbi wa Pius Msekwa mjini Dodoma jana.
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Maofisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi muda mfupi baada ya kufungua mkutano wao wa Mwaka uliofanyika katika ukumbi wa Pius Msekwa Mjini Dodoma jana Jioni,Kauli Mbiu ya mkutano Huo ni” Tujenge Uwezo wa Jamii na Polisi kukabiliana na Vurugu kwa Kuimarisha Utii wa Sheria Bila Shuruti,”.Walioketi Mbele ni.Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dkt.Emmanuel Nchimbi,Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi Saidi Mwema,Spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Anna Makinda na Naibu Spika Johna Ndugai.
Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akijadiliana jambo na Waziri wa Mambo ya Ndani Dkt.Emmanuel Nchimbi pamoja na Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi Saidi Mwema muda mfupi baada ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Maofisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi Mjini Dodoma jana. Picha na Freddy Maro wa Ikulu

Rais Kikwete azindua utoaji wa Vitambulisho vya taifa katika viwanja vya Karimjee leo

 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akibonyesha kitufe kuashiaria kuzindua
rasmi mfumo wa usajili na utambuzi wa watu na utoaji wa vitambulisho vya taifa
uliofnyika katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam leo.Watatu kushoto
ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Dkt.Emmanuel Nchimbi, kushoto ni Mkurugenzi
Mkuu wa NIDA Bwana Mwaimu na kulia nia Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Bwan Said
Meck Sadik.
 Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dkt.Emmanuel Nchimbi akimkabidhi Rais
Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete kitambukisho cha Taifa katika hafla ilkiyofanyika
katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam leo.
 Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dkt.Emmanuel Nchimbi akimkabidhi mke wa
Rais Mama Salma Kikwete kitambulisho chake cha Taifa katika viwanja vya
Karimjee leo huku Rais Kikwete akishuhudia.Kushot o Mkurugenzi Mkuu wa NIDA
Bwana Mwaimu
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Rais Mstaafu awamu ya pili
Mzee Ali Hassan Mwinyi kitambulisho chake cha taifa katika viwanja vya Karimjee
leo.
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Rais Mstaafu wa Zanzibar
Amani Abeid Karume kitambulisho chake cha taifa katika viwanja vya Karimjee
leo.
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Rais Mstaafu awamu ya Tatu
Benjamin William Mkapa kitambulkisho cha taifa katika viwanja vya Karimjee leo.
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Makamu wa Kwanza wa Rais wa
Zanzibar Maalim Seif Shariff Hamad kitambilisho cha Taifa katika viwanja vya
Karimjee leo wakati wa hafla ya Uzinduzi wa mfumo wa usajili na utambuzi wa
watu.
 Rais Kikwete akimkabidhi Kada wa CCM Mzee Kingunge Ngombale Mwiru
kitambulisho cha taifa.
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Dkt. Alex Malasusa kiongozi wa kanisa la KKKT
kitambulisho cha taifa.
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Shekhe Mkuu wa mkoa wa Dar es
Salaam Alhaj Elihad kitambulkisho cha taifa.
 Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete  akimkabidhi Mwenyekiti wa CUF
Professa Ibrahim Lipumba kitambukisho cha taifa.
 Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Mkurugenzi Mkuu wa NSSF
Dkt.Ramadhani Dau kitambulisho cha taifa leo katika viwanja vya Karimjee.
Rais Dkt.Jakaya Kikwete akimkabidhi mkurugenzi Mkuu wa PPF Bwana William
Erio kitambulisho cha taifa.

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akifurahi na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni wa PPF Bw.William Erio mara baada ya kupokea Kitambulisho cha Taifa

Baadhi ya wageni walioudhuria sherehe za uzinduzi wa Vitambulisho vya Taifa kutoka kushoto ni Kaimu Mhariri Mtendaji wa TSN Bw.Gabriel Nderumaki,Mkurugenzi Mkuu wa NSSF DKt.Ramadhani Dau,Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni wa PPF Bw.William Erio na Mkurugenzi Mkuu wa NHIF Bw.Emanuel Humba

Picha  na Freddy Maro  wa Ikulu

RAIS KIKWETE KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA SHERIA NCHINI

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na wanasheria  leo  Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na wanasheria  leo  Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia  leo Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini 
  Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na Jaji Mkuu Mhe Mohamed Chande Othman, Jaji Kiongozi  Mhe Fakihi Jundu, Jaji January Msofe, Spika Anne Makinda, Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Mathias Chikawe na Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Mhe. Saidi Mecky Sadik leo Februari 6, 2013 baada ya kuhutubia katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu leo Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini
 :Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Mchungaji Christopher Mtikila leo Februari 6, 2013 katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini. Kushoto ni Jaji Mkuu Mhe Mohamed Chande Othman
 Viongozi wa dini ya Kihindu wakielekea kwenye kipaza sauti ili kuomba dua leo Februari 6, 2013 wakati wa  maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini. Viongozi wa dini za Kiislamu na Kiktristo pia walishiriki kwenye maadhimisho hayo.

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na majaji wa Mahakama ya Rufaa leo Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini
  Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania leo Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na majaji wakuu wastaafu na viongozi wengine leo Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa dini pamoja na Naibu Mwanasheria Mkuu  Rais wa Mawakili leo Februari 6, 2013  katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini nje ya Mahakama Kuu ya Tanzania jijini

RAIS KIKWETE AZINDUA UJENZI WA UWANJA WA NDEGE WA KIGOMA LEO, PIA AKAGUA UJENZI WA DARAJA LA MALAGARASI

Rais Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na viongozi wengine akikata utepe kuzindua ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo Januari 4, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mkurugenzi mkazi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Uganda na Burundi Bw Phillipe Dongier, wakifunua kitambaa cha jiwe la msingi katika uzinduzi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo Januari 4, 2013.
Rais Kikwete akiongezana na mkurugenzi mkazi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Uganda na Burundi Bw Phillipe Dongier mara baada ya uzinduzi huo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi mbalimbali wakipata maelezo juu ya ujenzi wa uwanja wa ndege wa Kigoma toka kwa mhandisi George Sambali
wakati wa uzinduzi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo Januari 4, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisindikizwa na viongozi wengine baada ya uzinduzi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo Januari 4, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na wananchi wa Kigoma wakati wa uzinduzi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo Januari 4, 2013.
mkurugenzi mkazi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Uganda na Burundi,Bw. Phillipe Dongier akiongea na wananchi wa Kigoma wakati wa uzinduzi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo Januari 4, 2013.
Msanii Diamond na kundi lake wakitumbuiza wakati wa sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo Januari 4, 2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisikiliza maelezo ya Daraja la Maragarasi kutoka kwa Meneja wa Kampuni ya HANIL ambao ni Wakandarasi wa ujenzi wa Daraja hilo,Bw. Jung-Sik You kutoka nchini Korea,leo Januari 4,2013.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa ameongozana na Mama Salma Kikwete na maafisa mbali mbali wakikagua ujenzi wa Daraja la Mto Malagarasi lililopewa jina la Daraja la Kikwete mkoani Kigoma leo Februari 4, 2013. Asilimia zaidi ya 90 ya ujenzi wa daraja hilo zimekamilika nan linatarajiwa kufunguliwa baadaye mwaka huu.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Muungano eneo la Kibaoni wilayani Uvinza, Kigoma, akiwa njiani kuelekea mjini Kigoma, akitokea kukagua ujenzi wa daraja la Mto Malagarasi leo.Picha na IKULU.

MAMA SALMA KIKWETE AWASILI ARUSHA JIONI YA LEO ,TAYARI KWA KUFUNGA MKUTANO WA KIMATAIFA UNAOJADILI AFYA YA MAMA NA MTOTO

Mke wa Rais mama Salma Kikwete akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa
Arusha,Magesa Mulongo mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege
wa kimataifa wa Kilimanjaro(KIA)jioni ya leo,kesho atafunga mkutano wa
kimataifa juu afya ya mama katika ukumbi wa mikutano AICC.
Mke wa Rais mama Salma Kikwete akisalimiana na Katibu Tawala wa Mkoa
wa Arusha,Mama Itanisa mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege
wa kimataifa wa Kilimanjaro(KIA)jioni ya leo,kesho atafunga mkutano wa
kimataifa juu afya ya mama katika ukumbi wa mikutano AICC.
Mke wa Rais mama Salma Kikwete akisalimiana na Mkuu wa wilaya ya
Arusha,John Mongela mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa
kimataifa wa Kilimanjaro(KIA)jioni ya leo,kesho atafunga mkutano wa
kimataifa juu afya ya mama katika ukumbi wa mikutano AICC.
Mke wa Rais mama Salma Kikwete akisalimiana na Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Arusha,Liberatus Sabas mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa
ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro(KIA)jioni ya leo,kesho atafunga
mkutano wa kimataifa juu afya ya mama katika ukumbi wa mikutano AICC.
Mke wa Rais mama Salma Kikwete akiwapungia mkono waimbaji wa kikundi
cha Msanja cha jijini Arusha , mara baada ya kuwasili kwenye uwanja
wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro(KIA)jioni ya leo,kesho atafunga
mkutano wa kimataifa juu afya ya mama katika ukumbi wa mikutano
AICC.
Mke wa Rais mama Salma Kikwete akisalimiana na viongozi wa Umoja wa wanawake wa Chama cha Mapinduzi(UWT) Mkoa wa Arusha, mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro(KIA)jioni ya leo,kesho atafunga mkutano wa kimataifa juu afya ya mama katika ukumbi wa mikutano AICC.Picha zote na Filbert Rweyemamu

RAIS KIKWETE ATOA MILIONI 30 KWA MRADI WA KULEA NA KUHIFADHI MBWA MWITU KATIKA HIFADHI YA TAIFA YA SERENGETI MKOANI MARA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ametoa shilingi milioni 30 kuchangia mradi endelevu wa kulea na kuhifadhi mbwa mwitu waliokuwa wameanza kutoweka kabisa katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.

Mhe. Rais pia amezishukuru na kuzipongeza taasisi za umma na binafsi zinazoshiriki katika kuufanikisha mradi huo unaojulikana kama Vodacom Foundation Serengeti Wild Dogs Conservation Project.

“Juhudi hizi za kurudisha tena makundi ya mbwa mwitu kwenye mbuga hii inayojulikana kimataifa ni ya kupongezwa kwani itahakikisha kwamba wanyama hawa wanaendelea kuwepo Serengeti na pia itaongeza idadi ya vivutio vyetu vya utalii mbugani humu”, alisema Mhe. Rais.

Aliyasema hayo Jumapili Desemba 23, 2012 wakati wa sherehe za kuachiwa huru kundi la pili lenye mbwa mwitu 15 waliokuwa wamehifadhiwa kwa miezi kadhaa kwenye boma maalumu la mradi huo, lililojengwa katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.

“Nashukuru taasisi zote zinazounga mkono juhudi za serikali katika kuhakikisha kwamba mbwa mwitu wanakuwepo kwa wingi mbugani Serengeti kama ilivyo katika mbuga zingine”, aliongezea Mhe. Rais.

Katika taarifa yake wakati wa sherehe hizo, Mkurugenzi Mkuu wa Tawiri, Dk. Simon Mduma, alimueleza Rais Kikwete kuwa jumla ya Mbwa mwitu ishirini na sita (26), wamerudishwa mbugani hadi sasa, kufuatia kundi la kwanza la wanyama mwitu hao kumi na moja (11) kuachiwa siku ya Alhamisi Agosti 30, 2012.

Alitanabahisha kwamba mradi huo unaohusisha mbwa mwitu walioondolewa katika msitu wa Samunge wilayani Loliondo ni mojawapo ya juhudi za kurudisha tena makundi ya wanyama hao katika mbuga hiyo maarufu duniani, na kwamba baada ya kuhifadhiwa na hatimaye kuachiwa kwao huku wakiwa wamevishwa collar maalumu zenye redio ili kufuatilia nyendo zao, ni muendelezo wa juhudi za kupata makundi sita yenye mbwa mwitu takriban kumi (10) kila moja, ikiwa ni hatua endelevu ya muda mrefu ya kuhakikisha uwepo wa wanyama hao mbugani humo.

Dkt. Mduma alisema kundi la kwanza la mbwa mwitu hao kumi na moja (11) wote wapo hai na wanaendelea vizuri katika maisha yao mbugani humo, na kwamba pamoja na wanyama hao kutembelea hadi maskani yao ya awali ya Loliondo, malalamiko ya kuwapo kwa uharibifu wa mifugo sehemu hizo kama ilivyokuwa awali hayajaripotiwa hadi sasa.

Mkurugenzi Mkuu huyo wa utafiti wa wanyama pori alieleza kuwa mbwa mwitu wamekuwa wakitoweka kutokana na kuuawa kwa sumu na wananchi baada ya kula mifugo yao, ama kwa kuugua magonjwa mbalimbali kama vile kichaa cha mbwa.

“Hivi sasa kuna makundi 11 yanayofuatiliwa, manane yakiwa Loliondo na matatu katika Hifadhi ya Ngorongoro, yakifanya idadi ya mbwa mwitu kuwa 200″, alisema Dkt Mduma.

Aliongezea kuwa awali, katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti makundi ya mbwa mwitu yalikuwa yakionekana kwa wingi, lakini yamekuwa yakitoweka kwa kasi sana kiasi hata mara ya mwisho ni wanyama mwitu hao wawili tu walioonekana katika mbuga ya Serengeti mnamo mwaka 1998.

Mbwa mwitu ni miongoni mwa wanyamapori ambao wapo hatarini kutoweka duniani. Takwimu zinaonyesha kuwa katika Bara la Afrika kuna mbwa mwitu takriban 8,000 na kwamba Tanzania pekee inakadiriwa kuwa na wanyama hao 3,500 katika mbuga mbalimbali nchini, isipokuwa katika Hifadhi h ya Taifa ya Serengeti ambako walianza kutoweka kabisa kabla ya juhudi hizi za kuwarejesha kuanza.

Kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom imechangia dola za Marekani 450,000 kwa kipindi cha miaka mitatu ili kufanikisha mradi huo, ambao ulizinduliwa rasmi mwezi Julai mwaka 2011.

“Vodacom tunajisikia furaha sana kuwa sehemu ya juhudi za serikali katika kuimarisha sekta ya utalii ambayo kwa sasa mchango wake ni mkubwa sana kwa taifa”, alisema Bw. Salum Mwalimu, Meneja Uhusiano wa Nje wa Vodacom wakati wa sherehe za kuwarudisha mbugani mbwa mwitu hao 15.

Bw. Mwalimu alisema kampuni yake siku zote inalenga kubadili maisha ya watu na kwamba ni wazi kuimarika kwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti inayochangia kwa kiasi kikubwa sekta ya utalii nchini na ambayo inategemewa kwenye kuongeza pato la Taifa na ustawi wa watu ni jambo muhimu sana.

Taasisi zingine zinazoshiriki katika zoezi hilo ni Idara ya Utafiti wa Wanyamapori (TAWIRI), Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCCA), Frankfurt Zoological Society (FZS) , Grumeti Fund (GF) na Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika picha ya pamoja na wasimamizi na wafadhili wa mradi huo

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa  na wawakilishi wa Kampuni  ya simu za mkononi ya Vodacom ambayo imechangia  dola za Marekani 450,000 kwa kipindi cha miaka mitatu ili kufanikisha mradi huo, ambao ulizinduliwa rasmi mwezi Julai mwaka 2011. kushoto ni meneja wa mradi huo Bw. Emmanuel Masenga wa Taasisi ya Utafiti wa wanyama pori (TAWIRI).

Rais Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wa TANAPA Jumapili Desemba 22, 2012  akikata utepe katika boma maalumu la kulea na kuhifadhi mbwa mwitu  kuashiria rasmi kuachiwa huru kundi la pili la wanyama hao  15 waliokuwa wamehifadhiwa kwa miezi kadhaa kwenye boma maalumu la mradi huo,  lililojengwa katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara. 
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wa TANAPA Jumapili Desemba 22, 2012 wakiwa nje ya  boma maalumu la kulea na kuhifadhi mbwa mwitu akishuhudia kuachiwa huru kundi la pili la wanyama hao  15 waliokuwa wamehifadhiwa kwa miezi kadhaa kwenye boma maalumu la mradi huo,  lililojengwa katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.

 Mbwa mwitu wakirejea mbugani baada ya kuachiwa huru kundi la pili la wanyama hao  15 waliokuwa wamehifadhiwa kwa miezi kadhaa kwenye boma maalumu la mradi huo,  lililojengwa katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimpongeza Bw. Joseph Kaboya, mhifadhi wa  boma maalumu la mradi huo  katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara, kwa kufanikisha zoezi hilo kwa mara ya pili. Kushoto ni meneja wa mradi huo Bw. Emmanuel Masenga wa Taasisi ya Utafiti wa wanyama pori (TAWIRI).

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisindikizwa na Mkurugenzi Mkuu wa Tawiri, Dkt. Simon Mduma (kushoto kwake) na meneja wa mradi huo Bw. Emmanuel Masenga baada ya sherehe hizo eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wa TANAPA Jumapili Desemba 22, 2012  wakielekea kwenye sehemu ya boma maalumu la kulea na kuhifadhi mbwa mwitu muda mfupi kabla ya kuachiwa huru kundi la pili la wanyama hao  15 waliokuwa wamehifadhiwa kwa miezi kadhaa kwenye boma maalumu la mradi huo,  lililojengwa katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara. 
Wahifadhi wakifungua wigo wa senyenge  ili kuachia huru kundi la pili la mbwa mwitu  15 waliokuwa wamehifadhiwa kwa miezi kadhaa kwenye boma hilo maalumu la mradi huo,  lililojengwa katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.
Mbwa mwitu hao 15 wakitoka katika hifadhin waliokuwa wamehifadhiwa kwa miezi kadhaa kwenye boma hilo maalumu la mradi huo,  lililojengwa katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.PICHA NA IKULU.

RAIS KIKWETE ATUNUKU KAMISHENI KWA MAAFISA WANAFUNZI 192 NA KUFUNGUA MAKTABA YA CHUO CHA MAFUNZO YA KIJESHO MONDULI LEO

Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwasili katika uwanja wa gwaride wa Chuo Cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Arusha, leo Jumamosi Desemba 15, 2012 tayari kutunuku kamisheni kwa maafisa wanafunzi 192 waliohitimu chuoni hapo.
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikagua gwaride la maafisa wanafunzi katika Chuo Cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Arusha, leo Jumamosi Desemba 15, 2012 kabla ya kuwakutunuku kamisheni maafisa hao 192 waliohitimu chuoni hapo.
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikata utepe kufungua rasmi kamtaba ya kisasa katika Chuo Cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Arusha, leo Jumamosi Desemba 15, 2012 baada ya kuwakutunuku kamisheni maafisa hao 192 waliohitimu chuoni hapo.
Gwaride la maafisa wanafunzi katika Chuo Cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Arusha, leo Jumamosi Desemba 15, 2012 wakati wa kuwakutunuku kamisheni maafisa hao 192 waliohitimu chuoni hapo.
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa jukwaa kuuna maafisa wakuu wa jeshi.
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akitunuku kamisheni kwa maafisa wanafunzi 192 katika Chuo Cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Arusha, leo Jumamosi Desemba 15, 2012.
 Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete na mkewe Mama Salma Kikwete wakitembelea bweni namba 15 ambamo Rais Kikwete alikuwa akiishi wakati akiwa mafunzoni hapo katika Chuo Cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Arusha, leo Jumamosi Desemba 15, 2012 kabla ya kuwakutunuku kamisheni maafisa hao 192 waliohitimu chuoni hapo.
Mheshimiwa Rais naomba kukupiga picha msichana Shalom anamwambia Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika Chuo Cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Arusha, leo Jumamosi Desemba 15, 2012 baada ya kuwakutunuku kamisheni maafisa hao 192 waliohitimu chuoni hapo.PICHA NA IKULU

RAIS KIKWETE AZINDUA UJENZI WA BOMBA LA GESI ASILIA KUTOKA MTWARA-DAR ES SALAAM

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na ujumbe wa kampuni inayojenga bomba la gesi asilia kutoka Mtwata hadi Dar es salaam, Benki ya Exim ya China na viongozi waandamizi wa serikali alipowakaribisha Ikulu kwa mazungumzo baada ya uzinduzi rasmi wa ujenzi wa bomba hilo maeneo ya Kinyerezi jijini Dar es salaam.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizindua rasmi ujenzi wa bomba la gesi asilia toka Mtwara hadi Dar es salaam leo Novemba 8, 2012 maeneno ya Kinyerezi njijini Dar es salaam. Nyuma yake ni Makamu wa Rais Dkt Mohamed Ghalib Bilali.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Makamu wa Rais Dkt Mohamed Ghalib Bilali na viongozi wengine wakimsikiliza  Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo miundombinu ya  bomba la gesi asilia toka Mtwara hadi Dar es salaam leo Novemba 8, 2012 maeneno ya Kinyerezi njijini Dar es salaam. Nyuma yake ni Makamu wa Rais Dkt Mohamed Ghalib Bilali. PICHA NA IKULU

Rais Kikwete akagua miradi 19 katika wiki moja

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amerejea Dar es Salaam mchana wa leo, Jumanne, baada ya kumaliza ziara ya siku tisa katika mikoa minne ambako amekagua, kuanzisha ama kuzindua miradi 19 ya maendeleo na kutembea kiasi cha kilomita 2,770. 
Rais Kikwete amewasili Dar es Salaam akitokea Dodoma ambako amefanya ziara ya kikazi ya siku mbili baada ya kumaliza ziara katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Manyara na Singida. 
Katika Mkoa wa Kilimanjaro ambako Rais Kikwete alianzia ziara yake Oktoba 28, mwaka huu, miongoni mwa mambo mengine alikagua nyumba za wahanga wa maporomoko ya mwaka 2006 kwenye kijiji cha Goha na akafungua Kiwanda cha Kusindika Tangawizi kilichoko Mamba Miamba, Wilaya ya Same, na akafungua Shule ya Sekondari ya Kata ya Asha Rose Mingiro iliyoko mjini Mwanga. 
Miradi mingine aliyoifungua Rais Kikwete katika Mkoa wa Kilimanjaro ni uzinduzi wa barabara za Rombo Mkuu-Tarakea na Kwasadallah-Masama na akafungua Ofisi ya Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (NAO) mjini Moshi. 
Katika Mkoa wa Arusha, Rais Kikwete alizindua Hospitali ya Wilaya ya Arusha ya Olturumet, akazindua Mradi Mkubwa wa Uboreshaji wa Miji kwa kufungua barabara za Jiji la Arusha, akazindua Jiji la Arusha, akafungua rasmi Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela na akatembelea Kiwanda cha Nguo cha A-Z. 
Kabla ya kuondoka Mkoani Arusha, Rais Kikwete alifungua Shule ya Msingi ya Sokoine na kuzindua ukarabati mkubwa wa Barabara ya Minjingu-Arusha.Mkoani Manyara, Rais Kikwete alifungua rasmi Barabara ya Singida-Minjingu-Arusha, akazindua mradi mkubwa wa maji wa Mji wa Babati na akaweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Barabara ya Babati-Bonga.

Mkoani Singida, Rais Kikwete alizindua mradi mkubwa wa maji wa Mwankoko kwa ajili ya Mji wa Singida, akaweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Barabara ya Manyoni-itigi-Chaya na akafungua Barabara ya Issuna-Manyoni.Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu.

Dar es Salaam.

6 Novemba, 2012

RAIS KIKWETE AZINDUA MIRADI YA BARABARA MANYONI-ITIGI-CHAYA na ISSUNA-MANYONI MKOANI SINGIDA LEO

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikata utepe kufungua rasmi barabara ya Issuna-Manyoni akiwa na viongozi wa serikali na wa TANROADS pamoja na wabunge wa mkoa wa Singida.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizindua ujenzi wa Barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya mkoani Singida leo. Pembeni yake kulia ni Waziri wa Ujenzi Dkt John Pombe Magufuli.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipozi na viongozi wa serikali na wa kampuni ya ujenzi baada ya kuzindua ujenzi wa Barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya mkoani Singida leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati wa sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa Barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya mkoani Singida leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikata utepe kuzindua ujenzi wa Barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya mkoani Singida leo.
Sehemu ya barabara mpya karibu na mji wa Manyoni iliyozinduliwa leo na Rais Kikwete.
Sehemu ya barabara mpya iliyozinduliwa na Rais Kikwete karibu na mji wa Katesh mkoani Manyara.
Sehemu ya barabara mpya iliyozinduliwa na Rais Kikwete mkoani Manyara.PICHA NA IKULU

RAIS JAKAYA KIKWETE ZIARANI JIJINI ARUSHA

Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika Tonia Kandiero na viongozi wengine wakikata utepe kuzindua barabara ya Minjingu-Babati-Singida nje kidogo ya mji wa Babati Mkoa wa Manyara. Anayeshuhudia kushoto ni Waziri wa Ujenzi Dkt John Pombe Magufuli na kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwezeshaji) Dkt Mary Nagu.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Mkurugenzi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Uganda na Burundi Bw. Philippe Dongier wakiweka jiwe la msingi kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa barabara ya Arusha Minjingu maeneo ya kijiji cha Mguu-wa-Zuberi wilayani Monduli, Mkoani Arusha.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika Tonia Kandiero wakifurahia baada ya kuzindua barabara ya Minjingu-Babati-Singida nje kidogo ya mji wa Babati Mkoa wa Manyara. Anayeshuhudia kushoto ni Waziri wa Ujenzi Dkt John Pombe Magufuli na kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwezeshaji) Dkt Mary Nagu.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe Frederick Sumaye wakati wa mkutano wa hadhara mjini Katesh mkoani Manyara.
Mkurugenzi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Uganda na Burundi Bw. Philippe Dongier akipanda mti kama kumbukumbu baada ya Rais Kikwete kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa barabara ya Arusha Minjingu maene ya kijiji cha Mguu-wa-Zuberi wilayani Monduli, Mkoani Arusha.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Mkurugenzi wa Benki ya Dunia kwa nchi za Tanzania, Uganda na Burundi Bw. Philippe Dongier wakielekea kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa barabara ya Arusha Minjingu maeneo ya kijiji cha Mguu-wa-Zuberi wilayani Monduli, Mkoani Arusha.
Rais Kikwete akisalimiana na baadhi ya wanahabari wa mkoa wa Arusha baada ya kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa barabara ya Arusha Minjingu maene ya kijiji cha Mguu-wa-Zuberi wilayani Monduli, Mkoani Arusha.
Rais Kikwete akisalimiana na baadhi ya wanahabari wa mkoa wa Arusha baada ya kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa barabara ya Arusha Minjingu maene ya kijiji cha Mguu-wa-Zuberi wilayani Monduli, Mkoani Arusha.
Sehemu ya barabara ya Minjingu-Babati-Singida iliyozinduliwa na Rais Kikwete.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Mbunge wa Viti Maalum (CHADEMA) Mhe Rose Kamili baada ya kuzindua mradi mkubwa wa maji wa Mwakonko Singida Mjini.PICHA NA IKULU

Rais Kikwete azindua mradi wa kuboresha na kuendeleza miji ya Tanzania jijini Arusha

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Alhamisi, Novemba Mosi, 2012, amezindua rasmi mradi mkubwa wa kuboresha na kuendeleza miji ya Tanzania unaojulikana kama Mradi wa Uboreshaji Miji ya Tanzania (Tanzania Strategic Cities project – TSCP) utakaogharimu mabilioni ya fedha. 

Aidha, Rais Kikwete amezidua rasmi Jiji la Arusha katika sherehe ya kufana iliyofanyika kwenye Mnara wa Azimio la Arusha katikati ya jiji hilo.
Mradi wa TSCP unalenga kuboresha huduma za msingi katika miji saba na Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA) kwa kujenga upya, kukarabati na kupanua miundombinu pamoja na kuijengea uwezo wa kukusanya na kusimamia mapato ya miji husika. 

Mradi huo ni mmoja ya miradi mitatu inayogharimiwa na Benki ya Dunia kwa nia ya kuboresha miji ya Tanzania. Mbali na TSCP, miradi mingine ni Mradi wa Uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam (Dar es Salaam Metropolitan Development Project – DMDP) na Urban Local Government Strengthening Programme (ULGSP). Mpaka sasa Benki hiyo imekwishakutoa sh bilioni 8.76 kati ya sh bilioni 34.7 za TSCP. 

Chini ya TSCP ambao unagharimu kiasi cha sh bilioni 191.3 miji itakayonufaika ni Tanga, Arusha, Mwanza, Kigoma, Dodoma, Mbeya, Mtwara na CDA ambayo ndiyo itakayopata pesa kubwa zaidi kuliko mjini mingine.
Aidha, chini ya TSCP, miji hiyo itajengewa miundombinu ya barabara zenye jumla ya kilomita 141.2, ujenzi wa madampo matano, ununuzi wa vifaa vya kusimamia taka ngumu, vituo vya mabasi sita, vituo viwili vya kuegesha malori na kilomita 15.9 za mitaro ya maji ya mvua.
Katika mji wa Arusha, kiasi cha barabara za lami zenye urefu wa kilomita 7.23 zitajengwa, mtaro mkubwa wa maji ya mvua wa mita 800 utajengwa, zitafungwa taa za kuongoza magari kwenye makutano ya barabara tatu ambazo ni Sokoine na Viwandani, Sokoine na Esso na Kanali Middleton na Makongoro. Katika awamu ya pili, kiasi cha barabara zenye urefu wa kilomita 7.8 zitajengwa katika Jiji la Arusha. 

Miji itakayonufaika na ULGSP ambako Benki ya Dunia inatoa mkopo wa dola za Marekani milioni 255 na unatarajiwa kuanza katika mwaka ujao wa fedha ni Morogoro, Tabora, Moshi, Sumbawanga, Shinyanga, Songea, Singida, Musoma, Iringa, Bukoba, Lindi, Njombe, babati, Kibaha, Mpanda, Geita, Korogwe na Bariadi.
DMDP kwa ajili ya Jiji la Dar Es Salaam, itahusika wilaya zote tatu za Kinondoni, Ilala na Temeke na utagharimu kiasi cha dola za Marekani milioni 75. 

Baada ya kuzindua mradi huo wa TSCP, Rais Kikwete amezindua Jiji la Arusha ambalo linapanda hadhi kutoka Manispaa. Katika uzinduzi huo, Rais amezindua nembo ya Jiji pamoja na kukabidhi cheti cha kulipandisha hadhi Jiji hilo.
Rais Kikwete amezindua miradi hiyo ikiwa ni shughuli zake katika siku ya kwanza ya ziara yake ya siku mbili kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Arusha. Rais amewasili Arusha mchana wa leo kutoka Dodoma.
 

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akilakiwa na Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mhe. John Mongella kuzindua rasmi mradi mkubwa wa kuboresha na kuendeleza miji ya Tanzania
Rais Kikwete akizindua rasmi mradi mkubwa wa kuboresha na kuendeleza miji ya Tanzania
bango la mradi mkubwa wa kuboresha na kuendeleza miji ya Tanzania
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Mbunge wa Arumeru Mashariki,Mh. Joshua Nassari





Rais Jakaya Mrishi Kikwete akisalimiana na wananchi wa Mji wa Arusha wakati alipokuwa akiwasili kwenye uzinduzi rasmi wa jiji la Arusha.
Waziri wa Ujenzi,Mh. John Magufuli akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa jiji la Arusha uliofanywa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete.

RAIS KIKWETE AZINDUA UJENZI WA BARABARA YA KWA SADALA-MASAMA, WILAYANI HAI,LEO

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipokewa na Mkuu wa Wilaya ya Hai Mhe Novatus Makunga katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.Katikati yao ni Waziri wa Ujenzi,Mh. John Magufuli.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipongezwa na wananchi katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.Kulia ni Waziri wa Ujenzi,Mh. John Magufuli.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimpongeza Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe kwa hotuba nzuri ya kumkaribisha na kumsifia kwa kazi anayofanya katika maendeleo ya miundombinu nchini katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe Leonidas Gama na Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wananchi katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisaidiwa kuzindua jiwe la msingi na Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipongezwa na kupewa shukurani na Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.Kushoto ni Waziri wa Ujenzi,Mh. John Magufuli.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Waziri wa Ujenzi, Mhe John Pombe Magufuli Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe Leonidas Gama na Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe wakikata utepe mojawapo ya magreda katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisindikizwa na Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe kutoka katika eneo la sherehe za uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Waziri wa Ujenzi Mhe John Pombe Magufuli Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe Leonidas Gama na Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA Mhe Freeman Mbowe katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa Mkoa wa Kilimanjaro baada ya uzinduzi wa ujenzi wa barabara ya Kwa Sadala-Masama wilayani hai leo.PICHA NA IKULU.

RAIS KIKWETE AFUNGUA RASMI BARABARA YA MKUU ROMBO-TARAKEA

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisaidiwa na Mbunge wa Rombo Mhe Joseph Selasini kukunjua pazia kama ishara ya kufungua rasmi wa barabara ya KM32 kutoka Mkuu Rombo hadi Tarakea leo Oktoba 30, 2012 kijijini Tarakea, wilaya ya Rombo mkoa wa Kilimanjaro ambako Rais Kikwete yuko katika ziara ya kikazi ya siku nne.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipongezwa na Mbunge wa Rombo Mhe Joseph Selasini kukunjua pazia kama ishara ya kufungua rasmi wa barabara ya KM32 kutoka Mkuu Rombo hadi Tarakea leo Oktoba 30, 2012 kijijini Tarakea, wilaya ya Rombo mkoa wa Kilimanjaro ambako Rais Kikwete yuko katika ziara ya kikazi ya siku nne.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete na washika dau wa miundombinu wakikata utepe ishara ya kufungua rasmi wa barabara ya KM32 kutoka Mkuu Rombo hadi Tarakea leo Oktoba 30, 2012 kijijini Tarakea, wilaya ya Rombo mkoa wa Kilimanjaro ambako Rais Kikwete yuko katika ziara ya kikazi ya siku nne.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akifurahia jambo na Mbunge wa Rombo Mhe Joseph Selasin katika hafla ya ufunguzi rasmi wa barabara ya KM32 kutoka Mkuu Rombo hadi Tarakea leo Oktoba 30, 2012 kijijini Tarakea, wilaya ya Rombo mkoa wa Kilimanjaro ambako Rais Kikwete yuko katika ziara ya kikazi ya siku nne.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea kabla ya kufungua rasmi wa barabara ya KM32 kutoka Mkuu Rombo hadi Tarakea leo Oktoba 30, 2012 kijijini Tarakea, wilaya ya Rombo mkoa wa Kilimanjaro ambako Rais Kikwete yuko katika ziara ya kikazi ya siku nne.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea katika moja ya maongezi yake na wananchi wakati alipokuwa akisimamishwa karibu kila kijiji wakati wa ziara yake Wilaya ya Same.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea katika moja ya maongezi yake na wananchi wakati alipokuwa akisimamishwa karibu kila kijiji wakati wa ziara yake Wilaya ya Same.PICHA NA IKULU.

RAIS KIKWETE AONGOZA KIKAO CHA KAZI KWA MAWAZIRI NA MAAFISA WAANDAMIZI WA SERIKALI

Rais Jakaya Mrisho kikwete na Waziri Mkuu Mhe. Mizengo Pinda wakipitia Waraka wa Utumishi Namba 5 wa mwaka 2009 kuhusu matumizi bora na salama ya vifaa na mifumo ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEKNOHAMA) serikalini wakati wa kikao cha kazi (retreat) cha siku tatu cha
Mawaziri, Manaibu Mawaziri na maafisa waandamizi wa serikali kujadili mikakati endelevu na utekelezaji wa sasa na wa baadae katika ukumbi wa
St Gaspar mjini Dodoma.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongoza kikao cha kazi (retreat) cha siku tatu cha Mawaziri, Manaibu Mawaziri na maafisa waandamizi wa serikali
wanaokutana kujadili mikakati endelevu na utekelezaji wa sasa na wa baadae katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma. Pamoja naye meza kuu ni
Makamu wa Rais Dkt Mohamed Ghalib Bilali (kulia) na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue.
Dk. Jabir Kuwe Bakari, Mtendaji Mkuu, Wakala ya Serikali Mtandao, akitoa mada kuhusu wakala huo kwa wajumbe kikao cha kazi (retreat) cha siku
tatu cha Mawaziri, Manaibu Mawaziri na maafisa waandamizi wa serikali kujadili mikakati endelevu na utekelezaji wa sasa na wa baadae katika
ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma.
Wajumbe wakichangia katika kikao cha kazi (retreat) cha siku tatu cha Mawaziri,Manaibu Mawaziri na maafisa waandamizi wa serikali wanaokutana kujadili mikakati endelevu na utekelezaji wa sasa na wa baadae ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma.
Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. George Yembesi akifafanua juu ya Waraka wa Utumishi Namba 5 wa mwaka 2009 kuhusu matumizi bora na salama ya vifaa na mifumo ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEKNOHAMA) serikalini kwa wajumbe kikao cha kazi (retreat) cha siku tatu cha Mawaziri, Manaibu Mawaziri na maafisa waandamizi wa serikali kujadili mikakati endelevu na utekelezaji wa sasa na wa baadae katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma.PICHA NA IKULU.

Rais Kikwete amteua Meja Jenerali Samuel Albert Ndomba kuwa Mnadhimu Mkuu wa JWTZ, Jenerali Raphael Mugoya Muhuga kuwa mkuu wa JKT

 


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mheshimiwa Jakaya
Mrisho Kikwete amemteua Meja Jenerali Samuel Albert Ndomba  (pichani kushoto) kuwa Mnadhimu Mkuu
wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Aidha,
Rais Kikwete amempandisha cheo Meja Jenerali Ndomba kuwa Luteni Jenerali. 
Taarifa
iliyotolewa leo, Ijumaa, Septemba 21, 2012, mjini Dar Es Salaam na Katibu Mkuu
Kiongozi Balozi Ombeni Y. Sefue kupitia Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais –
Ikulu, imesema kuwa uteuzi huo unaanza leo.

Taarifa
hiyo ya Balozi Sefue imesema kuwa kabla ya uteuzi wake, Meja Jenerali Ndomba
alikuwa Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).

Jenerali
Ndomba anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Luteni Jenerali Abdulrahman  A. Shimbo ambaye amestaafu Jeshi kwa mujibu
wa sheria baada ya kufikisha umri wa miaka 60.
            
Taarifa ya Balozi Sefue pia imesema
kuwa Rais Kikwete amemteua Brigedia Jenerali Raphael Mugoya Muhuga (pichani kulia) kuwa Mkuu wa
Jeshi la Kujenga Taifa kuanzia leo, Ijumaa, Septemba 21, 2012.
 
    

 

  Aidha,
Rais Kikwete amempandisha cheo Brigedia Jenerali Muhuga kuwa Meja Jenerali. 
Kabla
ya uteuzi wake, Brigedia Jenerali Muhuga alikuwa Mkuu wa Utawala na Mafunzo wa
Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Imetolewa
na
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
21 Septemba, 2012

Rais Kikwete azindua ujenzi wa Daraja la Kigamboni

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiweka jiwe la msingi kuashiria kuzindua rasmi ujenzi wa Daraja la Kigamboni katika hafla iliyofanyika huko Kurasini jijini Dar es Salaam.Kushoto ni Waziri wa Ujenzi Dkt.John Pombe Magufuli na wapili kulia ni mkurugenzi Mkuu wa NSSF Dkt.Ramadhani Dau.NSSF itatoa asilimia 60 za ujenzi wa daraja hilo na serikali itatoa asilimia 40

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akisisitiza jambo wakati akiongea na Waziri wa Ujenzi Dkt.John Pombe Magufuli wakati wa hafla ya
uzinduzi wa Ujenzi wa Daraja la Kigamboni uliofanyika huko Kurasini jijini Dar es Salaam.Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Said Meck
Sadik

Waziri wa Ujenzi Dkt.John Pombe Magufuli akimpa maelezo Raid Dtk.Jakaya Mrisho Kikwete juu ya Ujenzi wa Daraja la Kigamboni wakati wa
hafla ya uzinduzi wa ujenzi wa Daraja hilo ulofanyika Kurasini jijini Dar ea Salaam.

Rais Kikwete aweka jiwe la msingi kuzindua rasmi ujenzi wa Barabara ya Bagamoyo-Msata

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiweka jiwe la msingi kuzindua rasmi ujenzi wa Barabara ya Bagamoyo-Msata uliofanyika katika kijiji cha Kiwangwa wilayani Bagamoyo leo mchana.Wengine katika picha kutoka kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Ahmed Kipozi, Kaimu Mkuu wa mkoa wa Pwani ambaye pia ni mkuu  wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik(Wapili kushoto),Waziri wa Ujenzi Dkt.John Pombe Magufuli(wanne kushoto) na kulia ni Waziri wa Mazingira Mhe. Theresa Hoviza.

Ndoto ya miaka mingi ya kujengwa kwa barabara ya Msata-Bagamoyo kwa kiwango cha lami imetimia leo, Jumanne, Septemba 18, 2012, wakati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alipoweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa barabara hiyo katika sherehe kubwa iliyofanyika eneo la Kiwangwa.

Barabara hiyo ya kilomita 64 inajengwa na mkandarasi wa ndani ya nchi, Estim Construction, na inagharimiwa asilimia mia na Serikali ya Tanzania bila msaada kutoka kwa mfadhili yoyote.
Akizungumza kwenye sherehe hiyo, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania, Injinia Patrick L. Mfugale amesema kuwa barabara hiyo inayogharimu kiasi cha Sh. bilioni 94, ikiwa ni pamoja na fedha za fidia na kumlipa mkandarasi mshauri, itakamilika Juni mwakani.
Pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais ameweka jiwe la msingi kwenye barabara hiyo, Injinia Mfugale amesema kuwa mkandarasi wa sasa alianza ujenzi tokea 2010 baada ya usanifu wa barabara hiyo kukamilika na baada ya Serikali kumtimua mkandarasi wa mwanzo wa barabara hiyo, TACOPA, Novemba 13, mwaka 2009.
Amesema kuwa mpaka sasa barabara hiyo imekamilika kwa asilimia 65, yaani kwamba kiasi cha kilomita 36.7 tayari zimewekwa lami na kuwa ni kilomita 23 zilizosalia na ambazo zitamalizika katika miezi tisa ijayo.
Injinia Mfugale amesema kuwa mpaka sasa Serikali imekwishakulipa kiasi cha Sh. bilioni 56.8 ikiwa ni pamoja na fedha iliyolipwa kama fidia kwa wananchi ili kupisha ujenzi wa barabara hiyo.
Amesema kuwa ujenzi wa barabara hiyo hautahusisha ujenzi wa daraja kwenye Mto Ruvu kwa sababu usanifu wa daraja hilo ulichelewa kidogo kukamilika hata kama tayari sasa umekamilishwa.
Akizungumza kwenye sherehe hiyo, Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa John P. Magufuli amesema kuwa ujenzi wa barabara hiyo ni sehemu ya ujenzi wa kilomita 11,154 za barabara za lami zinazojengwa na Serikali ya Mheshimiwa Kikwete.
“Nataka muelewe vizuri maana ya kilomita hizi. Wakati wa Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961, tulikuwa na barabara za lami zenye urefu wa kilomita 1,330. Kati ya Uhuru na mwaka 2005, tulijenga barabara zenye urefu wa kilomita 6,500 na kati ya 2005 na sasa tunajenga barabara zenye urefu wa kilomita 11,154,” amesema Waziri Magufuli.
Waziri huyo amerudia msimamo wake kuwa kamwe Serikali haitawaachia watu wanaojenga ama kufanya shughuli katika eneo la hifadhi ya barabara bila kuwachukulia hatua.
Naye Rais Kikwete amewaambia mamia kwa mamia ya wananchi walioshiriki katika sherehe hizo kuwa barabara ndiyo mishipa ya damu ya uchumi wa nchi yoyote na ndiyo maana Serikali inatenga kiasi kikubwa katika Bajeti yake kwa ajili ya ujenzi wa barabara.
 Amesema kuwa katika Bajeti ya sasa, barabara zimetengewa kiasi cha Sh. trilioni 2.2 ambacho ni kiasi kikubwa cha pili baada ya Bajeti ya elimu.
Rais Kikwete amesema kuwa pamoja na faida zake kubwa na nyingi, barabara hiyo itakuwa na changamoto zake ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa ajali za barabara, kuongeza urahisi wa kusambaa kwa ugonjwa wa ukimwi na hata kuvutia watu wenye lengo la kununua ardhi kubwa ya wanavijiji ambako inapita barabara hiyo.
Rais pia ameungana na Waziri Magufuli kwa kuonya: “Kama alivyosema Waziri, wanaoifuata barabara watavunjiwa nyumba zao na hawatalipwa, lakini wale ambao barabara inawafuata watalipwa hata wakivunjiwa.”

Rais Kikwete aishukuru Vodacom kwa kuchangia katika mradi wa kuhifadhi mbwa mwitu Hifadhi ya Taifa ya wanyama ya Serengeti

 Mtunzaji wa Mbwa Mwitu akiandaa mlo wa mwisho kwa wanyama hao 11 kabla hawajarejeshwa
mbugani siku ya Alhamisi Agosti 30, 2012  baada ya kuhifadhiwa kwenye boma maalumu la mradi huo,  
katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara.
 Mbwa mwitu hao wakijipatia mlo wao wa mwisho kabla ya kuachiliwa huru
 Ni vuta nikuvute
 Mlo ukiendelea
 Si ugomvi bali ni namna yao ya kupata mlo
 Mkuu wa Vodacom Foundation Bw Yesaya Mwakifulefule akiangalia
Mbwa Mwitu hao wakijipatia mlo wa mwisho 
 Hatimaye Mbwa Mwitu hao wakiondoka bomani na kuingia mbugani wakiwa wanyama
huru baada ya kuhifadhiwa kwa mwaka mmoja katika boma hilo la  mradi wa kuhifadhi
mbwa mwitu katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mradi unaojulikana kama Vodacom
Foundation Serengeti Wild Dogs Conservation Project
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom hapa nchini
Bw.  Rene Meza, Ikulu  Dar-Es-Salaam, walipokutana jana jioni, Ijumaa Agosti 31,2012  
kwa mchango wa kampuni hiyo ya simu za mkononi  katika mradi wa
kuhifadhi mbwa mwitu katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti, (Vodacom Foundation
Serengeti Wild Dogs Conservation Project), ambayo ilichanga
dola za Marekani 450,000 kwa kipindi cha miaka mitatu.
=============================================

Rais Jakaya Mrisho Kikwete ameishukuru kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom kwa kuchangia katika mradi wa kuhifadhi mbwa mwitu katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mradi unaojulikana kama Vodacom Foundation Serengeti Wild Dogs Conservation Project, kwa dola za Marekani 450,000 kwa kipindi cha miaka mitatu.

 Rais ametoa shukrani hizo Kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom hapa nchini Bw.  Rene Meza, Ikulu  Dar-Es-Salaam, walipokutana jana jioni, Ijumaa Agosti 31,2012

 ”Napenda kutoa shukrani zangu kwa Vodacom kwa msaada huu mkubwa, tunashukuru kwa jitihada zenu kubwa katika hili” Rais amesema.

 Naye Mtendaji Mkuu wa Vodacom amemhakikishia Rais kuwa kampuni yake itaendelea kushirikiana na serikali katika miradi mbalimbali ya maendeleo, elimu na Afya. 

“Tunajisikia faraja sana kuwa miongoni mwa washirika wa mradi huu. Ni heshima kwetu na tuko makini nao, tunataka kuendelea na mradi huu” Bw, Rene Meza amemhakikishia Rais.

Tayari mbwa mwitu kumi na Moja, wamerudishwa mbugani siku ya Alhamisi Agosti 30, 2012  baada ya kuhifadhiwa kwenye boma maalumu la mradi huo,  katika eneo la Nyamuma, Magharibi mwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, mkoani Mara. 

Wadau wengine walioshiriki na kufanikisha zoezi hilo ni pamoja na Idara ya Wanyamapori, Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya  Ngorongoro (NCCA),  Frankfurt Zoological Society , Grumeti Fund na Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro. 

Kuachiwa kwa Mbwa Mwitu hao 11 walioondolewa katika msitu wa Samunge wilayani Loliondo ni mojawapo ya juhudi za kurudisha tena makundi ya wanyama hao katika mbuga hiyo maarufu duniani. Hivi sasa kuna makundi 11 yanayofuatiliwa, manane yakiwa Loliondo na matatu katika Hifadhi ya Ngorongoro, yakifanya jumla ya Mbwa Mwitu 200. 

Mtafiti wa Magonjwa ya Wanyama kutoka Taasisi ya Utafiti wa Wanyama (TAWIRI) Dkt. Ernest Mjingo, alimwambia Rais Kikwete kwamba katika Hifadhi ya Serengeti makundi ya Mbwa Mwitu yalikuwa yakionekana kwa wingi, lakini sasa yametoweka na mara ya mwisho Mbwa Mwitu wawili walionekana mwaka 1998. 

Mtafiti huyo  alisema Mbwa Mwitu wamekuwa wakitoweka kutokana na kuuawa kwa sumu na wananchi baada ya kula mifugo yao na kuugua  magonjwa mbalimbali kama kichaa cha mbwa. 

Dkt. Mjingo alisema baada ya kuachiwa Mbwa Mwitu hao, waliovishwa collar maalumu zenye redio,  juhudi zitaendelea ili kupata makundi sita yenye Mbwa Mwitu takriban kumi kila moja, ikiwa ni hatua endelevu ya muda mrefu ya kuhakikisha  uwepo wa wanyama hao mbugani humo. 

Mbwa Mwitu ni miongoni mwa wanyamapori ambao wapo hatarini kutoweka duniani. Takwimu zinaonyesha kuwa  katika Bara la Afrika kuna Mbwa Mwitu wanaofikia 8,000 na Tanzania pekee inakadiriwa kuwa  wanyama hao 3,500 katika mbuga mbalimbali nchini. Katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti walitoweka kabisa kabla ya juhudi hizi za kuwarejesha kuanza.

HOTUBA YA MHESHIMIWA DK JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWA WANANCHI KUHAMASISHA SENSA YA WATU NA MAKAZI, TAREHE 25 AGOSTI, 2012

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisoma hotuba ya kuwahamasisha wananchi kushiriki Sensa ya Watu na Makazi kwa mwaka 2012.

Ndugu wananchi;

Imekuwa ni mazoea yetu kuwa Rais huzungumza na taifa kila mwisho wa mwezi. Lakini, leo nazungumza nanyi siku saba kabla ya mwisho wa mwezi kwa sababu maalum. Sababu yenyewe si nyingine bali ni Sensa ya Watu na Makazi itakayofanyika kwa siku saba kuanzia kesho Jumapili tarehe 26 Agosti, 2012. Shabaha yangu ni kutaka kuwakumbusha Watanzania wenzangu wote kuhusu wajibu wao wa kujitokeza kuhesabiwa siku hizo. Naomba kila mmoja wetu ahakikishe kuwa anakuwepo kuhesabiwa na kujibu maswali yote yatakayoulizwa na makarani wa sensa kwa ufasaha.

Ndugu wananchi;

Katika historia ya nchi yetu, Sensa ya mwaka huu itakuwa ni ya tano tangu Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961, Mapinduzi ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari, 1964 na kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 26 Aprili, 1964. Sensa nyingine zilifanyika mwaka 1967, 1978, 1988 na 2002. Kumbukumbu zinaonesha kuwa kwa upande wa Tanzania Bara wakati wa ukoloni zilifanyika Sensa mwaka 1910, 1931, 1948 na 1957. Kwa upande wa Zanzibar wakati wa ukoloni na utawala wa Sultan kulifanyika Sensa mara moja mwaka 1958.

Ndugu Wananchi;

Kama ilivyokuwa kwa Sensa zilizotangulia, madhumuni makubwa ya Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 ni kujua idadi ya watu, mahali walipo, jinsia zao, umri wao, elimu, shughuli wazifanyazo, vipato vyao, upatikanaji wa huduma mbalimbali pamoja na makazi. Taarifa hizi hutumiwa na Serikali kupanga mipango ya maendeleo, kutengeneza programu mbalimbali na kubuni miradi ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini. Aidha, huisaidia Serikali kupanga na kupeleka huduma za kiuchumi na kijamii kwa wananchi kwa kuzingatia mahitaji halisi ya maeneo yao wanayoishi kwa mujibu wa idadi yao na mgawanyiko wao kijinsia, kiumri na huduma zinazohitajika. Hivyo basi, idadi halisi isipojulikana kuna hatari ya wananchi kukosa huduma wanazohitaji kwa kiwango kinachostahili. Vilevile, takwimu hizi hutumiwa na Serikali katika kufikia uamuzi wa kugawa majimbo ya uchaguzi na maeneo ya utawala kama vile mikoa, wilaya, kata, vijiji na vitongoji vipya.

Ndugu wananchi;

Pamoja na umuhimu huo wa jumla wa Sensa kwa maendeleo ya nchi yetu, Sensa ya mwaka 2012 ina umuhimu wa aina yake. Taarifa zake zitatumika kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa Dira za Taifa za Maendeleo za Tanzania Bara na Zanzibar; Mkakati wa Kukuza na Kupunguza Umaskini Tanzania Bara (MKUKUTA II); Mkakati wa Kupunguza Umaskini Zanzibar (MKUZA II); na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa 2011/12 – 2015/16. Vilevile taarifa zitakazopatikana zitatumika kupima maendeleo ya utekelezaji wa Malengo ya Milenia (Millenium Development Goals) yaliyowekwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 2000. Kama tujuavyo, itakapofika mwaka 2015 ndicho kilele cha utekelezaji wa Malengo hayo hivyo kujua hatua tuliyofikia sasa itasaidia kujipanga vizuri katika miaka mitatu iliyosalia.

Ndugu Wananchi;

Pamoja na faida hizo, taarifa za Sensa hii zitasaidia kufanikisha zoezi linaloendelea sasa, la kuwapatia Watanzania vitambulisho vya taifa. Baadhi ya maswali yatakayoulizwa kwenye Sensa ya Watu na Makazi yatasaidia katika kuhakiki maombi ya vitambulisho vya taifa. Bila ya shaka sote tunatambua vyema manufaa ya vitambulisho vya taifa, hivyo basi ndugu yangu, shiriki zoezi la sensa ili kuirahisishia Serikali kazi ya utoaji wa vitambulisho kwa raia wake.

Ndugu wananchi;

Shughuli yoyote kukabiliwa na changamoto mbalimbali ni jambo la kawaida. Lakini, tofauti na miaka ya nyuma, Sensa ya mwaka huu imekabiliwa na changamoto ambazo hazijawahi kuwepo. Kuna baadhi ya wenzetu wamekuwa wanafanya jitihada za makusudi za kutaka kulivuruga zoezi la Sensa nchini. Wamekuwa wanawashawishi watu wasishiriki kuhesabiwa, kwa sababu ambazo baadhi yake hazina uhusiano wo wote na Sensa. Zipo sababu nyingine ambazo hata haziingii akilini. Kwa mfano, wapo watu wanaodai kuwa hawatashiriki Sensa mpaka mjusi aliyeko kwenye Jumba la Makumbusho kule Berlin, Ujerumani atakaporudishwa. Kinachozungumzwa hapa ni mabaki ya mifupa ya mnyama wa kale aliyekuwepo hapa nchini zaidi ya miaka milioni 200 iliyopita. Mwaka 1906 wana sayansi wa Kijerumani waliyagundua mabaki hayo kule Tendaguru, Lindi, wakayafukua na kuyapeleka Ujerumani ambako yamehifadhiwa tangu wakati huo.

Ndugu Wananchi;

Kudai mifupa hiyo irejeshwe nchini si jambo baya, watu wataona wanyama wa kale waliokuwepo wakati huo wanafananaje. Huenda pia kikawa kivutio cha utalii. Hata hivyo, kugeuza kurejeshwa kwa mabaki hayo kuwa sharti la kushiriki Sensa ni jambo ambalo mantiki yake siielewi. Watu wakisusia Sensa kwa sababu hiyo itakuwa siyo tu haieleweki wala haielezeki, bali hata watu wengine nchini na duniani watawashangaa. Lakini, jambo ambalo ningependa wajiulize ni kuwa hivi hasa wanamsusia nani? Mjerumani au wanajisusia wenyewe? Hivi kweli mtu uko tayari kuacha manufaa yako ya maendeleo yapotee au yaathirike kwa sababu ya mjusi ambaye hata akirejeshwa huna manufaa ya moja kwa moja? Hasara anapata nani sisi au wao? Nawasihi, Watanzania wenzangu, tusiwasikilize watu wanaoeneza maneno yahusuyo Mjusi au mambo mengine ya upotoshaji na uvurugaji wa mambo yenye maslahi makubwa zaidi kwetu binafsi na nchi yetu. Tuachane nao hawatutakii mema na wala hawaitakii mema nchi yetu. Nawaomba tusitumie vibaya uhuru wa kutoa maoni.

Ndugu Wananchi;

Wapo ndugu zetu wengine wanaotaka liongezwe swali la dini ya mtu katika orodha ya maswali yatakayoulizwa katika Sensa ya mwaka huu. Wahusika wakuu hasa ni baadhi ya viongozi na wanaharakati wa Kiislamu. Wao wanasema bila ya swali hilo kuwepo, Waislamu wasikubali kuhesabiwa. Wamekuwa wanafanya juhudi kubwa ya kuwashawishi Waislamu wawaunge mkono katika msimamo wao huo. Nimesoma baadhi ya nyaraka na vipeperushi vyao kuhusu madai hayo. Nilipata pia bahati ya kukutana na kuzungumza na baadhi ya wanaharakati na viongozi wa harakati hizo. Nia yangu katika kufanya hayo ilikuwa ni kutaka kuelewa kwa undani hoja na madai yao. Yako mambo kadhaa yanayotajwa kama sababu, lakini ukweli ni kwamba jambo linaloweza kuhusishwa moja kwa moja na Sensa, ni lile la takwimu za idadi ya Waislamu, Wakristo na Wapagani zilizotolewa na Baraza la Maaskofu Katoliki, Shirika la Utalii na Shirika la Utangazaji Tanzania.

Hawazikubali taarifa hizo kwa hoja kwamba, Waislamu hawajawahi kuhesabiwa na watoaji wa takwimu hizo. Kwa sababu hiyo hawaelewi ni kwa vipi watoe idadi ya kuwa ni asilimia fulani Watanzania. Hawana ugomvi nao kuhusu takwimu za Wakristo na Wapagani kwani huenda waliwahesabu. Kwa maoni yao, taarifa hizo si za kweli na ni upotoshaji unaofanywa maksudi kwa sababu wanazozijua watoaji wa taarifa hizo. Ili kuondoa upotoshaji huo, wanaharakati na viongozi hao wa Waislamu wakataka swali la dini liwepo katika Sensa hii ili ukweli ujulikane.

Katika mazungumzo yangu na baadhi ya viongozi wa Waislamu niliwaambia kuwa naelewa sababu na hoja za wao kukasirishwa na kutokuzikubali takwimu hizo. Vile vile, niliwaeleza kuwa takwimu hizo si za Serikali bali ni za mashirika hayo. Nilisisitiza kuwa takwimu za Serikali kuhusu idadi ya watu hutolewa na Ofisi Kuu ya Takwimu na si chombo kingine chochote cha Serikali. Bahati nzuri Ofisi Kuu ya Takwimu haijatoa takwimu hizo na wala siyo chanzo cha takwimu zilizotolewa na mashirika hayo. Walikozipata wanajua wenyewe. Taarifa hizo hazina ithibati yo yote na ndiyo maana zinatofautiana. Niliwasihi waachane nazo, wazipuuze na wakipenda watoe tamko la kuzikataa.

Ndugu Wananchi;

Niliwaambia pia kuwa kuelekeza lawama kwa Serikali kwa ajili ya taarifa hizo ni kuionea na kutoitendea haki. Vile vile kuibebesha dhima ya kuongeza swali la dini ili kuyajibu mashirika hayo ni kuipa mzigo usiostahili. Napenda, kutumia nafasi hii kuwasihi wale wote wanaotoa takwimu za namna hiyo kutambua unyeti wake na kuepuka kufanya hivyo. Zinatuletea mifarakano isiyokuwa ya lazima kama ilivyo sasa.

Ndugu Wananchi;

Kwa upande wetu, yaani Serikali, imekuwa vigumu kukubali maombi ya kuliingiza swali la dini katika Sensa hii kwa sababu za kisera na kiutekelezaji. Wakati wa ukoloni maswali ya rangi, dini na kabila la mtu yaliulizwa katika Sensa. Baada ya uhuru, maswali hayo yaliulizwa katika Sensa ya kwanza ya mwaka 1967 kwa vile ilikuwa bado inafuata misingi ya kikoloni. Baada ya hapo ulifanyika uamuzi wa kisera wa kutokuuliza maswali hayo kwani nia ya wakoloni kuuliza maswali yale ilikuwa ni kwa sababu ya sera yao ya wagawe uwatawale. Walitoa huduma kwa ubaguzi, sera ambayo Serikali zetu ziliachana nayo baada ya Uhuru na Mapinduzi. Huduma hazikuwa zinatolewa kwa ubaguzi wa rangi, kabila wala dini, bali kwa msingi wa haki ya uraia na ubinadamu wake.

Ndugu Wananchi;

Sera hiyo pia ilikuwa na lengo la kudumisha umoja na mshikamano wa taifa letu na watu wake. Badala ya watu kubishana juu ya watu wa dini ipi ni wengi na hivyo kufarakana kwa kutokubaliana na takwimu zilizotolewa, sera mpya inawataka watu wajivunie uwingi wao kama Watanzania.

Ndugu Wananchi;

Nionavyo mimi Sera hii ni nzuri na kwamba ulikuwa ni uamuzi wa busara na hekima kubwa. Tuendelee kuidumisha na kuienzi. Kufanya vinginevyo, na hasa kuingiza sera ya kutoa huduma kwa misingi ya dini zetu ni kuliingiza taifa letu ambalo lina sifa ya amani, upendo na utulivu, katika migogoro isiyokuwa ya lazima. Ni migogoro inayoweza kuepukika kwa kuenzi na kudumisha sera yetu hii nzuri na sahihi.

Ndugu Wananchi;

Sababu ya pili inayotupa ugumu kiserikali ni ya kiutekelezaji. Imechukua miaka kadhaa ya maandalizi mpaka kufikia hatua hii ya sasa ya kuwa tayari kutekeleza zoezi la Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012. Isitoshe Sensa ya majaribio imeshafanyika kwa kutumia vifaa, madodoso na maswali yaliyopo na marekebisho kufanywa baada ya hapo. Kuingiza mambo au jambo jipya sasa itakuwa viguku kiutekelezaji. Kutachelewesha zoezi zima na kusababisha hasara kubwa kwa taifa.

Kwa vile watu wote hawataulizwa swali la dini na kwa kuwa dini si kigezo cha kutoa huduma kwa wananchi, hakuna ulazima wa kusisitiza swali hilo liwepo. Napenda kuwasihi ndugu zangu wanaokereketwa na jambo hili waache kuling’ang’ania na badala yake wajitokeze kuhesabiwa. Tujitokeze kuhesabiwa ili na Waislamu nao wawemo katika idadi ya wananchi wa Tanzania.

Ndugu Wananchi;

Sioni ulazima wa kuunda Tume Huru ya Sensa yenye uwakilishi sawa wa Wakristo na Waislamu. Tangu mwaka 1931 kazi ya Sensa imekuwa inafanywa na Ofisi Kuu ya Takwimu nchini na ndipo ujuzi na maarifa yote yapo. Hata ukiamua uiite Tume bado utawatumia watu hao hao, hivyo mabadiliko hayo hayana sababu. Vile vile, sioni haja ya kuwa na mgao wa wafanyakazi wake kwa msingi wa dini kwa sababu Sensa siyo kwa ajili ya kujua Wakristo na Waislamu. Huduma hazitolewi kwa misingi ya dini za watu.

Ndugu Wananchi;

Katika maelezo yao kwangu, hivi karibuni Kamishna wa Sensa, Hajat Amina Mrisho Said na Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Muungano, Mama Albina Chuwa walinieleza kwamba kwa kawaida katikati ya Sensa moja na nyingine, hufanyika utafiti wa kidemografia, yaani Demographic Survey. Huu ni utafiti wa kina unaofanywa katika ngazi ya kaya ambapo taarifa za mambo mengi yahusuyo watu ambazo hazikusanywi, katika Sensa hukusanywa. Mara ya mwisho utafiti huo kufanyika ilikuwa mwaka 1973, yaani baada ya Sensa ya mwaka 1967 na kabla ya ile ya mwaka 1978. Ni makusudio ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu kuanzisha tena utaratibu huo mwaka 2016 ambapo baadhi ya masuala yaliyoachwa yanaweza kujumuishwa. Subira yavuta heri.

Ndugu Wananchi;

Nimehakikishiwa na mamlaka zinazohusika kuwa maandalizi ya sensa yamefikia hatua nzuri na zoezi liko tayari kuanza siku ya Jumapili, tarehe 26 Agosti, 2012. Lakini, mafanikio ya zoezi lenyewe yatategemea sana ushiriki wa watu ambao ndiyo walengwa na wadau wengine. Naomba nitumie fursa hii kuwataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya na Wenyeviti na Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri za Wilaya na Miji na wadau wengine wa kisiasa na kiutendaji wa ngazi mbalimbali waendelee kusimamia utekelezaji wa shughuli zote za Sensa katika maeneo yao ya uongozi. Hawana budi kuhakikisha kuwa zoezi linakuwa na mafanikio makubwa. Wale wote wanaofanya vitendo vya kuvuruga zoezi hili wachukuliwe hatua stahiki za kisheria.

Nawaomba viongozi wa kisiasa na kijamii nao waendelee kuwahamasisha na kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kujitokeza kuhesabiwa na kushirikiana na Makarani wa Sensa watakapokuwa wanafanya kazi yao. Wakumbusheni kukataa kuwasikiliza au kuwafuata watu wanaowashawishi wasijitokeze kuhesabiwa. Watu hao si wema wao na wala hawaitakii mema nchi yetu.

Ndugu wananchi;

Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitawapongeza Hajat Amina Mrisho Said, Kamishna wa Sensa wa Tanzania Bara na Ndugu Mwalim Ameir, Kamisaa wa Sensa Zanzibar kwa kazi kubwa na nzuri wanayoendelea kuifanya ya kutoa uongozi wa kisiasa, kusimamia na kuratibu zoezi la Sensa nchini. Nawapongeza pia Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu na Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na watendaji wengine wa Sensa katika ngazi mbalimbali katika Mikoa, Wilaya, Majimbo, Tarafa, Kata, Mitaa, Vijiji na Shehia kwa kazi nzuri ya matayarisho na uendeshaji wa Sensa ya mwaka 2012. Nawatakia mafanikio mema katika kazi hii muhimu na adhimu kwa nchi yetu na watu wake.

Ndugu zangu, Watanzania wenzangu, nawaomba sote tuwaunge mkono ndugu zetu hawa kwa kushiriki katika zoezi la Sensa kuanzia siku ya Jumapili tarehe 26 Agosti, 2012. Haya shime sote tujitokeze kuhesabiwa kwani kujitokeza kwetu ndiyo ukamilifu na mafanikio ya Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012. Ewe Mtanzania mwenzangu shiriki Sensa kwa maendeleo yako na ya taifa letu.

Mungu Ibariki Tanzania!

Mungu Ibariki Afrika!

Asanteni kwa kunisikiliza

RAIS KIKWETE AZINDUA AWAMU YA TATU YA MFUKO WA MAENDELEO YA JAMII (TASAF III) KATIKA UWANJA WA JAMHURI,MJINI DODOMA LEO

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizindua awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia mamia ya wananchi wakati akizindua awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akilekea kukagua mabanda ya maonesho wakati wa uzinduzi wa awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo Agosti 15, 2012. pamoja naye ni Spika wa Bunge Mhe Anne Makinda na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Iddi na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uratibu na Mahusiano), Mhe Steven Wassira.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikagua mabanda ya maonesho wakati wa uzinduzi wa awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo. pamoja naye ni Spika wa Bunge Mhe Anne Makinda na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Iddi
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipata maelezo toka kwa Mkurugenzi Mkuu wa TASAF Bw. Ladislaus Mwamanga wakati akikagua mabanda ya maonesho wakati wa uzinduzi wa awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo Agosti 15, 2012. pamoja naye ni Spika wa Bunge Mhe Anne Makinda na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif IddI.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi tuzo aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa TASAF Dr Servacius Likwelile wakati wa uzinduzi wa awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Iddi kitabu cha uzinduzi wa awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) katika Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo Agosti 15, 2012. pamoja naye ni Spika wa Bunge Mhe Anne Makinda.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue kwa niaba ya Rais wa Awamu ya Tatu Mhe Benjamin William Mkapa wakati wa uzinduzi wa awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) katika Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo Agosti 15, 2012. Pamoja naye ni Spika wa Bunge Mhe Anne Makinda na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Iddi.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizindua kitabu cha awamu ya tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) katika Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo Agosti 15, 2012.

*****************  *****************  ***************

HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE AKIZINDUA AWAMU YA TATU YA MFUKO WA MAENDELEO YA JAMII (TASAF III) UWANJA WA JAMHURI, DODOMA, 15 AGOSTI 2012


Mhe. Spika;
Mhe. Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar;
Mhe. Steven Wassira, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – Uratibu na Mahusiano,;
Waheshimiwa Mawaziri;
Mhe. Daktari Rehema Nchimbi, Mheshimiwa Steven Wassira (Mb);
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;,
Mheshimiwa Dr. Rehema Nchimbi;
Waheshimiwa Mawaziri na Wabunge;
Mhe. Katibu Mkuu Kiongozi;
Mwakilishi wa Benki ya Dunia: Tanzania, Uganda na Burundi,
Bwana Philippe Dongier;
Ndugu Peniel Lyimo, Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Uongozi wa TASAF;
Mwakilishi wa Benki ya Dunia;
Wawakilishi wa Ndugu Peniel Lyimo;
wWashirika wetu wangine wa mMaendeleo; ,
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa;
Waheshimiwa Wabunge
Viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa nawa Serikali;
Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF;
Wageni wWaalikwa;
Mabibi na Mabwana:;:

Shukrani
Ndugu Wananchi:
Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Steven Wassira na Nndugu Ladislaus Mwamanga, Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) na Kamati yake kwa kunialika nije kushiriki nanyi kwenye uzinduzi wa Awamu ya Tatu ya TASAF.Tarehe 30 Machi 2000 tulizindua Awamu ya Kwanza ya Mfuko wa Kwa kuwa huko tulipotoka tumepata mafanikio ya kutia moyo, naomba nianze kwa kutoa pongezi na kuwashukuru wote walioshiriki kufanikisha utekelezaji wa awamu mbili za TASAF zilizotangulia. 
Pongezi
Ndugu Wananchi;
Napenda kuishukuru kwa dhati Benki ya Dunia na Mwakilishi Mkazi wa Benki hiyo wa wao hapa nchini kwa kushirikiana na sisi kutekeleza miradi mbalimbali ya TASAF tangu mwaka 2000. Siku zote Benki ya Dunia imekuwa mwenzetu muhimu na wa kutumainiwa na hii inasikiliza hoja zetu na kuzingatia vipaumbele vya sSerikali na wananchi wa Tanzania yetu katika jitihada zetu za kupambana na umaskini na kujiletea maendeleo. Tunafurahishwa sana na sera ya kusikiliza vipaumbele vyetu.
 Jambo hilo Hali hii ndiylo limetuwezesha sisi kushirikiana nao kubuni mpango huu wa TASAF unaofadhiliwa na ubia mzuri wa maendeleo kati yetu Serikali na Benki ya Dunia, , kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo, Serikali zetu mbili na wananchi wa nchi yetu. 
Natoa ipongezai nyingi kwa sana Kamati ya Taifa ya Uongozi ya TASAF, chini ya uenyekiti imara wa Ndugu Peniel Lyimo, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa uongozi wake thabiti wa kusimamia vizuri shughuli za TASAF. Aidha, nampongeza Katibu Mkuu, Afisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa usimamizi wake thabiti. Hali kadhalika nNawapongeza pia viongozi na watendaji katika Halmashauri zote za Tanzania Bara , Afisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kazi nzuri waifanyayo ya usimamizi na utekelezaji wa miradi katika awamu iliyotangulia.
 Bila uongozi wao thabiti, mafanikio ya Awamu zya Kwanza na Pili yangekuwa ni ndoto. Kwa namna ya pekee nawapongeza wananchi wote walioitikia wito na kuchangia kwa hali na mali kufanikisha utekelezaji wa mpango huo wa kujiletea maendeleo yao wenyewe.
Nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipoipongeza Kamati ya Dkt. Servacius Likwelile, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, kwa kazi nzuri ya kuandaa Awamu ya Tatu ya TASAF. Kazi hiyo wameifanya vizuri na kwa umakini mkubwa wahuku akikishirikiana na Bibi Ida Manjolo na wataalamu wengine wa Benki ya Dunia. Tunawashukuru sana.
Mabibi na Mabwana;
Kuna msemo wa Kiswahili usemao “ukiona vyaelea, ujue vimeundwa”. Na hivi ndivyo ilivyo kwa TASAF. Siri ya mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa Awamu ya Pili ni usimamizi mzuri unaofanywa na Menejimenti ya TASAF. Hivyo napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Menejimenti, Mkurugenzi Mtendaji, na wafanyakazi wote wa TASAF kwa kusimamia vizuri shughuli na miradi mbalimbali iliyotekelezwa katika Awamu ya Pili. Ni matumaini yangu kuwa mtafanya vizuri maradufu katika Awamu ya Tatu tunayoizindua leo.
Utekelezaji wa Awamu ya Pili ya TASAF
Ndugu Wananchi;
Utekelezaji wa Awamu ya Pili ya TASAF ulikuwa na mafanikio makubwa. Jumla ya miradi 11,572 imetekelezwa na kati ya hiyo, miradi 4,294 ilikuwa ya huduma za jamii; miradi 1,405 ya ujenzi na miradi 5,875 ya makundi maalum. Miradi hiyo imegharimiwa na serikali kwa kushirikiana na washirika wake wa maendeleo.
 Serikali imetoa Shillingi bilioni 32.2 na Benki ya Dunia ilitupatia mkopo wa masharti nafuu wa Shilingi bilioni 322. Washirika wetu wengine walituongezea nguvu kwa kuchangia Shillingi bilioni 72. Aidha, wananchi wametoa fedha, rasilimali na nguvu kazi ambazo thamani yake inakadiriwa kuwakwa ujumla ni zaidi ya Shilingi billioni 20.2.

Miradi ya Huduma
Miradi ya Huduma za Jamii imeongeza na/au kuboresha madarasa 5,485; ofisi za walimu 150; nyumba za walimu 152;, maabara kwenye shule za sekondari 157; majengo ya utawala katika shule za sekondari 20; mabweni ya wanafunzi 163; vyoo vya wanafunzi 705; madawati 22,946, viti 5,483, meza 4,354; vituo vya afya 63; zahanati 606, nyumba za watumishi wa zahanati 301, vyoo kwenye zahanati 339, vichomea taka 182; vituo vya maji 2,198, visima virefu 192, visima vifupi 335 na matanki ya maji 205.
Miradi ya Ujenzi
Miradi ya ujenzi, yenyewe imeongeza au kuboresha barabara za vijijini 825; mabwawa madogo 78; mifumo midogo ya umwagiliaji 289; mifumo ya kuondoa maji ya mvua barabarani mita 4,593; maghala ya kuhifadhia nafaka 113; masoko 80; makaravati 901; madaraja ya watembea kwa miguu 64; na, miradi ya mazingira 608 yenye walengwa 566,938.
Makundi Maalum
Na miradi ya makundi maalum imetoa huduma kwa yatima 32,113; wajane 15,205; wazee 17,961; watu wenye ulemavu 7,840; watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI 52,316; na vijana wasio na ajira 36,859. Vilevile, watu 2,083 wamehamasishwa kujikinga na ugonjwa wa UKIMWI.
Mabibi na Mabwana;
Mafanikio ya utekelezaji wa Awamu ya Pili ya TASAF hayakuishia hapo. Vikundi 1,778 vyenye wanachama 22,712 vimeundwa kupitia Mpango wa Kuweka Akiba na Kuwekeza (COMSIP ) katika Halmashauri 44 zilizopo Tanzania Bara, Unguja na Pemba. Walengwa wote wamepatiwa mafunzo ya kuendesha vikundi vyao kwa ufanisi pamoja na vifaa. Vilevile, mafunzo ya usimamizi, utekelezaji bora wa miradi na fani mbalimbali katika ngazi ya vijiji, wilaya na taifa yametolewa kwa walengwa 27,373.
Serikali kupitia TASAF imefanikiwa pia kutekeleza Programu ya Kijamii ya Uhawilishaji Fedha kwa Kaya Maskini kwa majaribio katika Wilaya za Bagamoyo, Kibaha na Chamwino. Walengwa zaidi ya 13,000 kutoka kaya 6,000 maskini na zilizo katika mazingira hatarishi zilipatiwa ruzuku ya jumla ya shillingi bilioni moja na nusu. Kaya hizo zimejengewa uwezo na watoto sasa wanapelekwa kwenye zahanati na vituo vya afya kwa ajili ya chanjo na kufuatiliwa maendeleo yao. 
Aidha, watoto 1,638 ambao hawakuweza kwenda shule kwa sababu ya umasikini sasa wameandikishwa na wanakwenda shule. Kati ya wanafunzi hao, 392 wamefaulu kwenda shule za sekondari za kata. Vile vile wazee 4,956 wamewezeshwa kupata huduma za afya na baadhi yao wamejiunga na bima ya afya ili kupata huduma kwa urahisi na uhakika zaidi. Kufuatia mafanikio ya haraka ya programu hii, sasa maandalizi yanafanyika ili isambazwe kwenye Halmashauri zote katika utekelezaji wa Awamu ya Tatu ya TASAF.
Ndugu Wananchi;
Inafurahisha kuona jinsi suala la jinsia lilivyozingatiwa katika utekelezaji wa programu na miradi ya TASAF. Wanaume na wanawake walishirikishwa sawa sawa katika hatua zote za utekelezaji wa miradi yao. Idadi ya wanawake katika kamati ya mradi ilipangwa makusudi ili isipungue asilimia 50 ya jumla ya wajumbe, na idadi ya walengwa wanawake katika miradi ya ujenzi nayo isipungue asilimia 50. 
Bahati nzuri akina mama waliokuwa wajumbe kwenye Kamati mbalimbali wameonesha uwezo mkubwa wa uongozi. Naomba ushirikishwaji huu uendelee kuimarishwa na akina mama wajitokeze kwa wingi kushiriki katika usimamizi wa miradi ya TASAF ya Awamu ya Tatu. 
Ni wazi kuwa siri ya mafanikio ya Awamu ya Pili ya TASAF ni ushiriki mzuri wa wananchi, utayari wao wa kumiliki maendeleo yao wenyewe na moyo wa kujituma kwao pamoja na uongozi na usimamizi mzuri wa miradi katika ngazi zote.
Changamoto Katika Utekelezaji wa Awamu ya Pili
Maendeleo ya Jamii (TASAF I) kule Mwanhuzi, Wilayani Meatu, Mkoa wa Shinyanga.

Vile vile tarehe 23 Mei 2005, tulizindua Awamu ya Pili ya Mfuko huu (TASAF II ) kule Wilayani Magu, Mkoa wa Mwanza.

Leo hii ninayo furaha kubwa kuja hapa Dodoma kuzindua Awamu ya Tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III).

Tunazindua Awamu ya Tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii kwa kuwa Awamu ya Kwanza na ya Pili zimetekelezwa kwa mafanikio makubwa. Hivyo basi, naanza kwa kutoa shukurani na pongezi zangu za dhati kwa wote walioshiriki kufanikisha Awamu mbili zilizotangulia na walioshiriki kuandaa Awamu hii ya Tatu.

Naishukuru Benki ya Dunia na ninamshukuru Mkurugenzi Mwakilishi wa Benki hii kwa nchi za Tanzania, Uganda na Burundi, Bw. Philippe Dongier. Kwa hakika Bw. Dongier anaiwakilisha vyema Benki ya Dunia ambayo siku zote inasikiliza hoja na kuzingatia vipaumbele vya vita dhidi ya umaskini vinavyowekwa na Serikali yetu. Mfano halisi ni Mfuko huu wa Maendeleo ya Jamii – TASAF. Kwa usikivu huo, tumebuni ubia mzuri wa maendeleo kati ya Serikali yetu, Benki ya Dunia, Wadau wengine wa Maendeleo na Wananchi.

Napenda pia, kuwashukuru washirika wengine wa maendeleo ambao wanashiriki Awamu hii ya Tatu ya TASAF hususan Serikali ya Uingereza kupitia Idara yake ya Maendeleo ya Kimataifa (DFID), Serikali ya Hispania na Serikali ya Watu wa Marekani kupitia Shirika lake la Maendeleo ya Kimataifa (USAID).

Ninawashukuru Wataalam wa Benki ya Dunia na Washirika wengine wa Maendeleo wakiongozwa na Bibi Ida Manjolo ambao walishirikiana nasi kwa karibu katika utekelezaji wa Awamu ya Pili ya TASAF na kuandaa Awamu ya Tatu.

Naipongeza pia Kamati ya Taifa ya Uongozi ya TASAF ambayo mwenyekiti wake ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Ndugu Peniel M. Lyimo, pamoja na Kamati ya Maandalizi ya Awamu ya Tatu ya TASAF iliyoongozwa na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Dkt. Servacius B. Likwelile, kwa kazi nzuri.

Nawapongeza Viongozi na Watendaji katika Halmashauri zote za Tanzania Bara, Afisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar na wananchi wote kwa jumla kwa usimamizi na utekelezaji wa miradi ya jamii katika awamu zote mbili zilizotangulia. Wananchi wote waliitikia kwa moyo mkunjufu na ari kubwa kupokea mawazo ya Serikali katika utekelezaji wa mpango huo wa kujiletea maendeleo yao wenyewe.

Naipongeza pia Menejimenti ya TASAF, ikiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Ndugu Ladislaus J. Mwamanga na wasaidizi wake. Nina imani kuwa wataendelea kufanya kazi nzuri katika Awamu hii ya Tatu.

Tangu mwaka 2000 TASAF imekuwa ni kichocheo katika jitihada za wananchi kujiletea maendeleo. TASAF haina miradi; miradi ni ya wananchi. Inachokifanya TASAF ni kuwawezesha tu wananchi kutekeleza vipaumbele vyao vya maendeleo. 
Awamu ya Pili ya TASAF iligharimiwa kwa kiasi kikubwa na mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia. Mkopo huo ni kiasi cha Shilingi 322 bilioni sawa na Dola za Kimarekani 215 milioni. Vilevile kwa utekelezaji mzuri wa TASAF, kumekuwa na Wahisani na Miradi mingine kupitishia fedha TASAF zenye jumla ya shilling 72 bilioni sawa na Dola za Kimarekani 45 milioni. Mchango wa Serikali yetu ulikuwa ni Shilingi 32.2 bilioni, na wananchi walichangia fedha rasilimali na nguvu kazi ambazo thamani yake ilifikia zaidi ya Shilingi 20.2 bilioni.

Ndugu Wananchi
Ushiriki wa wananchi, utayari wao wa kumiliki maendeleo yao na kujituma kwao pamoja na uongozi na usimamizi mzuri wa kitaifa na halmashauri husika ndio msingi wa mafanikio ya Awamu ya Pili ya TASAF.

Mafanikio hayo ni pamoja na :-
1.Jumla ya miradi 11,572 ilipitishwa na kupewa fedha; miradi 4,294 ikiwa ya Huduma za Jamii, miradi 1,405 ya Ujenzi na miradi 5,875 ni ya Makundi Maalum.

2.Miradi ya Huduma za Jamii imeongeza na/au kuboresha madarasa 5,485, ofisi za walimu 150, nyumba za walimu 152, maabara kwenye shule za sekondari 157, majengo ya utawala katika shule za sekondari 209, mabweni ya wanafunzi 163, vyoo vya wanafunzi 705, madawati 22,946, viti 5,483, meza 4,354; zahanati 606, vituo vya afya 63, nyumba za watumishi wa zahanati 301, vyoo kwenye zahanati 339, vichomea taka 182; vituo vya maji 2,198, visima virefu 192, visima vifupi 335 na matanki ya maji 205.

3.Miradi ya ujenzi imeongeza au kuboresha barabara za vijijini 825, mabwawa madogo 78, na mifumo ya kuondoa maji ya mvua barabarani mita 4,593, maghala ya kuhifadhia nafaka 113, masoko 80, mifumo midogo ya umwagiliaji 289, makaravati 901, miradi ya mazingira 608 yenye walengwa 566,938 na madaraja ya watembea kwa miguu 64.

4.Miradi ya makundi maalum imetoa huduma kwa yatima 32,113, wajane 15,205, wazee 17,961, watu wenye ulemavu 7,840, watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI 52,316 na vijana wasio na ajira 36,859. Vilevile, uhamasishaji juu ya kudhibiti UKIMWI umetolewa kwa watu 2,083.

5.Vikundi 1,778 vyenye wanachama 22,712 vimeundwa kupitia Mpango wa Kuweka Akiba na Kuwekeza (COMSIP ) katika Halmashauri 44 na Unguja na PembaWalengwa wote wamepatiwa mafunzo ya kuendesha vikundi vyao kwa ufanisi pamoja na vifaa.

6.Mafunzo ya usimamizi, utekelezaji bora wa miradi na fani mbalimbali katika ngazi ya vijiji, wilaya na taifa yametolewa kwa walengwa mbalimbali 27,373.

Ndugu wananchi,
7.Serikali pia kupitia Awamu ya Pili ya TASAF imefanikiwa kutekeleza Programu ya Kijamii ya Uhawilishaji Fedha kwa Kaya Maskini kwa majaribio katika Wilaya za Bagamoyo, Kibaha na Chamwino. Walengwa zaidi ya 13,000 kutoka kaya 6,000 maskini na zilizo katika mazingira hatarishi zilipatiwa ruzuku ya jumla ya shillingi bilioni moja na nusu (Sh. 1,500,000,000). Kaya hizo zimejengewa uwezo na watoto ambao ndiyo walengwa wanapelekwa kwenye zahanati na vituo vya afya kwa ajili ya chanjo na kufuatilia maendeleo yao.

8.Aidha, watoto 1,638 ambao hawakuweza kwenda shule sababu ya umasikini sasa wameandikishwa na wanakwenda shule. Kati ya wanafunzi hao 392 wamefaulu kwenda shule za sekondari za kata. Vile vile wazee 4,956 ambao ni walengwa wamewezeshwa kupata huduma za afya. Pia Kaya za walengwa zimejiunga na mpango wa bima ya afya ili kupata huduma kwa urahisi na uhakika zaidi.

9.Programu hii imekuwa na mchango mkubwa katika kuboresha hali ya maisha ya kaya za walengwa kwa muda mfupi sana. Mafanikio yake yamefanya sasa programu hii kusambazwa kwenye Halmashauri zote katika utekelezaji wa TASAF Awamu ya Tatu. Haya yote yasingewezekana bila ninyi wananchi kukubali kwa pamoja kushiriki katika kurekebisha hali ya uchumi wetu, kwa kuwa muhimili mkuuwa maendeleo katika ngazi ya jamii. 
Ndugu wananchi,
Kwa kuwa TASAF imepanua uwigo wa kuwafikia walengwa masikini katika makundi mbalimbali ndani ya Tanzania Bara na Zanzibar na uzoevu wao wa zaidi ya miaka kumi na mbili; ni dhahili kuwa ni chombo pekee cha serikali chenye uwezo wa kutekeleza vizuri Mpango wa Kitaifa wa Kinga ya Jamii ( National Social Protection Framework)

Awamu ya Pili ya TASAF imeimarisha uwajibikaji katika ngazi zote kwa kuhakikisha kuwa fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali zinatolewa taarifa na wadau wote wanajulishwa mapato na matumizi yake. Kamati za usimamizi wa miradi ziliwajibika kutoa taarifa za utekelezaji hatua kwa hatua na matumizi ya fedha.

Suala la jinsia katika utekelezaji wa miradi lilizingatiwa, na kuonekana wazi kuwa ni jambo la haki na la manufaa kila palipokuwa na mradi unaochangiwa na TASAF. Wanaume na wanawake walishirikishwa sawa sawa katika hatua zote za utekelezaji wa miradi yao. 
Idadi ya wanawake katika kamati ya mradi ilipangwa kwa makusudi isipungue asilimia 50 ya jumla ya wajumbe, na idadi ya walengwa wanawake katika miradi ya ujenzi nayo isipungue asilimia 50. Lengo ni kuhakikisha kuwa kipato kisichopungua asilimia 50 kinaelekezwa kwa walengwa ambao ni wanawake. Matumaini yangu ni kuwa uwezo waliouonyesha wanawake waliokuwa kwenye kamati hizi utawasukuma wengi wao kuomba uongozi katika ngazi mbalimbali.



Ndugu wananchi;
Pamoja na mafanikio hayo ya kutia moyo, Wakati wa utekelezaji wa Awamu ya Pili ulikabiliwa na changamoto ya TASAF kumekuwepo na changamoto mbalilmbali.
 Changamoto hizo ni pamoja na uhaba wa fedha kutokutosheleza kukidhi wezo wa Mfuko kutokidhi mmahitaji ya wananchi; uwezo mdogo wa kusimamia miradi katika ngazi mbalimbali za uongozi; na ya wananchi ambayo ni mengi, ukosefu wa huduma kwenye baadhi ya vituo vya kutolea huduma kama zahuhaba wa watumishi katika vituo vya kutoa huduma. Bahati nzuri serikali na uongozi wa TASAF unazitambua changamoto hizo na tumejipanga vizuri kukabiliana nazo katika Awamu hii ya Tatu tunayoizindua leo.
Awamu ya Tatu ya TASAF
anati, vituo vya afya na masoko vilivyotokana na miradi kutokana na sababu mbalimbali kama vile uhaba wa watumishi.

Changamoto nyingine ni pamoja uhaba wa fedha za utekelezaji wa shughuli za kujenga uwezo, wigo mdogo wa utekelezaji wa jitihada nyingine, kama vile Mpango wa Jamii wa Uhawilishaji Fedha kwa Kaya Maskini, Mpango wa Jamii wa Kuweka Akiba na Kuwekeza, uansishwaji wa Taasisi za Maendeleo ya Jamii katika sehemu za mijini.

Kadhalika ilijitokeza changamoto ambapo baadhi ya wanasiasa walipotosha dhana ya kuanzishwa kwa TASAF na pia kutokuwepo mfumo wa uendelevu thabiti wa kutekeleza TASAF kwa kutegemea rasilimali za ndani.

Mabibi na Mabwana;Ndugu wananchi
Kufuatia mafanikio katika utekelezaji wa Awamu mbili zilizotangulia na pia katika kukabiliana na changamoto zake, Serikali imeamua kuanzisha Awamu ya Tatu ya TASAF itatekelezwa kwa miaka kumi, katika vipindi viwili vya miaka mitano mitano. ambapo Muondo wake umezingatia kupata ufumbuzi wa chanamoto zilizopatikana na hivyo ambayo itatekelezwa katika kipindi cha miaka kumi nchi nzima kwa Awamu mbili za miaka mitano mitano. 
Tunategemea
Awamu hii ya Tatu ya TASAF itatoa mchango mkubwa katika kufikia nalenga kuchangania kufikiwa malengo yetu yaliyomo kwenye ya D Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025, Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, Mkakati wa Pili wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA II) na Mkakati wa Pili wa Kukuza Uchumi Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Zanzibar (MKUZA II) na Mpango wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mita. Tutaweka mkazo zaidi katika miradi ya huduma za elimu, afya na maji nay a kuondoa umaskini wa kipato. no kwa kuwekeza katika kuendeleza rasilimali watu miongoni mwa kaya maskini na zilizo katika mazingira hatarishi.
 Kupitia utekelezaji wa Awamu ya Tatu ya TASAF tunatarajiainatarajiwa kuwa kaya nyingimaskini maskini zitapiga hatua na kutoka kwenyekuanza kutoka katika umaskini namaisha ya utegemezi. hatimaye kuwa na mchango katika kukuza uchumi na kuondokana na utegemezi.

Ili kutekeleza miradi ya Awamu ya Tatu ya TASAF, jumla ya Shilingi bilioni 408 zitahitajika. Fedha hizo zitatolewa na serikali yetu, Benki ya Dunia na washirika wengine wa maendeleo. Serikali itatoa Shillingi bilioni 45; Benki ya Dunia itachangia Shillingi bilioni 330; Hispania itatoa Shillingi bilioni 9; Uingereza Shillingi bilioni 24; na Marekani Shillingi bilioni 1.4. Kama ilivyokuwa kwa Awamu zilizotangulia, tunawategemea sana wananchi kutuunga mkono na kuchangia kwa hali na mali. Mafanikio ya Awamu hii yatategemea sana mchango wa wananchi katika maeneo husika.
Ahadi na Wito kwa Wananchi
Ndugu wananchi;
Tunapenda kuahidi kuwa tutaendelea kushirikiana na wananchi wote ambao wanaonesha dhamira ya dhati ya kupambana na umaskini na kujiongezea
Kwa ushirikiano wenu wananchi, TASAF imetekelezwa vizuri sana na matunda yake yapo wazi, na kwa vile mmeendelea kuiunga mkono Serikali yenu ya CCM katika kutekeleza Mwelekeo wa Sera zake za Miaka mitano (2010-2015) zinazohimiza mageuzi ya kiuchumi na uwezeshaji wananchi, serikali imetenga fedha tena na kupata mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia na washirika wengine wa maendeleo ili kutekeleza Awamu ya Tatu ya TASAF.

Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya Dunia iliridhia na kupitisha utekelezaji wa Awamu ya Tatu ya TASAF tarehe 29 Machi, 2012. Mkataba kati ya Benki ya Dunia na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ulisainiwa tarehe 15 Juni 2012. Na idhini ya kuanza kutumia fedha hizo tayari imeshatolewa.

Awamu ya Tatu ya TASAF inatarajiwa kugharimu Shilingi 408 Bilioni sawa na Dola za Kimarekani 272 Milioni kwa mchanganuo ufuatao:

1.Benki ya Dunia itachangia shilingi 330 bilioni (USD 220 milioni),
2.Serikali ya Hispania itachangia Shilingi 9 bilioni (USD 6 milioni)
3.Serikali ya Uingereza kwa kupitia Idara ya Serikali ya Uingereza ya Maendeleo ya Kimataifa(DFID) itachangia Shilingi 24 bilioni (USD 16 milioni)
4.Serikali ya Watu wa Marekani kupitia Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) itachangia Shillingi 1.44 bilioni ( USD 900,000)
5.Serikali ya Tanzania itachangia sh.45 bilioni (USD 30 milioni)

Ndugu wananchi
Utekelezaji wa Awamu ya Tatu ya TASAF unategemewa kuwa na changamoto zifuatazo:

1.Upatikanaji wa raslimali fedha za kukidhi mahitaji halisi ya walengwa. Jitihada za kupata rasilimali zaidi ziendelee na Wadau wa Maendeleo watoe ushirikiano zaidi hasa wale ambao wameonyesha nia ya kushiriki katika kuchangia mfuko huu.
2.Kujenga uwezo mapema wa kusimamia na kutekeleza kwa wakati uhawilishaji wa fedha kwa walengwa. Mpango wa kujenga uwezo wa watekelezaji katika ngazi mbalimbali upewe kipaumbele. Ufuatiliaji na tathmini vifanyike ili kubaini mapungufu mapema iwezekanavyo.
3.Uwezo wa kusimamia utekelezaji miradi kwa ufanisi na kwa wakati. Ngazi zote zinazohusika na utekelezaji zishiriki kikamilifu katika kuhakikisha usimamizi wa utekelezaji unafanyika ipasavyo. Aidha, utekelezaji ufanyike kwa awamu kuzingatia uwezo unavyojengwa.
4.Kusimamia uendelevu wa rasilimali na vituo vya kutolea huduma vilivyotokana na miradi iliyotekelezwa na wananchi. Wataalamu kutoka halmashauri husika na Viongozi katika maeneo ya utekelezaji wawezesha jamii kuwa na mipango endelevu ya uendeshaji.

5.Usimamizi wa fedha zitakazotolewa kutekeleza miradi inayochangiwa na TASAF utahitaji uwepo wa udhibiti mkubwa katika ngazi zote. Kazi hiyo nayo ifanywe kuanzia sasa na kwa kipindi chote cha utekelezaji.

Ndugu wananchi,
Leo tunapozindua Awamu ya Tatu ya TASAF napenda tujikumbushe kuwa historia yetu ya vita dhidi ya umaskini imetufundisha mambo kadhaa:

Kwanza, sera nzuri, mipango mizuri na nia njema peke yake havileti
maendeleo.

Pili, fedha za Serikali, mikopo au wahisani peke yake hazileti
maendeleo.

Tatu, ipo tofauti kubwa kati ya kutamani maendeleo na kuwa tayari
kutoka jasho kutafuta maendeleo.

Baada ya miaka 50 ya Uhuru sasa nadhani tumeelewa kunahitajika nini ili maendeleo yaje kwa kasi ya kutosha kuweza kupunguza na hatimaye kuondoa umaskini kabisa.

Hatua ya kwanza ya maendeleo ni mtu kutoridhika na hali duni ya maisha yake; ni kujenga tamaa na wivu wa maendeleo na kuchukia hali ya umaskini.

Hatua ya pili ni mtu kuamua kwa dhati kutafuta maendeleo kwa jasho
lake, na inapobidi kwa kushirikiana na wenzake wanaochukia umaskini kama yeye.

Hatua ya tatu ni mtu kupima uwezo alionao – uwezo wa fedha na wa mali nyingine; uwezo wa akili na maarifa; na uwezo wa nguvu za kufanya kazi na kubuni mbinu za kutumia ili kuboresha hali yake ya maisha na hali ya jamii yake kwa ujumla.

Hatua ya nne ni kutekeleza kwa kadri ya uwezo wake mbinu za maendeleo alizozibuni, au zilizobuniwa na jamii yake.

Hatua ya tano ni kuomba msaada kwa yale mambo yaliyo nje ya uwezo wake, ikiwemo msaada wa fedha, msaada wa vifaa, au msaada wa elimu na utaalamu.

Mfuko huu wa Kuongeza Uwezo wa Wananchi katika Maendeleo ni jitihada nyingine ya Serikali kuwasaidia wale wananchi ambao wamepitia hatua zote hizo za kutafuta maendeleo, yaani tayari wameonyesha chuki yao dhidi ya umaskini, wameamua kwa dhati kuondokana na umaskini kwa kuongeza kkipato chao. Kipato cha mtu kinapoongezeka watoto wake watahudhuria masomo na kupata huduma bora za afya. Wazee na akina mama nao watapata huduma bora za afya. 
Lakini kipato hakiwezi kuongezeka kama mtu hataki kufanya kazi, hataki maendeleo, na hataki kujishughulisha na kitu chochote. Maisha bora kwa kila mMtanzania yatapatikana kama tutafanya kazi kwa bidii na maarifa. Inawezekana, kila mtu atimize wajibu wake. 
kaya ili watoto wahudhurie masomo na kwenda kliniki kupata chanjo na huduma zingine za afya. Vile vile ongezeko la kipato litawezesha akina mama wajawazito na wazee kupata huduma zote muhimu za afya.

Hivyo ndugu zangu natoa wito kwa wananchi wote watumie vizuri fursa hii murua ya TASAF. Tushirikiane na uongozi wa TASAF kubuni miradi itakayotuletea maendeleo ya haraka, miradi itakayoboresha huduma za jamii. Tushirikiane nao kusimamia utekelezaji wa miradi hiyo. Tuhakikishe kuwa tunafuata maelekezo ya wataalam na viongozi wetu katika ngazi mbalimbali. 
Tuwafichue wabadhirifu wa fedha za miradi ya TASAF na wale wote wanaotumia vibaya rasilimali za miradi. Daima tukumbuke kuwa miradi hii ni kwa ajili yetu sisi pamoja na watoto wetu, ndugu zetu na jamaa zetu. Tukifanya hivi nina imani tutakuwa na msingi imara wa kujenga taifa linaloendelea na hatimaye kushinda vita dhidi ya adui watatu wa maendeleo: umaskini, njaa na magonjwa. 
Rai kwa Washirika wa Maendeleo na Viongozi wa TASAF
Mabibi na Mabwana;
Natumaini washirika wetu wa maendeleo wataendelea kuunga mkono juhudi zetu hizi za kuondoa maadui watatu wa maendeleo. Wamekuwa wakifanya hivyo tangu tulipoanzisha Mfuko huu wa TASAF na nina imani wataendelea. Msaada wao utasaidia sana kufikia malengo yetu tuliyojiwekea katika utekelezaji wa Awamu hii. 
Nawaomba pia viongozi wa TASAF, Kamati ya Taifa ya Uongozi, Menejimenti na Mkurugenzi Mtendaji waongeze ufanisi na maarifa katika utendaji wao. Waongeze usimamizi wa fedha na rasilimali, wajenge uwezo wa kusimamia utekelezaji wa miradi katika ngazi mbalimbali, na wabuni vyanzo vingine vya kupata fedha za kuendeleza miradi. Naamini wataweza.


Mwisho
Mheshimiwa Waziri;
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Kabla ya kumaliza hotuba yangu naomba nitoe shukrani za dhati kwa Mhe. Benjamin William Mkapa, Rais wa Awamu ya Tatu kwa kubuni wazo hili jema ambalo manufaa yake tunayaona. Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kufanya kazi iliyonileta hapa Nazindua Awamu ya Tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii kwa matumaini makubwa kuwawamba sasa Watanzania sasa tumeupata ufunguo wa maendeleo yetu sote. Napenda kutamka kwamba Awamu ya Tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii, (TASAF) umezinduliwa rasmi leo. Nawatakia kila la heri na mafanikio katika utekelezaji wake.

Asanteni sana kwa kunisikiliza.kwa kutumia fursa ambazo mageuzi ya uchumi, na usimamizi bora wa uchumi, umeweka mbele yetu.

Kwa pamoja tutafanya mengi. Na kwa mradi huu wa TASAF, ukichanganywa na miradi mingine, na utaratibu huu wa kushirikisha wananchi katika shughuli za kupunguza umasikini, ninaamini Watanzania wote tutakuwa na msingi imara wa kujenga taifa linaloendelea na hatimaye kushinda vita dhidi ya umaskini.

Na sasa natangaza kuwa nimezindua rasmi Awamu ya Tatu ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III).

Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.

RAIS KIKWETE AWAAPISHA WATENDAJI WAKUU WA MAHAKAMA LEO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. Jakaya Mrisho Kikwete akimuapisha Mhe.Hussein Kattanga kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama, kabla ya uteuzi wake,Mhe. Kattanga alikuwa Katibu Mkuu TAMISEMI.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akimuapisha, Mhe. Ignas Paul Kitusi kuwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, kabla ya uteuzi wake Mhe. Kitusi alikuwa Msajili wa Mahakama Kuu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akimuapisha Mhe. Panterine Kente kuwa Msajili wa Mahakama ya Rufani.

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Watendaji Wakuu wapya wa Mahakama ya Tanzania, mara baada ya kuwaapisha Ikulu jijini Dar es Salaam, kutoka kushoto ni Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Ombeni Sefue, Mhe. Hussein Kattanga, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Mhe. Ignas Paul Kitusi, Msajili Mkuu wa Mahakama na Mhe. Panterine Kente, Msajili wa Makahama ya Rufani.

KEYNOTE ADDRESS BY HIS EXCELLENCY JAKAYA MRISHO KIKWETE, PRESIDENT OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA, AT THE OFFICIAL OPENING OF A SPECIAL CABINET RETREAT ON TRANSFORMATION OF GOVERNMENT DELIVERY SYSTEMS, 4-5 AUGUST, 2012, DODOMA

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akifungua warsha kuhusu mfumo wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kwa mawaziri, makatibu wakuu na wakuu wa taasisi za serikali leo Agosti 4, 2012 katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akifungua warsha kuhusu mfumo wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kwa mawaziri, makatibu wakuu na wakuu wa taasisi za serikali leo Agosti 4, 2012 katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma.

  Waziri katika ofisi ya Waziri Mkuu wa Malaysia Mhe Idris Jala akitoa mada ya utangulizi katika  warsha kuhusu mfumo wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kwa mawaziri, makatibu wakuu na wakuu wa taasisi za serikali leo Agosti 4, 2012 katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma.

Washiriki wakimsikiliza Rais Jakaya Mrisho Kikwete wakati akifungua warsha kuhusu mfumo wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kwa mawaziri, makatibu wakuu na wakuu wa taasisi za serikali leo Agosti 4, 2012 katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma 

Washiriki wakimsikiliza Rais Jakaya Mrisho Kikwete wakati akifungua warsha kuhusu mfumo wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kwa mawaziri, makatibu wakuu na wakuu wa taasisi za serikali leo Agosti 4, 2012 katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma. 

Rais Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wakuu wa serikali pamoja na wawezeshaji kutoka Malaysia baada ya kufungua warsha kuhusu mfumo wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kwa mawaziri, makatibu wakuu na wakuu wa taasisi za serikali leo Agosti 4, 2012 katika ukumbi wa St Gaspar mjini Dodoma.

 Your Excellency Dr. Mohammed Gharib Bilal, Vice President of the United Republic of Tanzania;

Your Excellency Dr. Ali Mohammed Shein, President of Zanzibar and Chairman of the Revolutionary Council;

Honourable Mizengo Kayanza Peter Pinda, Prime Minister of the United Republic of Tanzania;

Honourable Anne Makinda, Speaker of the Parliament of the United Republic of Tanzania;

Honourable Dato’ Sri Idris Jala, Minister and Chief Executive Officer of the Performance Management and Delivery Unit (PEMANDU), Prime Minister’s Office, Government of Malaysia;

Honourable Ministers;

Ambassador Ombeni Sefue, Chief Secretary and Head of Public Service;

Dr. Abdulhamid Yahya Mzee, Chief Secretary, Zanzibar;

Permanent Secretaries;

Distinguished facilitators from PEMANDU;

Ladies and Gentlemen;

I am pleased to welcome you all to this unique seminar on Transformation of Government Delivery Systems. To you Dato’ Idris Jala and the entire team from Malaysia and the United States, I say welcome to Tanzania and welcome to Dodoma. In a very special way let me sincerely thank the government of Malaysia for allowing you and your colleagues to come and share with us the experience of Malaysia.  I also commend Dr. Philip Mpango, the Executive Secretary of the Planning Commission and his staff for organizing this important Seminar so well. To all my fellow participants may you realize that this is a rare opportunity for us so we must utilize well.

Ladies and Gentlemen;       

The idea of holding this Seminar was conceived in May 2011 during my participation at the Langkawi International Dialogue that took place in Kuala Lumpur, Malaysia. It was during that meeting the Malaysian government shared with Heads of State and Government attending the meeting, two of their development models. These were the Government Transformation Programme (GTP) and the Economic Transformation Programme (ETP). All of us were fascinated by these models and wanted to learn more about Malaysia’s experience, particularly its delivery systems.  The idea hidden behind the minds of all of us was the wish to learn more about these models and see how to emulate their good examples.

The government of Malaysia accepted our request and organized a special seminar in November 2011 on the Big Fast Results (BFR) approach. They invited senior officials from different countries of the Smart Partnership Movement to participate. We sent a delegation led by Dr. Phillip Mpango, the Executive Secretary of the Planning Commission, to attend the Seminar. Indeed, the delegation came back home excited and eager to see our government use the BFR methodology to help us perform better in the discharge of our responsible.

It is worth mentioning that the Prime Minister of Malaysia did a special favour to me when he agreed to allow Dato’ Idris Jala to give Tanzania  extra tuition after the general briefing to all Heads of State and Government.  It was during this private session that I requested Dato’ Idris Jala to come to Tanzania and conduct this seminar to my Cabinet and other senior government officials.  It is heartwarming, indeed, that we have him and his powerful team with us this morning.

On return from the November, 2011 seminar, Dr. Mpango and his team began preparations for this seminar.   They worked tirelessly with PEMANDU and Mckinsey to develop ideas and concretise the preparations of holding this seminar. This event today, therefore, is the outcome of the tremendous efforts of the Planning Commission of Tanzania and PEMANDU of Malaysia. Personally, I have been anxious to see this seminar is held because I thought what I learnt in Malaysia was worth sharing with the top echelons of my government. I believe learning the ABCs of Big Fast Results approach will interest all of us gathered here and inspire us to do better.

Excellencies;

Ladies and Gentlemen;

Many of you here may know that at our independence in 1961, the per capita income of Mainland Tanzania was about the same level as that of India and Pakistan. More interesting, our economic structure was generally similar to that of India, Pakistan and to some extent that of Malaysia. The economies of all the four countries were characterized by heavy dependency on agriculture. For example, in Tanzania the contribution of agriculture to GDP was 59 percent, Pakistan 45 percent, India 42 percent, and Malaysia 36 percent. The share of manufacturing sector in each of those four countries was less that 15 percent of GDP.

After 50 years, one can no longer compare Tanzania with those other three countries. They have just moved too many steps up the ladder of socio-economic transformation and development. While Tanzania remains undeveloped, heavily depending on agriculture with a low per capita income of US dollar 550, India, Pakistan and Malaysia have transformed their economies to remarkable levels. They have become highly industrialized and the share of agriculture has diminished significantly although it remains highly productive.  These countries are big exporter of food and manufactured goods.

With regard to Malaysia, her story is even more fascinating.  The country has been transformed incredibly from a commodity-based economy focusing on rubber and tin at independence in 1957 to one of the world’s largest producers of electronics and electrical products. They make cars and military hardware including sub-marines. Malaysia is now a high middle income, export-oriented economy with per capita income close to US dollar 10,000. Their target now is to become a developed country by 2020. Coming from such humble beginnings to what it is today gives us inspiration that we too can make it. That is why I felt learning their examples particularly about how they made it relevant to our country.

Ladies and Gentlemen;

Since 1961 Tanzania’s political leadership both on the mainland and Zanzibar have demonstrated strong political will to see their country develop fast. They identified poverty, disease and ignorance as the most critical challenges to the country’s development. Indeed, deliberate and focused efforts have been made in order to overcome   these challenges. Immediately after the independence the government launched the first development plan for 1961-1964 and later made a longer development plan of 15 years (1964-1980), divided into three equal implementation periods of five years.

Some of you will recall that the implementation of the first two phases were encouraging, but the third phase between 1975-1980 was heavily disrupted by various challenges of the time including drought, fuel crisis and disintegration of the East Africa Community. On top of that, the government was also forced to divert the resources from the development activities to protect the country’s territorial integrity during the Idd Amin invasion in 1978. Later in the mid 1980’s and early 1990’s, in response to the deteriorating economic situation, a major economic shift was made by introducing a market-oriented economy.

Ladies and Gentlemen;

Despite the many challenge encountered in our past planning initiatives, in 1994 the government started the preparations of another long term national development vision whose objective was to help lift millions of Tanzanians out of poverty. Subsequently it meant making   the country graduate into middle –income country by 2025.The work of preparing the new national development framework was completed in 1999 and the new blue print document that builds on the National Strategy for Growth and Poverty Reduction as well as sector specific programmes was launched.

As you will recall, in 2008 I established the Planning Commission. Among the major tasks I directed it to do was to undertake a comprehensive review of the Vision 2025 and develop structured systems of guiding its implementation. The Commission dutifully obliged.  They came up with both a Reviewed Vision 2025 and proposal for a long Terms Development Plan divided into three phases of five years each. In June, 2011 we launched the first of the three Five Years Development Plan covering the period 2011/12 – 2015/16. The main objective of this plan is to remove obstacles to growth and unleash Tanzania’s latent growth potentials.

Ladies and Gentlemen;

Our persistent efforts and commitment have enabled us to post modest progress, especially at the macro-economic level: macro-economic stability has been preserved; expenditure on social services has increased; exports and foreign currency reserves have increased; FDI flow has increased; inflation has been kept in check despite current challenges.  We have enjoyed relatively high economic growth rates over the past decade and a half. We have registered a modest increase of per capita income. However despite the encouraging progress we still have long ground to cover as poverty remained a major challenge. Many people still live below the poverty line.

In my view strengthening government delivery systems  d improving the performance of the private sector and the individual farmer and worker is the answer. We would be able to adequately translate our wishes inscribed on the many papers and documents into concrete results that would change lives of our people and our nation. Learning from examples of friends who not long ago were at our level could be useful. That is why we have invited our Malaysian friends to come and tell us their story of success and learn from their good examples.

Excellencies;

Ladies and Gentlemen;

This Seminar is intended to do that. I would like it to   be a turning point towards a journey where plans are effectively implemented. Where performance will be measured against clear and concrete deliverables. Let it be a journey of hope that will ensure the first five year development plan and indeed the long-term dream of Vision 2025 is realized in a timely manner. It is a journey of entrenching accountability that will see us move beyond planning and focus more on implementing what we have agreed to do in order to realize socio-economic transformation  and development of our country. A journey that we must all embark today and lead Tanzanians and their great country to momentous victory in the fight against underdevelopment,  hunger, poverty and deprivation.

Distinguished Participants;

This requires of us all to read all our major national development frameworks including the first five year development plan of 2011/ 12 – 2015/16 and the Vision 2025. We should fully understand the thrust and priorities contained in those frameworks. We must align policies and  our sectoral budgets to the objectives of the major national development frameworks.  There should be unity of purpose, because all of us are working towards a common goal. But all these efforts would be meaningless if our follow up mechanisms and delivery systems remain weak.

A strong delivery system is a key element to sustainable improvement and development.  A weak delivery system breeds a poor service delivery to the public and makes it difficult to break the poverty cycle.  In this regard, the time has come for Tanzania to formulate sound delivery frameworks and hold political leaders and top executives responsible for their failures. Perhaps this Seminar is a good starting point that will enable us to develop a forceful follow up mechanism. I therefore implore all of you here to be attentive throughout the Seminar and learn the new tested approaches of delivering high quality services to citizens and develop a nation from poor to  developed. Engage facilitators, seek clarification and also share your own experience and frustrations. There is a lot to learn and improve upon.

Excellencies;

Distinguished Guests;

Ladies and Gentlemen;

In conclusion, I want to thank once again the government of Malaysia for accepting our invitation and agreeing to send Honourable Jala and his team. I also thank the Planning Commission for excellent arrangements of the Seminar. We are now ready to listen, learn and be converted. I look forward to a successful Seminar.

Thank you for your kind attention.

  =============================

WELCOMING REMARKS BY AMBASSADOR OMBENI SEFUE, CHIEF SECRETARY OF THE GOVERNMENT OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA DURING THE WORKSHOP ON TRANSFORMATIONAL LEADERSHIP FOR EFFECTIVE AND EFFICIENT GOVERNMENT DELIVERY ON THE TANZANIA DEVELOPMENT VISION 2025

ST.GASPAR’S CONFERECE CENTRE, DODOMA

4-5 AUGUST, 2012

 

The Chief Secretary, Amb. Ombeni Sefue, delivers his speech
H.E. Excellency Dr. Jakaya Mrisho Kikwete, President of the United Republic of Tanzania;
H.E. Dr. Gharib Bilal, Vice-President of the United Republic of Tanzania;
Hon. Madam Anne Makinda, Speaker of the Parliament of the United Republic of Tanzania;
Rt. Hon. Mizengo Kayanza Peter Pinda, Prime Minister of the United Republic of Tanzania;
Hon. Dato’ Sri Idris Jala, Minister and CEO of the Performance Management and Delivery Unit (PEMANDU), Prime Minister’s Office, Government of Malaysia;
Honourable Ministers;
Hon. Dr. Abdulhamid Yahya Mzee, the Chief Secretary of Revolutionary Government of Zanzibar and Secretary of the Revolutionary Council;
Hon. Member of Parliaments;
Permanent Secretaries;
Distinguished Guests from PEMANDU and MCKinsey;
Ladies and Gentlemen,
        Good morning and welcome to this historic and important workshop on Transformational Leadership for Efficient and Effective Government Delivery on the Tanzania Development Vision 2025.
        I thank you all for coming, and I want to extend our special gratitude to you, Mr. President, for readily agreeing to spend two days out of your busy schedule, to chair and participate in this workshop – an indication of the priority that you personally attach to the need for the kind of transformation we are talking about. 
        I want to welcome and thank our very distinguished guest, The Honourable Dato’ Sri Idris Jala, Minister and CEO of the Performance Management and Delivery Unit (PEMANDU) of Malaysia who likewise graciously agreed to take time out of his very busy schedule to travel to Tanzania and talk to us about  their experience on transformational leadership to ensure “ Big Fast Results”.
        I also welcome and thank the team from PEMANDU and McKinsey who will also help us to figure out how the Malaysian model for achieving big and fast results can be adopted in Tanzania.
Mr. President;
        Almost eight years ago, we as a nation, in an inclusive and broadly participatory process, agreed on the kind of society we want for our country and our people come the year 2025.  We called it “Development Vision 2025”.
        But, as we all know, a vision is just that a vision, a dream, a wish. To turn vision into reality one needs an implementation plan, a strategy and a delivery system, one which is efficient and effective.
        The Fourth Phase Government under your able stewardship, Mr. President, has embarked upon the journey to transform Development Vision 2025 into reality.
        Under your leadership we now have in place the long-term  Perspective Plan up to 2015, we have three Five Year Development Plans; the first one focusing on removing obstacles to growth, the second one focusing on unleashing the growth potential of our country and the last one focusing on strengthening our external competitiveness.
        And, as you all know, the five year development plans are broken down into annual development plans.
        So, we now have in place an implementation plan for Vision 2025, we now have a strategy and this workshop is the beginning of a process to design an effective and efficient delivery system.
Your Excellency, Mr. President,
        Last year, you participated in the Langkawi Smart Partnership International Dialogue in Malaysia, where you and other African leaders were exposed to the “Big Fast Results” approach that Malaysia designed to accelerate delivery on its development plans, with outstanding and most impressive results.
        You expressed then a wish to see us in Tanzania adopting a similar system, tailored to our specific situation, which will introduce the elements of speed, results and impact in the implementation of Development Vision 2025.
        I want to thank and commend Dr. Phillip Mpango, Executive Secretary of the Planning Commission and his team and the Malaysian government, for agreeing to the president’s request that they share with us their experience in accelerating implementation of their national agenda, focusing on time-bound results.  I thank resource persons and facilitators, including the McKinsey Team and our own Prof. Joseph Semboja, and everyone else who worked so hard to organize this workshop.
Your Excellency,
        This workshop is intended to expose the top leadership from the three branches of government to the Malaysian transformation experience.  That experience, adjusted to suit our particular environment, should help us build a framework that will ensure robust implementation, monitoring and evaluation of our national plans for tangible results and in particular satisfactory delivery of public services.
        For that to happen, however, we must begin with open minds and with a willingness to think and do things differently.  We have to absorb and internalize the best in the experience of others.  We must learn to focus not so much on processes but on results, within prescribed timeframes.
        We must show the genuine willingness to measure and to be measured; to ascertain quality and standard, to ensure inclusion and to transform ourselves and our people.
Your Excellency;
Ladies and Gentlemen;
        The workshop is designed to ensure an interactive exchange of ideas, and as ideas have no protocol, we have likewise minimized protocol.  We encourage dialogue and participation by sharing experiences and thought on ways in which we can do things differently and better.
        With the hope that this indeed is what will happen over the next two days, it gives me great pleasure and honor to invite you, Mr. President, to deliver your opening speech to our workshop.
        Welcome Your Excellency.

RAIS KIKWETE AFUNGUA KONGAMANO LA TATU LA JUKWAA LA UHUSIANO WA CHINA NA AFRICA KATIKA KUPUNGUZA UMASKINI

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akifungua Kongamano la tatu la Jukwaa la Uhusiano wa China na Bara la Afrika lenye lengo la kuondoa umaskini katika hoteli ya White Sands jijini Dar es salaam July 28, 2012.Wa tatu toka kushoto ni Waziri wa China anayeshughulikia Umaskini Mhe Fan Xiaojian, wa pili kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya rais Mhe Steven Wassira, wa pili kushoto ni Naibu Waziri wa Fedha na Maendeleo ya Uchumi wa Sierra Leone Mhe Momodu Kargbo, kushoto ni Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango Mipango Dkt Philip Mpango na kulia kabisa ni Balozi wa China hapa nchini Mhe L.V. Youqing.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia katika ufunguzi wa Kongamano la tatu la Jukwaa la Uhusiano wa China na Bara la Afrika katika hoteli ya White Sands jijini Dar es salaam July 28, 2012.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika mazungumzo rasmi na Waziri wa China anayeshughulikia Umaskini Mhe Fan Xiaojian baada ya ufunguzi wa Kongamano la tatu la Jukwaa la Uhusiano wa China na Bara la Afrika lenye lengo la kuondoa umaskini,ufunguzi huo ulifanyika katika hoteli ya White Sands jijini Dar es salaam July 28, 2012.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimsikiliza Waziri wa China anayeshughulikia Umaskini Mhe Fan Xiaojian(kuhsoto) na Balozi wa China hapa nchini Mhe L.V. Youqing. baada ya kufungua Kongamano la tatu la Jukwaa la Uhusiano wa China na Bara la Afrika katika kuondoa umaskini.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe toka china unaohudhulia Kongamano la tatu la Jukwaa la Uhusiano wa China na Bara la Afrika katika kuondoa umaskini,lililofanyika katika hoteli ya White Sands jijini Dar es salaam July 28, 2012.PICHA NA IKULU.

RAIS JAKAYA KIKWETE AZINDUA KARAKANA (HANGA) YA NDEGE ZA SHIRIKA LA NDEGE LA PRECISION AIR

Mwenyekiti wa bodi ya Shirika la ndege la Precision Air Bw. Michael Shirima akimkabidhi zawadi Mh Rais Dk. Jakaya Kikwete mara baada ya kuzinduz rasmi karakana na ndege za shirika hili (Hanga) kwenye uwanja wa ndege wa Mwalimu J.K.Nyerere leo jijini Dar es salaam, Karakana hiyo itakuwa ikihudumia ndege za shirika hilo la mashirika mengine pia lakini pia itapokea wanafunzi walio kwenye mafunzo ya Uinjini wa ndege kutoka katika vuo vya ndani.
Rais Jakaya Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Uchukuzi Dk Harrison Mwakyembe pamoja na wakuu mbalimbali wa shirika la ndege la Precision Air na wafanyakazi wa shirika hilo mara baada  ya uzinduzi wa (Hanga) hiyo
Rais Jakaya Kikwete akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la ndege la Precision Air Bw. Alfonce Kioko alipokuwa akitoa maelezo  wakati wakati Rais alipokuwa akikagua  Hanga hiyo, kulia ni Waziri wa Uchukuzi Dk Harrison Mwakyembe 
Rais Jakaya Kikwete akizungumza jambo na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya shirika la ndege la Precision Air Bw. Michael Shirima katikati mara baada ya kuzindua Karakana ya ndege za shirika hilo, kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la ndege la Precision Air Bw. Alfonce Kioko
Rais Jakaya Kikwete akiweka mkasi mara baada ya kukata utepe ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa Karakana na ndege za shirika la ndege la Precision Air leo kwenye uwanja wa ndege wa Mwalimu J.K.Nyerere jijini Dar es salaam kulia ni Bw Bw. Michael Shirima
Rais Jakaya Kikwete akisalimiana na Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi ya Precision Air Bw Michael Shirima wakati alipowasili katika uwanja wa ndege wa J.K. Nyerere tayari kwa uziduzi wa Karakana wa ndege za  kampuni hiyo, kulia ni Mkurugenzi wa kampuni hiyo Bw Alfonce Kioko, katikati ni Waziri wa Uchukuzi Dk Harrison Mwakyembe na kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Said Meck Sadik
Mkurugenzi wa Hoteli ya Kibo Palace ya Arusha Bw Vicent Laswai naye amehudhuria katika uzinduzi huo kama mdau wa Utalii.Picha zaidi Bofya Hapa.

MAADHIMISHO YA KITAIFA YA SIKU YA KUMBUKUMBU YA MASHUJAA VIWANJA VYA MNAZI MMOJA JIJINI DAR ES SALAAM

Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwasili katika viwanja vya bustani ya Mnazi Mmoja tayari kutoa  heshima kwa mashujaa


Baadhi ya skari wa zamani wa KAR wanaounda Tanzania Legion
Gadi ya Askari Magereza
Gadi ya JWTZ
Askari wa JWTZ wakiwakumbuka mashujaa kwa heshima ya dakika tatu huku mizinga ikipigwa

Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiweka mkuki mnarani kama  heshima kwa mashujaa
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akitoa heshima kwa mashujaa baada ya kuweka mkuki na ngao
Mkuu wa Majeshi Jenerali Davis Mwamunyange akiweka sime mnarani
Ni wakati wa wimbo wa Taifa mara tu baada ya kuwasili kwa Rai Kikwete
Baadhi ya waalikwa ikiwa ni pamoja na mabalozi wa nchi za nje
Kiongozi wa Mabalozi na Balozi wa DRC Nchini Mhe Khalfan  Mpango akiweka shada la maua
Meya wa Jiji la Dar es salaam Mstahiki Dkt Didas Masaburi akiweka upinde na mshale
Mwenyekiti wa Wazee wa Dar es salaam Mzee Rashidi Bakari Ngonja akiweka shoka

Gadi ya FFU


Sheikh wa mkoa wa Dar es salaam Sheikh Alhad Mussa Salum akiomba dua 
Mchungaji  John Kamoyo wa CCT akitoa neno
Monsinyori Deogratias Mbiku wa Kanisa Katoliki akisoma sala
Baadhi y mashujaa waliowahi kupigana vita
Wimbo wa Taifa baada ya shughuli kumalizika
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Viongozi wa kitaifa
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na baadhi ya mashujaa
Salamu kwa Mashujaa
Mashujaa
Wanahabari wakirekodi shughuli nzima
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiongea na baadhi ya  mashujaa

Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiagana na viongozi wa majeshi baada ya kutoa  heshima kwa mashujaa
Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiagana na Mkuu wa Majeshi Jenerali Davis Mwamunyange

Rais Kikwete azindua mradi wa maji jijini Mbeya

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete,Kamishna wa Maendeleo katika Jumuiya ya Ulaya Andris Piebalgs(wapili kushoto), balozi wa jumuiya ya ulaya nchini Cerian Philberto Sebregondi(kushoto),Balozi wa Ujerumani nchini Klaus Peter Brandes na Waziri wa Maji Profesa Jumanne Maghembe wakikata utepe kuzindua rasmi mradi wa maji safi na mazingira Mjini Mbeya leo mchana.

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na Kamishna wa Maendeleo katika jumuiya ya Ulaya Andris Piebalgs wafunua kitambaa katika jiwe la msingi wakati wa uzinduzi wa MRADI WA MAJI SAFI na usafi wa mazingira katika eneo la Swaya mjni Mbeya leo.

Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete,Kamishna wa Maendeleo Jumuiya ya Ulaya Andris Piebalgs(Watau kushoto) na Waziri wa Maji Profesa Jumanne Maghembe wakikagua chanzo cha maji eneo la Swaya mjini Mbeya wakati wa uzinduzi wa mradi maji safi na mazingira mjni humo leo mchana.Picha na mdau Freddy Maro wa Ikulu.

Kusoma hotuba ya Rais Kikwete BOFYA HAPA

RAIS KIKWETE AKUTANA NA KAMATI YA BUNGE YA MAMBO YA NJE NA ULINZI NA USALAMA, ATEMBELEA MAKAO MAKUU YA SMART PARTNERSHIP

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika mazungumzo na wajumbe wa Kamati Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama iliyomtembelea jijini London, Uingereza, Julai 12, 2012.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimsindikiza Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama,Mhe. Edward Lowassa muda mfupi baada ya kukutana nao jijini London,Uingereza, Julai 12, 2012

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama iliyomtembelea jijini London, Uingereza, Julai 12, 2012.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akishiriki katika kikao maalumu cha maandalizi ya mkutano wa Commonwealth Partnership for Technology Management (CPTM) kwenye makao makuu ya CPTM inayojiandaa kwa mkutano wake mkuu wa Global 2012 International Smart Partneship Dialogue unaotarajiwa kufanyika mwezi Mei Mwakani jijini Dar es salaam.PICHA NA IKULU

wananchi wafurahia kuonana na Rais Jakaya Kikwete viwanja vya sabasaba

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na wananchi katika viunga vya uwanja wa maonesho vya Mwalimu Nyerere jijini Dar es salaam. Wananchi walijipanga njiani na kusalimiana naye wakati yeye na Mama Salma Kikwete walipokuwa wakitembelea banda moja hadi lingine.  

 

 

 Unamuona…yuleeeee anapita!

 Na mimi badooo jamani….

 Sisi tunatoka Marekani… tunafurahi kusabahiana nawe

 Wow! The man himself…awesome…

 Hamjambo,,,?

 Mambo,,,,!

Tumefurahi…

RAIS KIKWETE AREJEA NCHINI TOKA RWANDA NA BURUNDI

Rais Dkt Jakaya Mrisho Kikwete na Mama Salma Kikwete wakiwasili Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam jana jioni wakitokea Burundi na Rwanda walikohuidhuria sherehe za miaka 50 wa uhuru wa nchi hizo. Anayeongozana nao ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe Saidi Mecky Sadik.

Rais Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akilakiwa na Inspekta Jenerali wa Polisi Afande Saidi Mwema na Mkuu wa Majeshi Jenerali Davies Mwamunyange baada ya kuwasili Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es salaam jana jioni wakitokea Burundi na Rwanda walikohuidhuria sherehe za miaka 50 wa uhuru wa nchi hizo.PICHA NA IKULU.

HOTUBA YA MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWA WANANCHI, TAREHE 30 JUNI, 2012

Ndugu Wananchi,

          Kama ilivyo ada naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kumaliza nusu ya kwanza ya mwaka 2012 salama.  Kwa kutumia utaratibu wetu wa kuzungumza nanyi kila mwisho wa mwezi, leo napenda kuzungumzia mambo mawili. Jambo la kwanza ni suala la usafirishaji haramu wa binadamu nchini na la pili ni la mgomo wa madaktari.
Usafirishaji Haramu wa Binadamu Nchini
Ndugu Wananchi;
          Bila ya shaka mtakuwa mmezisikia taarifa za tukio la kushtusha na kuhuzunisha la kukutwa maiti 43 za watu wasiojulikana, zilizotupwa katika kichaka kilichopo kijiji cha Chitego, Wilayani Kongwa, Mkoa wa Dodoma tarehe 26 Juni, 2012.  Pamoja na maiti hao, walipatikana watu 84 wakiwa hai lakini wote wakiwa wamedhoofu na baadhi yao wakiwa mahututi.  Hatua za haraka zilichukuliwa kuwasafirisha watu hao hadi Dodoma ambapo wale waliokuwa mahututi walifikishwa Hospitali Kuu ya Mkoa wa Dodoma kwa matibabu na wengine walihifadhiwa katika Kituo cha Kati cha Polisi, Dodoma.  Maiti 22 zilipelekwa Dodoma na 21 zilipelekwa Morogoro kuhifadhiwa.
Taarifa zilizopatikana kutoka kwa wale walionusurika zimebainisha kuwa watu hao ni raia wa Ethiopia ambao walikuwa safarini kwenda Malawi na baadaye Afrika ya Kusini ambako wangetengenezewa utaratibu wa kwenda kuishi Marekani na Ulaya.  Kwa mujibu wa maelezo yao, safari yao ilianza miezi mitano iliyopita.  Mwezi mmoja waliutumia Ethiopia na miezi minne waliitumia Kenya kabla ya kuletwa Arusha ambako walipakiwa kwenye lori na kuanza safari ya kuelekea Malawi lakini ikaishia Chitego.  Lori walilopanda lilikuwa limezibwa kabisa na hivyo kusababisha vifo kwa kukosa hewa.
Tukio la Chitego, Dodoma la wahamiaji haramu kukamatwa na wengine kukutwa wamekufa si la kwanza kutokea hapa nchini.  Kwa jumla, katika kipindi cha takriban miaka 10 sasa kumekuwepo na tatizo kubwa la wahamiaji haramu kuingia nchini.  Kwa mfano, kati ya mwaka 2005 na hivi sasa jumla ya wahamiaji haramu 19,683 wamekamatwa.  Karibu wote wameshaondoshwa nchini na hivi sasa wapo karibu watu 1,500 tu magerezani wanaotumikia adhabu na kusubiri kurejeshwa makwao.  Wengi wa watu hao wanatoka Ethiopia na Somalia na baadhi kutoka Pakistan na Bangladesh.
Wahamiaji haramu wamekuwa wanaingia nchini kwa kupitia njia zisizo rasmi.  Wapo wanaotumia nchi kavu hasa kupitia mikoa ya Mara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga.  Na, wapo wanaopitia baharini kwa kutumia fukwe za Pemba, Unguja na za mikoa ya ukanda wa Pwani ya Tanzania Bara yaani Tanga, Pwani, Lindi na Mtwara.
Ndugu Wananchi;
Kwa mujibu wa kauli zao, watu hao wamekuwa wanaeleza kuwa hawaji nchini kuhamia bali wao ni wapita njia tu.  Wanaelekea Afrika ya Kusini ambako wameahidiwa kuwa watatengenezewa mipango ya kuhamia Marekani na Ulaya.  Watu hao pia wamethibitisha kuwepo kwa watu maalum wanaojihusisha na usafiri wao tangu nchi watokako na zote wanazopitia mpaka kule waendako.  Aidha, wamesema kuwa wao wanawalipa watu hao ili wawasafirishe na hakika si kiwango kidogo.  Kwa jumla ni kwamba hili si suala la uhamiaji haramu bali ni la biashara haramu ya kusafirisha binadamu.
Ndugu Wananchi;
Kufuatia vyombo vyetu vya usalama kuwa makini na watu wengi kukamatwa ndipo wasafirishaji walipobuni njia za kuwasafirisha kama mizigo.  Makontena, malori yaliyofunikwa nyuma na matenki ya mafuta na ya maji yamekuwa yanatumika kwa ajili hiyo.  Usafiri wa aina hiyo ndiyo uliosababisha vifo vilivyotokea Dodoma tarehe 26 Juni, 2012 na vya watu 21 vilivyotokea mwezi Desemba, 2011 Mkoani Morogoro, na vile vya watu 12 vilivyotokea katika matukio mawili ya Mkoa wa Mbeya, mwezi Mei, 2012.
Ndugu Wananchi;
Tarehe 27 Juni, 2012 nilikutana na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama nchini kuzungumzia tukio la Chitego na suala zima la biashara hii haramu na hasa mbinu mpya inayotumiwa na wasafarishaji.  Nilitoa pongezi kwa vyombo vya dola kwa kazi nzuri waifanyayo kudhibiti shughuli za biashara hii haramu hapa nchini.  Tulielewana kuwa waendelee kuimarisha udhibiti huo kwa lengo la kukomesha kabisa biashara hii.
 Niliagiza pia kwamba kikundi kazi nilichokiunda mwaka 2006 kushughulikia ujambazi sasa kielekeze sehemu ya nguvu zake kukabili tatizo hili. Aidha, kwa pamoja tulikubaliana kuwa nchi yetu ishirikiane na wenzetu wa Ethiopia, Kenya, Malawi, Msumbiji na Afrika ya Kusini kutambua mawakala na kuwabana kwa mujibu wa sheria.  Tayari nimeshaanza kufanya mawasiliano na baadhi ya Wakuu wa Nchi hizo kuhusu ushirikiano huo.  Nashukuru wote wameafiki nchi zetu zishirikiane kwa pamoja kuvunja mtandao huu mchafu na kutokomeza biashara hii haramu na inayodhalilisha utu wa mwanadamu.
Ndugu Wananchi;
Napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wenzetu, wakazi wa vijiji vya Chitego na Mkoka kwa kazi nzuri walioifanya. Kwa kweli, wenzetu wameonesha uzalendo wa hali ya juu kwa kutoa taarifa mapema juu ya jambo lenyewe, lakini pia wameonesha utu kwa kuwajali wageni waliokumbwa na janga hili. Naushukuru pia uongozi wa Mkoa wa Dodoma na Morogoro ikiwa ni pamoja na vyombo vya ulinzi  na usalama kwa kulishughulikia tatizo hilo kwa umakini mkubwa.   Nimefurahishwa sana na ushirikiano ulioonyeshwa na vyombo na taasisi mbalimbali za Serikali katika kushughulikia suala hili.
Mgomo wa Madaktari
Ndugu Wananchi;
          Jambo la pili ni kuhusu mgomo wa Madaktari unaoendelea nchini hivi sasa.  Nilipozungumza na Wazee wa Dar es Salaam katika Ukumbi wa Diamond Jubilee tarehe 12 Machi, 2012, kuhusu mgomo wa Madaktari uliokuwa unaendelea wakati ule pamoja na kuelezea chimbuko la mgomo na hatua iliyokuwa imefikiwa, nilielezea mazungumzo yangu na viongozi wa Chama cha Madakari wakiwemo pia viongozi wa Jumuiya ya Madaktari.  Nilitoa taarifa kuwa tumeelewana kuwa watasitisha mgomo na watarudi kwenye meza ya majadiliano na Serikali.  Siku ile pia nilielezea matumaini yangu kuwa mgomo ule utakuwa wa mwisho katika nchi yetu.  Bahati mbaya matumaini yangu hayo hayakuwa na hivi sasa tunashuhudia tena wagonjwa wakiteseka, kuhangaika na wengine kufa kwa sababu ya kukosa huduma wanazostahili kwa vile madaktari wao wamegoma tena.
Ndugu Wananchi;
Kama walivyoniahidi, madaktari waliacha kugoma na viongozi wao walirudi kwenye mazungumzo na Serikali.  Kama ilivyoagizwa na Mahakama Kuu, Kitengo cha Kazi tarehe 8 Machi, 2012, kwa mujibu wa Sheria ya Mahusiano Kazini, Namba 6 ya mwaka 2004.   Chama cha Madaktari na Serikali walifika katika Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (Commission for Mediation and Arbitration) kwa ajili ya majadiliano.  Kwa pamoja na kwa ridhaa yao wote, pande hizo mbili ziliiomba Tume hiyo iwape fursa ya kuzungumza wao wenyewe na wakimaliza mazungumzo wataenda kusajili makubaliano yao.  Tume ikawakubalia.  Ni vizuri ikakumbukwa kuwa siku ile ya tarehe 8 Machi, 2012 Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, ilitoa zuio la mgomo pamoja na kuagiza kuwepo mazungumzo baina ya pande mbili.
Ndugu Wananchi;
Kati ya tarehe 10 Aprili, 2012 na tarehe 30 Mei, 2012, vilifanyika vikao sita vya majadiliano kati ya Serikali na Chama cha Madaktari.  Katika mazungumzo hayo hoja au madai 12 ya madaktari yalizungumzwa.  Mambo hayo ni haya yafuatayo:
1.    Posho ya kuitwa kazini (on call allowance) iwe asilimia 10 ya mshahara.
2.    Posho ya kufanya kazi katika mazingira hatarishi (Risk allowance) iwe asilimia 30 ya mshahara.
3.    Madaktari wapatiwe nyumba grade A au posho ya makazi ambayo iwe asilimia 30 ya mshahara.
4.    Posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu iwe asilimia 40 ya mshahara.
5.    Madaktari walipwe posho ya usafiri ya asilimia 10 ya mshahara au wakopeshwe magari.
6.    Madaktari wanaoanza kazi walipwe mshahara wa shilingi 3,500,00/= kwa mwezi.
7.    Madaktari wapatiwe Green Card za Bima ya afya.
8.    Hatua za kinidhamu zichukuliwe dhidi ya Watendaji Wakuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
9.    Viongozi wa Kisiasa kulazimisha kupewa rufaa nje.
10.           Madaktari waliofukuzwa warudishwe kazini.
11.           Huduma za afya ziboreshwe nchini.
12.           Posho ya uchunguzi wa maiti iongezwe.
Ndugu Wananchi;
          Katika mambo hayo 12 pande zote mbili zilifikia muafaka na kukubaliana wa pamoja kwa mambo saba.  La kwanza, ni kuhusu usafiri wa kwenda na kurudi kazini.  Serikali ilieleza kuwa upo utaratibu kwa mujibu wa Waraka wa Utumishi wa Serikali Na. 3 wa mwaka 2011 wa kuwakopesha wafanyakazi wa Serikali fedha za kununulia magari au pikipiki, samani na matengenezo ya magari.  Ilikubaliwa kuwa madaktari waitumie fursa hiyo.
          Jambo la pili, ni kuhusu madaktari kupatiwa Green Card za Bima ya Afya.  Jambo hili lilikubaliwa na Serikali na Wizara ya Afya imekwishachukua hatua za utekelezaji wake.
          Jambo la tatu, ni kuhusu hatua za kinidhamu kuchukuliwa dhidi ya Watendaji Wakuu wa Wizara ya Afya.  Kwa pamoja walikubaliana kuwa suala hilo liko nje ya mamlaka ya Kamati yao ya pamoja, waziachie mamlaka husika za uteuzi.  Uongozi wa juu wa Wizara umebadilishwa na sasa kuna uongozi mpya.  Lakini, jambo la kustaajanisha hata Waziri mpya wa Afya alipowataka waonane kuzungumzia hoja walikataa kumuona.  Kwanza walisema hawaoni sababu kwa vile wameyazungumza na Kamati yake kwa miezi mitatu bila ya mafanikio
          Jambo la nne walilokubaliana ni kuhusu viongozi kulazimisha kupewa rufaa ya kutibiwa nje.  Walikubaliana mambo mawili.  Kwanza, kwamba maelekezo ya Waziri Mkuu, Mhe. Mizengo Pinda kuwa madaktari wazingatie maadili ya kazi zao na kukataa kutoa rufaa kwa mtu asiyestahili awe kiongozi au asiwe kiongozi. Pili, walikubaliana kuwa hospitali zilizopo ziboreshwe ili viongozi watibiwe hapa nchini.  Ukweli ni kwamba kufanya hivyo ndiyo sera ya Serikali.  Nililieleza hili mwezi Desemba 30, 2005 katika hotuba yangu ya kuzindua Bunge baada ya kuchaguliwa kwa mara ya kwanza kuongoza nchi yetu.
Tumeiongeza sana bajeti ya sekta ya afya kutoka shilingi bilioni 300 2005/2006 hadi shilingi trilioni 1.2 mwaka 2011/12 na imekuwa ya tatu baada ya miundombinu na elimu.  Tumeziimarisha hospitali za Mikoa kwa vifaa tiba na wataalamu wa afya.  Kazi inaendelea katika hospitali za Wilaya. Tumewekeza katika Hospitali ya Muhimbili.  Hospitali hiyo ilivyo leo sivyo ilivyokuwa miaka sita nyuma.  Na kazi inaendelea hasa katika maeneo ambayo tunapeleka wagonjwa nje.  Matunda yake yanaanza kuonekana kwa upande wa figo, moyo, kinywa na mipango inaendelea kwa upande wa ubongo na mishipa ya fahamu.  Tunaendelea kuimarisha mafunzo ya  madaktari na madaktari bingwa, yote kwa nia hiyo hiyo.  Hivi sasa Chuo Kikuu cha Sayansi ya Tiba,Muhimbili kinachukua wanafunzi wengi zaidi ya ilivyokuwa siku za nyuma na makazi mapya ya chuo yanaendelea kuandaliwa ili kuchukua wanafunzi wengi zaid.    Mwaka 2005 tulikuwa na madaktari bingwa 46 mwaka huu tunao 520.
Ndugu Wananchi;
          Jambo la tano ambalo pande zote mbili zilikubaliana ni kuhusu madaktari waliofukuzwa.  Hawa ni wale Interns waliokuwa wamerudishwa Wizarani kutoka Muhimbili na kupangiwa hospitali za Temeke, Ilala, Mwananyamala na Lugalo.  Hili ni jambo ambalo lilikuwa limemalizika kitambo na wote walikuwa wamerudi Muhimbili.
          Jambo la sita ni kuhusu mapendekezo mbalimbali yaliyotolewa na madaktari kuhusu kuboresha huduma ya afya.  Mapendekezo hayo yalihusu kutathmini sera na mpango wa afya ya msingi, bajeti ya afya kuwa asilimia 15 ya bajeti ya Serikali, kuwepo na utaratibu mzuri wa kuajiri madaktari na kuboresha viwango vya ubora wa madaktari na kadhalika.  Serikali imeyaafiki mapendekezo hayo na yatafanyiwa kazi.
          Jambo la saba, ambalo pande zote walilokubaliana ni kuhusu kuongeza posho ya uchunguzi wa maiti.  Hili ni jambo jipya halikuwepo mwazoni.  Hata hivyo, Serikali imelikubali na posho hiyo imeongezwa kutoka shilingi 10,000/= hadi kufikia shilingi 100,000/= kwa daktari na shilingi 50,000/= kwa wasaidizi wake.
Ndugu Wananchi;
          Kuna masuala matatu ambayo yamekuwa na muafaka kwa kiasi fulani na kutoafikiana kwa baadhi ya mambo.  La kwanza ni suala la kufanya kazi katika mazingira hatarishi.  Serikali imekubali hoja ya kuchukua hatua ya kuwalinda madaktari wanaofanya kazi katika mazingira hatarishi.  Serikali iliwaeleza kuwa watumishi wa kada zote za afya watapatiwa chanjo dhidi ya maambukizi ya Hepatitis B na fedha zimetengwa katika bajeti ya 2012/13.
Aidha, Serikali imeeleza dhamira ya kurudisha posho ya mazingira hatarishi kwa watumishi wa umma wanaostahili.  Utekelezaji wake utafanyika baada ya uchambuzi wa kina wa kubainisha mazingira hatarishi ni yepi, viwango stahiki viwe vipi na nani hasa wahusike.  Madaktari wamekataa hili la kufanya uchambuzi, wanataka kiwango kiwe kama wanavyotaka wao, yaani asilimia 30 ya mshahara na kianze mara moja.
          Jambo la pili ambalo wamekubaliana nusu nusu ni kuhusu nyumba za kuishi.  Serikali imekiri wajibu wake wa kuwapatia madakari nyumba za kuishi.  Aidha, imeeleza mpango ulioanza wa kujenga nyumba 700 za madaktari kote nchini na kwamba hivi sasa ujenzi wa nyumba 90 unaendelea, 50 katika mkoa wa Mtwara na 40 katika mkoa wa Rukwa.
 Kwa maeneo ambayo madaktari wanalipwa posho ya pango Serikali imesema waajiri wataendelea kufanya hivyo kwa mujibu wa taratibu zilizopo kwa watumishi wa umma wenye stahili ya kupewa nyumba.  Jambo hilo limekataliwa na Madakari na kutaka lazima walipwe asilimia 30 ya mshahara kama posho ya nyumba.  Serikali kwa upande wake imeona vigumu kufanya hivyo na kuwasihi wakubali wanayotendewa wafanyakazi wengine wote wa umma.
          Jambo lingine ambalo lilikuwa na makubaliano ya nusu nusu ni kuhusu posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu.  Pande zote mbili ziliafikiana kuwa yapo baadhi ya maeneo nchini yanayo mazingira magumu kwa watumishi wa umma  hivyo hatua zichukuliwe kuwasaidia watumishi hao. Serikali imekubali wajibu wa kuweka utaratibu wa kuboresha maisha ya watumishi katika maeneo hayo.  Kwa ajili hiyo, Serikali itatoa mwongozo kwa mamlaka za ajira kuhusu namna ya kuwasaidia watumishi hao kupunguza makali ya maisha katika kila eneo badala ya kutegemea posho peke yake.
  Kuhusu posho, Serikali imeeleza kuafiki kuwepo posho ya aina hiyo ila itatekelezwa baada ya kufanya uchambuzi wa kuainisha mazingira husika, kutambua watumishi waliopo na gharama zake.
          Madaktari hawajakubali kusubiri zoezi la uchambuzi lifanyike, wanataka Serikali ilipe posho hiyo sasa.  Tofauti hapa si posho hiyo kuwepo, bali ni rai ya Serikali ya kubaini maeneo yenyewe na kupanga aina ya hatua na viwango vya posho kulingana na mazingira halisi ya maeneo.  Madaktari hawaoni haja ya kufanya hayo.
Ndugu Wananchi;
          Mambo mawili hayakuwa na muafaka kabisa kati ya pande zetu mbili.  Jambo la kwanza ni posho ya kuitwa kazini (on call allowance).  Kwanza sina budi kueleza kuwa Serikali imekubali kuongeza posho hiyo.  Tangu Februari, 2012 posho iliongezwa kutoka shilingi 10,000/= hadi shilingi 25,000/= kwa daktari bingwa (Specialist), shilingi 20,000/= kwa dakari mwenye usajili wa kudumu (Registrars) na shilingi 15,000/= kwa madaktari waliohitimu ambao wapo katika kipindi cha mafunzo kazini (Interns).  Viwango hivyo vya posho vinatumika hivi sasa.
  Madaktari kwa upande wao hawakukubali uamuzi huo wa Serikali na kusisitiza walipwe asilimia 10 ya mshahara.  Ugumu wa kukubali pendekezo la madakari ni kuwa sharti la malipo haya ni mtu kuitwa kazini.  Ukitaka ilipwe kiwango cha mshahara ina maana kuwa hata kama daktari hakupangwa kuitwa au alipangwa na hakutokea aendelee kulipwa.  Hili haliwezi kuwa sahihi kufanya.  Linaweza kuwafanya baadhi ya madaktari kutokutimiza wajibu wao kwa vile wana hakika mwisho wa mwezi malipo yako pale pale.
Ndugu Wananchi;
Jambo la pili ambalo muafaka haukufikiwa baina ya Serikali na madaktari ni kuhusu mshahara wa kuanzia kazi wa daktari.  Madaktari wanataka uwe shilingi 3,500,000/= wakati Serikali inasema kiasi hicho hatukiwezi.  Serikali imeeleza utayari wake wa kuongeza mshahara kwa kati ya asilimia 15 mpaka 20 kama ambavyo itafanya kwa watumishi wote wa umma katika mwaka huu wa fedha.  Kwa kiwango cha sasa cha mshahara wao, daktari ataanzia kati ya shilingi 1,100,000/= na 1,200,000/= kutegemea kiwango kipi hatimaye kitaamuliwa.  Madaktari wamekataa katakata na wameng’ang’ania shilingi 3,500,000/=.
Ndugu Wananchi;
Huo ndiyo mlolongo wa mambo yaliyozungumzwa na pande zote mbili na matokeo ya mazungumzo yenyewe.  Katika kikao cha sita kilichofanyika tarehe 30 Mei, 2012, upande wa Chama cha Madaktari ulisema kuwa kwa vile hoja ya nyongeza ya mshahara haina mabadiliko hawakuona haja ya kuendelea na majadiliano mpaka watakapowasiliana na wenzao.  Waliahidi kutoa taarifa ndani ya wiki mbili.  Tarehe 12 Juni, 2012, Rais wa MAT aliandika barua kwa Katibu Mkuu Utumishi ambaye ndiye kiongozi wa majadiliano kwa upande wa Serikali, kuwa Madaktari wameikataa taarifa na ufafanuzi waliopewa kutoka Serikalini kwa ujumla wake.
Ndugu Wananchi;
 Baada ya majibu yale ya madaktari, tarehe 19 Juni, 2012, Serikali na Madaktari walikwenda kwa Msuluhishi (CMA) kutoa taarifa kuwa mgogoro umekosa usuluhishi kama sheria inavyotaka.  Kwa pamoja pande zote mbili zilikubaliana suala hilo lifikishwe Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi.  Wakati pande zote zinasuburi mgogoro huu kufikishwa ngazi hiyo ya juu, upande wa Madaktari ukatangaza kuwepo kwa mgomo kuanzia saa sita ya usiku tarehe 23 Juni, 2012.  Hatua hiyo haikustahili kwani suala lenyewe halijafika mwisho wa kushughulikiwa kwa mujibu wa Sheria za Mahusiano ya Kazi nchini.
Ndugu Wananchi;
Tarehe 22 Juni, 2012, Mwanasheria Mkuu wa Serikali akaenda Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi kulifikisha suala la tishio la mgomo na kuomba zuio la muda kufanywa.   Mahakama Kuu ilikubali ombi hilo na kuagiza kuwa mgomo usitishwe.  Juhudi za kumtafuta Rais wa MAT, Dkt. Namala Mkopi na viongozi wengine wa MAT hazikufanikiwa, Ofisi ya MAT ilikuwa imefungwa na simu zote za viongozi wa MAT zilikuwa zimezimwa.  Hatimaye tarehe 25 Juni, 2012, alipatikana na kupewa amri hiyo ya Mahakama.  Tarehe 26 Juni, 2012, Dkt. Mkopi alifika Mahakamani ambapo alikana kuwa yeye hahusiki na kuitisha huo mgomo lakini hakumtaja aliyehusika.  Pamoja na rai hiyo, Jaji alimuamuru Rais wa MAT akawatangazie wanachama wake kusitisha mgomo.   Dkt. Namala Mkopi hajafanya hivyo hadi leo na mgomo umekuwa unaendelea kinyume cha Sheria.
Ndugu Wananchi;
Wagonjwa wanateseka na wengine kupoteza maisha kwa mgomo huu usiokuwa halali kisheria ambao pia haustahili kuwepo hata kwa mujibu wa maadili ya udaktari.  Viongozi wa  MAT na wenzao wanawaingiza Madaktari katika mgogoro na Mahakama na waajiri wao isivyostahili.  Ni vyema viongozi wa Madaktari na madaktari wakatambua kuwa wanashiriki katika mgomo usiokuwa halali ambao pia kiongozi wao mkuu amekana Mahakamani kuwa hahusiki nao.  Madaktari lazima watambue pia kwamba ajira zao wanaziweka hatarini.  Mfanyakazi ana kinga ya kutofukuzwa kazi na mwajiri kwa kushiriki mgomo unaokubalika kisheria.  Huu siyo.  Watapoteza ajira, hawana pa kukimbilia, hawana cha kiwalinda.  Kwa madaktari interns, wanahatarisha maisha yao kwani hawatapata cheti cha kudumu wakishiriki mgomo usiokuwa halali.   Lazima watafakari sana kwa hayo wafanyayo.
Ndugu Wananchi;
          Napenda kurudia maneno niliyoyasema tarehe 12 Machi, 2012, kuwa kuboresha mishahara na maslahi ya wafanyakazi ni Sera ya Serikali yetu kwa maelekezo ya Ilani ya Chama Tawala (CCM).  Tumeitekeleza kwa vitendo sera hiyo, hata hivyo ni ukweli ulio wazi kuwa nia yangu njema tu pekee haitoshi, lazima uwezo wa kufanya hivyo uwepo.  Kwa kulingana na uwezo uliopo, tumeendelea kuboresha mishahara na maslahi ya wafanyakazi hatua kwa hatua tangu tuingie madarakani.  Tumefanya hivyo kwa jumla kwa wafanyakazi wote na kwa kada mbalimbali za watumishi wa umma.
Miongoni mwa wafanyakazi wa umma walionufaika na hatua hizo za Serikali ni madaktari na watumishi wa kada nyingine za huduma ya afya.  Tena nadiriki kusema madaktari tumewapa upendeleo mkubwa kuliko watumishi wengine wa umma.  Upendeleo upo kwenye mafunzo ambapo wanafunzi wa udaktari wanagharimiwa na Serikali kwa asilimia mia moja wakati wanafunzi wenzao wa taaluma nyingine hawako hivyo.
Ndugu Wananchi;
Mwaka 2004/2005, mshahara wa kuanzia wa daktari ulikuwa shilingi 178,700/=, mwaka 2005/ 2006 tuliupandisha na kuwa shilingi 403,120/=. Tuliendelea kuupandisha mwaka hadi mwaka mpaka kufikia shilingi 957,700/= wanazolipwa sasa.  Kiasi hicho ni mara mbili ya mishahara ya watumishi wa taaluma nyingine wenye shahada ya kwanza wanaoanza kazi ambao kwa wastani hupata shilingi 446,100/=.
Tunafanya hivyo kwa kutambua na kuthamini nafasi maalum ya madaktari katika jamii na ukweli kwamba bado tunayo safari ndefu ya kuziba pengo la madaktari nchini.  Lakini inaonekana juhudi zetu zote hizo hazithaminiwi.
Ndugu Wananchi;
Sina budi kusisitiza  kwamba tunapofanya hivyo tunaongozwa na uwezo tulio nao wa kulipa.   Kwa sasa hatuwezi kuwaahidi kuwa tunao uwezo wa kuwalipa mshahara wa kuanzia wa shilingi 3,500,000/= na posho zote zile. Tukifanya hivyo malipo ya daktari anayeanza kazi yatakuwa shilingi 7,700,000/=.  Kwa hakika kiasi hicho hatutakiweza. Si vyema kutoa ahadi hewa kwa watu tunaowaheshimu na kuwathamini kama walivyo madaktari.
Kutokana na ukweli huo basi kama daktari anayeona kuwa hawezi kufanya kazi Serikalini bila ya kulipwa mshahara huo awe huru kuacha kazi na kwenda kwa muajiri anayeweza kumlipa kiasi hicho.  Nasi tutamtakia kila la heri.  Hana sababu ya kugoma ili ashinikize kulipwa mshahara huo. Asisumbuke, hatalipwa mshahara huo.  Isitoshe, hana sababu ya kuendelea kuwa na mgogoro na mwajiri ambaye hana uwezo wa kumlipa anachokitaka.  Huna sababu ya kumpa usumbufu mwajiri wa kukuandikia barua ya kujieleza au kukuachisha kazi.  Kwa nini upate usumbufu wa kupata barua hizo na kuzijibu. Kwa nini upate usumbufu wa kuachishwa kazi na kutakiwa kuondoka kwenye nyumba ya Serikali ndani ya saa 24.  Jiepushe na yote hayo kwa kujiondoa mwenyewe.  Usipofanya hivyo, mwajiri anakuwa hana jinsi bali kukuondoa kazini maana unakwenda kinyume na sheria za kazi na maadili ya kazi ya udaktari.
  Mamlaka za ajira zimeanza kuchukua hatua hizo na wataendelea kufanya hivyo kwa wote wanaoendelea kugoma.   Najua baada ya hatua hizo kuchukuliwa kuna manun’guniko ya kuonewa. Hivyo, mlitegemea mwajiri afanyeje? Ni bora kufanya hivyo ili ajue hana daktari aweze kufanya utaratibu wa kuziba hilo pengo na huyo ajae awe na mahali pa kuishi. Vinginevyo atakuwa anajidanganya kuwa anae daktari ambae hayupo kazini na wala hataki kufanya kazi.
Ndugu Wananchi;
Napenda kuwathibitishia kwamba dhamira ya Serikali ya kuboresha maslahi ya watumishi wa umma wakiwemo  madaktari iko wazi.  Tumekuwa tunafanya hivyo, na tutaendelea kufanya hivyo kulingana na uwezo wa kibajeti.  Ni vyema watumishi wa umma wakatambua kuwa hatuwezi kutumia fedha zote au kiasi kikubwa mno cha pesa za umma kulipana mishahara.  Tukifanya hivyo, Serikali itashindwa kutoa huduma muhimu kwa wananchi ambao ndiyo wengi na wanastahili kuhudumiwa.  Hata hizo huduma za afya tunazosema ni duni tuziboreshe, hatutaweza kuziboresha kama tutatumia sehemu kubwa ya pesa za Serikali kuwalipa mishahara wafanyakazi.
Hivi sasa matumizi ya mishahara ni asilimia 48 ya bajeti ya Serikali.  Kiwango hicho ni kikubwa mno.  Uwiano mzuri ni kuwa na matumizi ya mishahara yasiyozidi asilimia 35 ya bajeti na asilimia 65 zitumike kugharimia huduma na shughuli nyingine za maendeleo ya wananchi na taifa.  Sisi tumezidi kwa asilimia 13.  Hivyo, hatuna budi tukubali kujinyima kwa manufaa ya walio wengi.
Suala la Dkt. Steven Ulimboka
Ndugu Wananchi;
Kabla ya kumaliza hotuba yangu, napenda kuungana na Watanzania wenzangu wote kuelezea masikitiko yangu makubwa na kuhuzunishwa kwangu na kitendo cha kinyama alichofanyiwa Dkt. Steven Ulimboka usiku wa tarehe 26 Juni, 2012. Kitendo hicho ni kinyume kabisa na mila na desturi zetu. Watanzania hatujayazoea mambo hayo. Nimeelekeza vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi wa kina ili ukweli ujulikane.  Nimesema kuwa ningependa ukweli huo ujulikane mapema ili tuondoe wingu baya la kutiliana shaka na kulaumiana kunakoendelea hivi sasa.
Natambua kuwa Serikali nayo inatajwa katika orodha ya wanaotiliwa shaka.  Mimi nimeshangazwa sana na hisia hizo kwani siioni sababu ya Serikali kufanya hivyo.  Dkt. Ulimboka alikuwa mmoja wa kiungo muhimu katika mazungumzo baina ya Serikali na Madkatari.  Ni kweli kwamba yeye si mtumishi wa Serikali, hivyo hakustahili kuwa sehemu ya majadiliano haya.  Kulikuwa na rai ya kutaka asiwepo, lakini nilisema wamuache maadam Madaktari wanamuamini kuwa anaweza kuwasemea vizuri zaidi kuliko wao wenyewe walioajiriwa na Serikali.
Ndugu Wananchi;
Kama nilivyoeleza, mazungumzo yalienda vizuri na mafanikio makubwa yamepatikana.  Yapo maeneo machache na hasa eneo la mshahara ambalo hatukuweza kukubaliana.  Hapo tulipofikia si pabaya na tulikubaliana sote kurudi kwenye mkondo wa Sheria kusaidiwa.  Kwa nini Serikali imdhuru Dkt. Ulimboka? Na, kuhusu mgomo, Mahakama Kuu imekwishatoa amri ya kusitisha mgomo.  Anayekaidi amri ya Mahakama ananunua ugomvi na mhimili huo wa dola ambao wenyewe una mamlaka ya kumtia adabu mtu huyo.  Hivi baada ya kufika hapo Serikali iwe na ugomvi na Dkt. Steven Ulimboka kwa sababu ipi na jambo lipi hata iamue kumdhuru?  Kama kuna mtu wa Serikali kafanya, itakuwa kwa sababu zake binafsi na siyo za Serikali au kwa kutumwa na Serikali.
Ndugu Wananchi;  
Kwa niaba yangu na kwa niaba ya Serikali natoa mkono wa pole kwa Dkt. Steven Ulimboka na kumuombea apone haraka ili aungane na familia yake na Watanzania wenzake katika ujenzi wa taifa.  Kwa namna ya pekee namshukuru na kumpongeza Bwana Juma Mgaza, kwa moyo wake wa huruma na upendo na kwa hatua alizochukua za kumsaidia Dkt. Ulimboka.
Naomba kumaliza kwa kuwasihi madaktari kuacha mgomo na kurejea kazini.  Watanzania wenzenu wanateseka na kupoteza maisha.  Muwe na moyo wa huruma na upendo na msaada kwa wagonjwa kama kiapo chenu kinavyowataka.
Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!

Asanteni kwa Kunisikiliza.

 

Rais Kikwete aongoza watanzania sherehe za Muungano jijini Dar es Salaam leo

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiwapungia wananchi wakati alipokuwa akiingia katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam kuongoza maadhimisho ya mika 48 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar leo asubuhi.

Amiri jeshi Mkuu Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akikagua vikosi vya ulinzi na usalama wakati wa maadhimisho ya sikukuu ya miaka 48 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam leo.

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Mama Maria Nyerere leo katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam.

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba wakati alipowasili katika uwanja wa Uhuru kuongoza sherehe za Muungano zilizofanyika leo jijini Dar es salaam.picha na Freddy Maro.

RAIS KIKWETE KUZINDUA RASMI TUME YA KATIBA APRILI 13, 2012

Rais Jakaya Kikwete akitangaza majina ya wajumbe wa Tume ya katika

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete atazindua rasmi Tume ya Kukusanya na Kuratibu Maoni ya Mabadiliko ya Katiba na kuapisha wajumbe wa Tume hiyo Ijumaa ijayo, Aprili 13, mwaka huu, 2012.

Tume hiyo itazinduliwa na wajumbe wake kuapishwa kulingana na matakwa ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka 2011 iliyounda Tume hiyo. Aidha, Tume hiyo itazinduliwa rasmi wiki moja baada ya kuwa imetangazwa rasmi. Rais Kikwete alitangaza Tume hiyo jana, Ijumaa, Aprili 6, 2012, kwenye mkutano wa wahariri uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam.

Tume hiyo itakayoongozwa na Mwenyekiti Jaji Joseph Sinde Warioba akisaidiwa na Makamu Mwenyekiti Jaji Mkuu Mstaafu, Jaji Augustino Ramadhan ina wajumbe 30, ikiwa ni wajumbe 15 kutoka kila moja ya pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wajumbe wa Tume hiyo kutoka Tanzania Bara ni Profesa Mwesiga L Baregu, Ndugu Riziki Shahari Mngwali, Dkt. Edmund Adrian Sengodo Mvungi, Ndugu Richard Shadrack Lyimo, Ndugu John J Nkolo, Alhaji Saidi El Maamry na Ndugu Jesca Sydney Mkuchu.

Wajumbe wengine wa Tume hiyo kutoka Bara ni Profesa Palamagamba Kabudi, Ndugu Humphrey Polepole, Ndugu Yahya Msulwa, Ndugu Esther Mkwizu, Ndugu Maria Malingumu Kashonda, Mheshimiwa Al-Shaymaa J Kwegyir, Ndugu Mwantumu Jasmine Malale na Ndugu Joseph Butiku.

Wajumbe wa Tume hiyo kutoka Tanzania Visiwani ni Dkt. Salim Ahmed Salim, Ndugu Fatma Saidi Ali, Ndugu Omar Sheha Mussa, Ndugu Raya Suleiman Hamad, Ndugu Awadh Ali Saidi, Ndugu Ussi Khamis Haji na Ndugu Salma Maoulidi.

Wengine kutoka Visiwani ni Ndugu Nassor Khamis Mohammed, Ndugu Simai Mohammed Said, Ndugu Muhammed Yussuf Mshamba, Ndugu Kibibi Mwinyi Hassan, Ndugu Suleiman Omar Ali, Ndugu Salama Kombo Ahmed, Ndugu Abubakar Mohammed Ali na Ndugu Ally Abdullah Ally Saleh.

Shughuli za Tume hiyo zitaratibiwa na Sekretarieti ambayo Katibu wake atakuwa Ndugu Assaa Ahmad Rashid na Naibu Katibu atakuwa Ndugu Casmir Sumba Kyuki.

Mwisho.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu.

Dar es Salaam.

07 Aprili, 2012

RAIS KIKWETE AFUNGAU MKUTANO MKUU WA MWAKA WA MAAFISA WAANDAMIZI WA JESHI LA POLISI LEO MJINI MOSHI

Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiwasili Chuo cha Polisi mjini Moshi leo tayari kwa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi. Kulia kwake ni Waziri wa Mambo ya Ndani,Mh. Shamsi Vuai Nahodha na kushoto kwake ni Inspekta Jenerali wa Polisi,Saidi Mwema.

Rais Dkt. Jakaya Kikwete akizindua mojawapo ya vitabu vya muongozo wa Jeshi la Polisi wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi Chuo cha Polisi mjini Moshi leo.Kulia ni Waziri wa Mambo ya Ndani,Mh. Shamsi Vuai Nahodha wa kulia kwa Rais ni Inspekta Jenerali wa Polisi,Saidi Mwema akifuatiwa na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro,Mh. Leonidas Gama.

Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi Chuo cha Polisi mjini Moshi leo.

Sehemu ya washiriki wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi Chuo cha Polisi uliofunguliwa na Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete mjini Moshi leo.PICHA NA IKULU

 

HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA KUFUNGUA MKUTANO MKUU WA MWAKA WA MAAFISA WAANDAMIZI WA JESHI LA POLISI,

CHUO CHA POLISI MOSHI, TAREHE 06 MACHI 2012

Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi;

Inspekta Generali wa Polisi, Said Ally Mwema;

Mheshimiwa Leonidas Gama, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro;

Makamishna na Manaibu Makamishna wa Jeshi la Polisi;

Maofisa Wakuu wa Jeshi la Polisi;

Wageni waalikwa;

Mabibi na Mabwana;

Nakushukuru sana wewe Mheshimiwa Waziri pamoja na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini kwa kunialika kuja kufungua Mkutano wenu. Nakupongeza kwa dhati Mkuu wa Jeshi la Polisi na viongozi wenzako kwa kuwa na utaratibu wa kukutana kila mwaka kufanya tathmini ya shughuli zenu. Huu ni utaratibu mzuri kwa vile kila Kamanda kwa ngazi yake anatoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa sera, mikakati na mipango mbalimbali ihusuyo usalama wa raia na mali zao katika eneo lake la uongozi.

Nathubutu kusema kuwa msingeweza kuwa na utaratibu mwingine mzuri kushinda huu. Matumaini yangu ni kuwa taarifa hizo zinafanya uchambuzi wa kina wa mafanikio yaliyopatikana, kasoro zilizojitokeza na changamoto mlizokabiliana nazo na mnazoendelea kukabiliana nazo. Aidha, ni matumaini yangu kuwa mjadala unakuwa wa uwazi na ukweli na kwamba hamtaoneana muhali kuambiana ukweli kuhusu kasoro za mwenzenu pale inapostahili. Ni jambo jema na la kijasiri kujiwekea utaratibu wa kujipima wenyewe.

Mheshimiwa Waziri,

Ndugu Mkuu wa Jeshi la Polisi;

Nimefurahishwa sana na Kauli Mbiu ya mkutano wenu “Usingoje, tumia rasilimali ulizonazo kuongeza ufanisi”. Ni Kauli Mbiu muafaka inayohimiza uwajibikaji na ufanisi wa kazi kwa kuzingatia rasilimali zilizopo. Inatambua hali halisi kwamba utegemee ulichonacho kutimiza majukumu yako. Usisubiri usichokuwa nacho. Usisubiri ulichoomba au ulichoahidiwa kupata. Nawaomba mkitoka hapa mwende kwenye vituo vyenu vya kazi mkiwa mmebeba ujumbe huu mzito wa Kauli Mbiu. Mwende mkatekeleze maudhui yake kwa vitendo, kwa kushirikiana na maofisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali. Mkifanya hivi, bila shaka mtaweza kukidhi matarajio ya wananchi na hivyo kulinda heshima ya Jeshi letu la Polisi.

Ni ukweli ulio wazi kuwa sote tungetamani muwe na zana na vitendea kazi vilivyo bora, vingi vya kutosheleza mahitaji yetu. Lakini uwezo wa kifedha uliopo ni mdogo, vitu hivyo unavyovitaka hutavipata vyote kwa wakati mmoj. Hivyo basi hamna budi kuwa na subira, kupanga vipaumbele vyenu vizuri na hasa kuwa wabunifu ili kwa kutumia vifaa vilivyopo vizuri muweze kutekeleza majukumu yenu kwa kiwango cha kuridhisha.

Mheshimiwa Waziri;

Ndugu IGP,

Maafisa na Askari,

Nataka kuwahakikishia kuwa mimi na viongozi wenzangu Serikalini tunatambua umuhimu wa kuendelea kuliongezea Jeshi la Polisi uwezo wa kibajeti ili liweze kutimiza kwa ufanisi zaidi majukumu yake. IGP ni shahidi kwa kiasi gani tumeendelea kuongeza bajeti ya Jeshi la Polisi mwaka hadi mwaka. Kwa mfano, mwaka 2005 Bajeti ilikuwa Shilingi 69 bilioni na mwaka huu wa fedha zimetengwa Shilingi 134 bilioni. Nawaahidi kuwa tutaendelea kuongeza fedha kila mwaka katika miaka ijayo. Pia tumetumia uhusiano wetu na nchi rafiki kuomba misaada inayoendelea kuimarisha Jeshi letu kwa zana, mafunzo na weledi.

Napenda kutumia nafasi hii kuwapongeza Maofisa, Wakaguzi na askari wote kwa kazi kubwa na nzuri muifanyayo katika kulinda maisha na mali za raia. Nawapongeza kwa uchapakazi wenu na moyo wenu wa kujitolea na kujituma. Hakika maudhui ya Kauli Mbiu yenu ya mwaka huu mmekuwa mnayatekeleza kwa vitendo. Matokeo ya jitihada zenu yanaonekana. Mafanikio ya kutia moyo yanazidi kupatikana na sote tunayashuhudia. Mwenye macho haambiwi tazama. Uhalifu (hususan wa kutumia nguvu) unaendelea kupungua nchini kuliko ilivyokuwa miaka ya nyuma. Kulingana na takwimu za mwaka wa jana makosa makubwa ya jinai yalipungua kutoka 94,390 mwaka 2010 hadi 76,052 mwaka 2011.

Haya ni mafanikio ya kutia moyo, lakini hamna budi mtambue kuwa bado idadi ya makosa 76,052 ni kubwa mno. Hivyo bado mnayo na tunayo kazi kubwa ya kufanya mbele yenu na yetu. Inatupasa tuongeze juhudi maradufu au hata zaidi ili tupunguze kabisa uhalifu nchini.

Ndugu Makamanda,

Maofisa Waandamizi wa Polisi;

Mheshimiwa Waziri na Inspekta Generali wamezieleza vizuri changamoto zinazolikabili Jeshi la Polisi na mimi sina haja ya kuzirudia. Napenda kutumia nafasi hii kurudia kuwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kusaidiana nanyi kwa kuwawezesha ili muweze kuzikabili changamoto hizo kwa mafanikio. Tumefanya hivyo miaka iliyopita, tunafanya hivyo hivi sasa na tutafanya hivyo miaka ijayo.

Tutaendelea kuliwezesha Jeshi la Polisi kifedha ili muweze kutekeleza ipasavyo majukumu yenu. Tutaendelea kuwawezesha muongeze idadi ya askari. Tutawawezesha mpate vyombo vya usafiri, zana na vitendea kazi vya kisasa vya kufanyia kazi za kukabiliana na uhalifu. Kazi ya kulipatia Jeshi la Polisi zana na vifaa vipya vya kazi inaendelea ikiwa ni sehemu ya Programu ya Maboresho ya Jeshi la Polisi. Nawahakikishia kuwa tutaendelea kutoa fedha za kutekeleza Programu hiyo na shughuli nyingine za Jeshi la Polisi.

Tutaendelea kuwawezesha katika kuboresha mafunzo ya askari na maafisa wa Jeshi la Polisi. Natambua mahitaji ya kuviboresha vyuo vilivyopo sasa. Panapohitaji kukarabati pakarabatiwe na panapotakiwa ujenzi wa majengo mapya yajengwe. Na panapotakiwa kuanzishwa chuo kipya kianzishwe. Hatuna budi kuwekeza katika mafunzo kwani mafunzo ni msingi mzuri wa weledi na kuwa na askari wenye tabia na mwenendo mwema. Kupata zana za kisasa za upelelezi na kudhibiti uhalifu pekee hazitoshi kama zitakuwa mikononi mwa askari asiyejua kitu, asiyekuwa na nidhamu na utiifu. Kufanya hivyo kunalihakikishia Jeshi uwezo wa kutimiza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa na kuleta sifa kwa Jeshi la Polisi Tanzania.

Dunia imebadilika, Tanzania imebadilika na mbinu za uhalifu na aina za uhalifu yamebadilika. Pia, mbinu, mikakati na maarifa ya kukabiliana na uhalifu, nayo yamebadilika duniani. Lazima tusisitize mafunzo, kwani ndiyo msingi wa weledi na ufanisi. Mafunzo ndiyo njia ya kuwawezesha askari na maofisa wa Jeshi la Polisi kupata elimu na maarifa mapya kuhusu uhalifu na namna ya kukabiliana nao. Mafunzo ndiyo yatakayowezesha kuelewa zana na vifaa vipya vya kupambana na uhalifu na kujua namna ya kuvitumia. Hakuna badala ya mafunzo.

Mheshimiwa Waziri,

Ndugu Inspekta Jenerali,

Maofisa,

Wakaguzi na Askari;

Mimi na wenzangu katika Serikali tunatambua umuhimu wa kuboresha maslahi ya maofisa na askari wa Jeshi la Polisi pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi na kuishi. Mara baada ya kuchaguliwa mwaka 2005, nilipotembelea Makao Makuu ya Jeshi la Polisi na baadhi ya kambi nilijifunza mengi kuhusu hali ya maslahi na mazingira ya kazi na malazi ya wanajeshi wetu. Baada ya hapo tulianza kuyachukulia hatua mambo hayo na tumekuwa tunaendelea kufanya hivyo hadi sasa. Tumeboresha maslahi kwa kiasi chake na bado tunaendelea. Tumeanza ujenzi wa nyumba bora za kuishi na bado tunaendelea na mpango huo.

Napenda kurudia kuwahakikishia kuwa kwangu na wenzangu Serikalini, hakuna upungufu wa dhamira ya kuboresha na kuimarisha Jeshi la Polisi nchini kwa maana ya idadi, mafunzo, vitendea kazi, maslahi na mazingira ya kuishi. Kinachotutatiza ni uwezo wa kifedha wa Serikali ambao si mkubwa sana kuweza kumudu sawia mahitaji yote ya kugharamia shughuli zote za Serikali na Taifa. Pamoja na changamoto hizo, bado tumeendela kuthubutu kuchukua hatua na kwa haya tuliyoweza kufanya kwa upande wa Jeshi la Polisi si haba. Tunaendelea.

Mheshimiwa Waziri,

Ndugu IGP;

Sina budi kuelezea furaha yangu na pongezi za dhati kwako IGP, Makamishna walioko Makao Makuu ya Polisi pamoja na Makamanda wa ngazi mbalimbali kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana kutokana na rasilimali iliyopo. Huu ni uthibitisho wa uongozi wako makini ukishirikiana na viongozi wa ngazi mbalimbali wa Jeshi letu. Hakika Kauli Mbiu ya mwaka huu kwenu si jambo geni hivyo tunategemea kuona mafanikio makubwa zaidi miaka ijayo. Aidha, mnanipa moyo kuwa hapo rasilimali zitakapoongezeka Jeshi la Polisi litastawi sana.

Usalama Barabarani

Mheshimiwa Waziri,

Inspekta Generali wa Polisi,

Ndugu Makamanda;

Napenda kutumia nafasi hii kurudia maombi yangu kwenu kuimarisha usimamizi wa usalama barabarani. Ajali za barabarani zimezidi mno, hatuna budi kuzizuia zisizidi kuongezeka. Tufanye kila tuwezalo zipungue. Nawaomba mtumie fursa ya mkutano wenu huu kujadili tatizo hili kwa marefu na mapana yake na mkubaliane juu ya nini cha kufanya. Naamini mtaweza.

Nawaomba jambo hili mlipe uzito unaostahili kabla halijageuka kuwa janga la kitaifa. Ukweli kwamba katika kipindi cha Januari hadi Desemba mwaka juzi (2010) jumla ya watu 3,687 walipoteza maisha kutokana na ajali za barabarani. Mwaka na jana (2011) katika kipindi hicho hicho idadi hiyo iliongezeka na kufikia watu 4,013. Hili si ongezeko dogo inatulazimu kushtuka na kuchukua hatua. Nafahamu dhana ya kuwianisha kuongezeka kwa ajali na kuongezeka kwa pikipiki na magari na hali ya barabara zetu. Hata hivyo hivi visiwe visingizio vya kuona kuongezeka kwa ajali za barabarani ni jambo la kawaida. Tuseme ukweli kuwa ajali nyingi zinasababishwa na uzembe wa madereva kutokuheshimu Sheria ya Usalama Barabarani na ubovu wa vyombo vya usafiri. Kwa sababu zote hizi mbili Jeshi la Polisi lina wajibu maalum kukabiliana nazo. Tafadhali timizeni ipasavyo wajibu wenu. Mkajipange vizuri, kwa kushirikiana na Idara nyingine husika za Serikali, ili ajali na vifo viweze kupungua.

Madereva wazembe, walevi na wasiotaka kufuata Sheria na Kanuni za usalama barabarani wachukuliwe hatua kali. Wakati umefika madereva wakaidi wanyang’anywe leseni zao ili wasihatarishe tena maisha ya Watanzania. Najua haiwezekani kukomesha kabisa ajali za barabarani, lakini naamini kuzipunguza inawezekana. Endapo kuna msaada mnahitaji au jambo mnataka kutoka kwetu, tuambieni. Kama mnadhani Sheria ya Usalama Barabarani na Kanuni zake zinahitaji marekebisho, tuleteeni mapendekezo yenu tuyafanyie kazi. Au kama mnaona kuna mapungufu katika mfumo wa kitaasisi uliopo, msisite kutushauri na sisi tutaangalia namna ya kurekebisha.

Mheshimiwa Waziri,

Ndugu IGP,

Makamanda, Maafisa na Askari,

Jambo lingine ninalopenda mlizungumze kwa kina na mkubaliane katika Jeshi letu ni juu ya hatua za kuchukua dhidi ya tuhuma za kuenea kwa vitendo vya rushwa katika Jeshi la Polisi. Najua mnajitahidi lakini bado ni hisia ya muda mrefu ya wananchi na haionekani kubadilika. Utafiti unaofanywa na taasisi zinazojihusisha na masuala ya utawala bora kuhusu rushwa bado zinalinyooshea kidole chombo chetu hiki muhimu sana cha dola. Natamani sana hisia na taarifa hizo ingekuwa hazina chembe ya ukweli lakini, bahati mbaya huo ndio mtazamo wa jamii na inaelezea wakati mwingine kwa nini baadhi ya wananchi huchukua sheria mikononi mwao.

Pamoja na kuwepo kwa hisia hizo mimi naamini wapo Polisi wengi wazuri na kwamba hali haijafikia kusema imeshindikana kupambana na kukomesha vitendo vya rushwa katika Jeshi la Polisi. Penye nia pana njia. Tafadhali sana tieni nia ya dhati kupambana na tatizo hili na kushinda. Watambueni wale wenzenu miongoni mwenu wenye tabia ya kuomba kitu kidogo muwawajibishe ipasavyo kwa adhabu zinazostahili. Hawa ni watu wanaosaidia wahalifu wasibanwe na mkono wa sheria hivyo ni kikwazo kwa Jeshi la Polisi kutimiza ipasavyo wajibu wake wa msingi wa kupambana na uhalifu. Waondoeni katika Jeshi kwani wanaharibu sifa yenu nzuri na kudhoofisha Chombo chetu.

Mheshimiwa Waziri,

Ndugu IGP,

Ndugu Makamishna,

Maofisa Waandamizi wa Polisi;

Mabibi na Mabwana;

Yamekuwapo malalamiko mengi ya ukiukwaji wa haki za binadamu yanayoelekezwa kwa Jeshi letu la Polisi katika utendaji kazi. Taarifa za kila mwaka zinazotolewa na Tume ya Haki za Binadamu na taasisi nyingine mbalimbali za Kitaifa na Kimataifa zimekuwa zikionesha hivyo. Yapo pia madai ya watu kunyanyaswa na Polisi kwa kukamatwa bila makosa, kubambikiwa makosa, kuteswa wakiwa mahabusu na hata kuuliwa. Kuna madai ya Polisi kutumia nguvu kupita kiasi na hata kusababisha vifo ya raia.

Nawaomba mtumie fursa ya mkutano huu myazungumze madai hayo na kuamua hatua zipasazo za kuchukua. Natambua kuwa katika Programu ya Maboresho ya Jeshi kuwaelimisha wanajeshi wetu kuhusu masuala ya haki za binadamu ni moja ya mambo yaliyopewa kipaumbele. Nawaomba mtekeleze dhamira yenu hii njema kwa kasi zaidi ili katika kipindi kifupi muwafikie Polisi wetu wote. Aidha, mafunzo kuhusu haki za binadamu yawemo katika mitaala ya vyuo vyetu hapa CCP, Police College – Kurasini na Chuo cha Maafisa Wakuu Kidatu.

Aidha, Jeshi liweke utaratibu mzuri na unaoeleweka wa kupokea na kufanyia kazi malalamiko au maoni yanayopelekwa kwao na wananchi.

Ni muhimu kwa Jeshi la Polisi kusisitiza na kusimamia kwa dhati nidhamu ya maofisa na askari wake. Nidhamu ni sifa ya msingi ya askari. Askari asiye na nidhamu amepoteza sifa ya kuendelea kuwa mwanajeshi. Ni hatari sana kwa usalama wa raia na anaharibu sifa ya Jeshi. Vitendo vya utovu wa nidhamu vinavyofanywa na baadhi ya maofisa na askari kamwe visivumiliwe. Hivi majuzi nimesikia kuwa hapa Moshi askari ametoroka lindo na kwenda disco, tena akiwa na silaha! Vitendo vya namna hii vinaleta fedheha kwa Jeshi la Polisi na kuwaacha watu wakishangaa na kuwa na maswali mengi juu ya Jeshi lao. Inawezekanaje ifikie hapo kwa askari aliyefunzwa vizuri.

Nawaomba mzingatie upya taratibu zenu za ajira. Wakati umefika wa kuwepo na utaratibu mzuri wa upekuzi wa vijana kabla ya kuteuliwa kusomea kazi ya Polisi. Pawepo na utaratibu thabiti na kufuatilia mienendo ya askari wakati wote wa utumishi wao. Majeshi mengine yanafanya hivyo. Kufanya hivyo kutasaidia kupata vijana walio safi kwa tabia na mwenendo kuajiriwa na kuendelea na utumishi katika Jeshi la Polisi. Kwa ajili hiyo tutakuwa na askari walio watiifu, waaminifu, wachapa kazi hodari na kuliletea sifa Jeshi letu.

Mwisho

Mheshimiwa Waziri,

Inspekta Generali,

Makamanda wa Polisi;

Kabla ya kumaliza hotuba yangu napenda kurudia kutoa pongezi za dhati kwa kazi kubwa na nzuri muifanyayo pamoja na changamoto mbalimbali mnazokabiliana nazo. Nawapongeza sana kwa kubuni utaratibu wa Polisi Jamii ambao ni mfano mzuri wa ubunifu wa kutumia rasilimali zilizopo. Tafadhali uimarisheni na kuuboresha utaratibu huu mzuri. Sisi katika Serikali tutafanya kila linalowezekana kuongeza rasilimali kwa Jeshi la Polisi ili kuliwezesha kukabiliana na uhalifu nchini. Nawaomba mkumbuke na kuzingatia ukweli kwamba katika kila hatua mnayopiga, sisi Serikalini na taifa zima kwa ujumla tutakuwa pamoja nanyi kuwapa moyo na kuwaunga mkono kwa rasilimali muhimu.

Ndugu Inspekta Jenerali,

Makamanda wa Mikoa na Vikosi,

Mabibi na Mabwana,

Baada ya kusema hayo, ninayo furaha sasa kutamka kwamba, Mkutano Mkuu wa Mwaka 2012 wa Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi umefunguliwa rasmi. Nawatakia mkutano mwema, mazungumzo yenye ufanisi na matokeo mazuri.

“Ahsanteni kwa kunisikiliza”

RAIS KIKWETE AWASILI MKOANI KILIMANJARO KWA ZIARA YA KIKAZI YA SIKU TATU

 Viongozi wa Kitaifa na wa Mkoa wa Kilimanjaro wakimsubiri Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ashuke kwenye ndege katika uwanja wa Kilimanjaro International Airport tayari  kwa ziara ya kikazi ya siku tatu ya mkoa huo.

Miongoni mwa shughuli ambazo Mheshimiwa Rais atafanya ni pamoja na kuzindua kampeni ya kupinga ukatili na matumizi ya nguvu dhidi ya wanawake ambayo ataizindua kwa kuanzisha safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro iliyopewa jina la “Kilimanjaro Speak Out, Climb Up”.
Shughuli hiyo itakayofanyika kesho Jumatatu, Machi 5, 2012 asubuhi, imepangwa kwenye Lango la Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA)
Mbali na kuanzisha kampeni hiyo, Mhe Rais pia atafungua Mkutano wa Mwaka wa Maofisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi unaofanyika kwenye Chuo cha Polisi mjini Moshi.
Hii ni ziara ya kwanza ya Mhe Rais Kikwete katika Mkoa wa Kilimanjaro tokea alipotembelea Mkoa huo wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
 Rais Kikwete akisalimiana na viongozi wa kada mbalimbali wa Kilimanjaro
 Rais Kikwete akiangalia burudani za ngoma
 Rais Kikwete akiwa ameongozana na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mh Leonidas Gama
 Rais Kikwete akisalimiana na wananchi wa Kilimanjaro waliofika kumlaki
 Rais akiendelea kusalimiana na wananchi wa kilimanjaro
 Kinamama wamejitokeza kwa wingi kumlaki
 Karibu Kilimanjaro….
 Ngoma za kiasili zikimtumbuiza wageni
 Msafara umewasili Ikulu ndogo ya Moshi, sasa ni utambulisho kabla ya breafing
 Kamati ya Ulinzi na Usalama
 Wakuu wa Wilaya za mkoa wa Kilimanjaro
 Viongozi wa taasisi mbalimbali katika kikao cha breafing
 Kikao kinaendelea
 Viongozi wa mkoa wa taasisi na idara mbalimbali
 Viongozi katika kikao hicho
 Wazee wa mji wa Moshi
 Wazee wa Moshi
 Kada mbalimbali za mkoa wa Kilimanjaro katika kikao hicho
 Mkuu wa Mkoa wa Kiliman jaro akitoa maelezo ya mkoa
 Kiongozi wa idara ya afya ya Mkoa akitoa maelezo yake 
 Taarifa ya elimu
 Taarifa ya hali ya mifugo
Waziri wa Maendeleo ya jamii, Jinsia na Watoto Mh.Sophia Simba akitoa taarifa ya maandalizi ya kampeni ya kupinga ukatili na matumizi ya nguvu dhidi ya wanawake ambayo Rais Kikwete leo asubuhi ataizindua kwa kuanzisha safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro iliyopewa jina la “Kilimanjaro Speak Out, Climb Up”.